TUNGO ZA Binmasika

TUNGO ZA Binmasika Karibuni kwenye ukurasa huu wapenzi wa Lugha ya Kiaswahili.

Tungo za Binmasika ni mkusanyiko wa mashairi yaliyotungwa kwa minajili ya visa vilivyofanyika, vinavyofanyika vina vyokisiwa kufanyika siku za usoni.

06/01/2018

Vijana wa siku hizi hawachagui uwanja, yaweza kua mvunguni ama juu ya Dari -Platinumz

18/11/2017

Damu ya mtu hainenepeshi- mbu, chawa na wengine wangenenepa, acheni kutafuta damu ya watu. -Walah bin Walah

18/10/2016

SIFI MOYO

Siku nyingi sijanena, mengi nimeshuhudia,
Nitasema sitabana, upeo kuufikia,
Mateso sitakana, kila mja hupitia,
Sifi moyo mimi bwana, mola anifikiria,

Kila swala shatimiza, ka sheria sijavunja,
Kwanini naona kiza, cha mwenzangu sijapunja,
Mawazo najipokeza, jameni nipe ujanja,
Moyo Wangu kuuliza, nnyota yangu kuikunja,

Njozi njema nishaota, tangia jadi hadi sasa,
Nitakacho sijapata, haki yangu nimekosa,
Panda shuka k**a vita, kilio changu napasa,
Matatizo yatapita, machozi nayapangusa,

Moyo nisipige konde, mateso yakuza wazo,
Nafsi nisiiponde, tena natia mkazo,
Nakaza nishike tende, kejeli ni hamnazo,
Vya bwerere nisipende, nisije jitia bezo,

Nahapa sifi moyo, hakika nitala mbivu,
Mtima usiwe na choyo, kabisa tema uvivu,
Nazidi fuata nyayo, nitoroke na maovu,
Niepuke na miayo, niepushe na makovu,

Nashukuru kwa kidogo, nikikosa sifukuru,
Wala mimi si kigogo, sijigambi ja kifaru,
Siachi sukuma gogo, bidii ya mbeberu,
Moyo tuliza mapigo, natazamia uhuru,

Nisije chagua kazi, cha mno kiwe riziki,
Nipunguze usingizi, niotacho niafiki,
Ustaarabu uwe kozi, kisirani sikitaki,
Na mwishoe kwa mapozi, nitapata yangu haki,

Jappio naona mwangaza, sitakoma na kusali,
Majibu yanishangaza, kukicha Napata hali,
Sifi moyo napongeza, panua zangu akili
Kalamu naikatiza, labda kuwe na swali

16/01/2014

HAKI – MSINGI BORA_ 6TH November, 2013

Haki zetu kikatiba, nguzo kidemokrasia,
Uhuru usio haba, usawa wa kijinsia,
Mombasa au Malaba, uhuru wa kutembea,
Haki zetu ndo’ msingi, hutuepusha dhuluma,

Kutuepusha dhuluma, adhabu zisizofaa,
Tusitendewe unyama, habari kutufikia,
Daima kuwe heshima, itikadi kukolea,
Haki zetu ndo’ msingi, Vijana kuwajalia,

Tuwajalie Vijana, tuwapeni na masomo,
Uchumi kuinuana, ajira iwe mfumo,
Siasa zenye maana, husika pasi kikomo,
Haki zetu ndo’ msingi, hata k**a ni wafungwa,

Wafungwa kufahamishwa, kifungu kikamilifu,
Na wakili kuonyeshwa, wala pingu si mkufu,
Hukumu bora kupishwa, asije akawa mfu,
Haki zetu ndo’ msingi, sisahau wanunuzi,

Usawa kwa wanunuzi, bidhaa bora kupewa,
Bei nazo ziwe wazi, afya njema kufikiwa,
Usalama uwe kozi, na hasara kufidiwa,
Haki zetu ndo’ msingi, jamii kuheshimiwa,

Kuiheshimu jamii, tekeleza tamaduni,
Kujiunga na vikundi, utulivu maskani,
Mila zilizokamili, milele shikilieni,
Haki zetu ndo’ msingi, kuilinda familia,

Heshima kwa familia, nayo asasi ya ndoa,
Amani kufurahia, usawa wa kijinsia,
Watoto nao kulea, ukatili kuondoa,
Haki zetu ndo’ msingi, kusiwe na ukabila,

Tumia lugha yoyote, ni haki ya kila mja,
Makaazi jenga kote, na wala kusiwe njaa,
Maji safi kwetu wote,matibabu ni ya haja,
Haki zetu ndo’ msingi, hongera wafanyikazi,

Tujali wafanyikazi,wao wakuza uchumi,
Miungano natuenzi, mishahara ya usomi,
Hali njema za kikazi, kugoma pasi uvumi,
Haki zetu ndo’ msingi, tuilinde raslimali.

Kuilinda raslimali, jukumu la serikali,
Miliki yoyote mali, popote pale pahali,
Mali iwe ya halali, ukiweza inakili,
Haki zetu ndo’ msingi, siasa zenye kujenga,

Tujiunge navyo vyama, kisha vipigie debe,
Kuwania nako vyema, onyesha wako ubabe,
Uchaguzi wa salama, nchi iliyo na shibe,
Haki zetu ndo’ msingi, turuhusu na habari,

Habari zilizohuru, na zisizoegemea,
Uchochezi tuuguru, uzalendo kufikia,
Nchi yetu Kenya huru, tujenge demokrasia,
Haki zetu ndo’ msingi, waziwazi kuwe haki.

08/11/2013

UONGOZI ADILIFU
Naomba mzingatie, kilio kiwafikie,
Maoni niwapatie, adili tushikilie,
Majigambo sijitie, dharau tufutilie,
Uongozi maadili, hung’aa k**a dheluji,

Hung’aa k**a dheluji, kila mja huvutiwa,
Kuwe uwajibikaji, uzembe kuondolewa,
Kwa wengine ni kipaji, hupata katunikiwa,
Uongozi maadili, Maulana hutunuku,

Hutunuku Maulana, si sifa kusingiziwa,
Kwa heshima kupatana, katiba kuzingatiwa,
Pasiwepo kugawana, wananchi haki kupewa,
Uongozi maadili, kusiwe na ubinafsi,

Ubinafsi kuondoa, mfanowe ni mzazi,
Busara ilokolea, ari ya usaidizi,
Kabila wala jinsia, katu si pingamizi
Uongozi maadili, nguzo bora aushini,

Nguzo bora aushini, uhuru wa kujadili,
Mwenye pendo mtimani, kulinda raslimali,
Hakimbilii mitini, iwapo hukuna hali,
Uongozi maadili, kuenzi maendeleo,

Huenzi maendeleo, mfano kwa wafuasi,
Kuondolewa tishio, mipango ya ufanisi
Hulifungua sikio, kwa vilio vyao insi,
Uongozi maadili, kamwe kusiwe matusi,

Kujitenga na matusi, kinywa kilichosafishwa,
Kusiwe ila ya fisi, ufisadi kukomeshwa,
Mwendo wake ni wa kasi, k**a kosa kusafishwa,
Uongozi maadili, kuzitimiza ahadi,

Ahadi huleta deni, kulipa ni taadhima,
Amani na isheheni, uwazi kwayo umma,
Ujasiri afisini, utendakazi kupima,
Uongozi maadili, aliyoagiza mola,

Rabuka ashaagiza, lilobaki tutimize,
Kutolewa kwenye giza, kizazi chema tukuze,
Tuishi kwenye mwangaza, kwa hekima tuongoze,
Uongozi maadili, mapenzi kwa watu wote,

Mapenzi kwa watu wote, pasipo kubaguana,
Asimamaye kidete, lengo lake bayana,
Suluhu nayo tupate, pasiwepo kugombana
Uongozi maadili, jifunze kunyenyekea,

Kiongozi kunyenyekea, hutizama atokako,
Daraja yeye huvuka, pindi alifikiaopo,
‘Vumilivu mbivu hula, hutimiza haja yako,
Uongozi maadili, la ziada mimi sina,

Sina mimi la ziada, naombea uongozi,
Tuondoe sote shida, maadili yawe vasi,
Lilobaki kwetu ada, kutimiza hii njozi,
Uongozi maadili, Kheri njema viongozi.

30/10/2013

PENZI LIMEISHA
Sitaki kupenda tena, bayana naweka wazi,
Na hisia mimi sina, nakana tena siwezi,
Lijapo hodi hapana, penzi ni k**a jambazi,
Ondoka kidosho nenda, penzi langu limeisha,

Langu penzi limeisha, sidhubutu rudi nyuma,
‘metosha nivokulisha, kukutunza nimekoma,
Kwa kweli ulinichosha, ku’miza wangu mtima,
Vitisho ulonitisha, nikiwa mimi mfungwa,

Sitaki kuwa mfungwa, nikiwa mwangu nyumbani,
Kwa machozi ukasongwa, uzuwapo kisirani,
Lako domo lilichongwa, matusi kuwa mbeleni
‘kahapa kutosikiza, dharau kunipokeza,

Kanipokeza dharau, langu jibu ni talaka,
Kashindwa tuliza kiu, himahima ukataka,
Nimepiga yangu mbiu, matesoni nimetoka,
Leo hii niko huru, pingu kuzitupilia,

Pingu kuzitupilia, wenzangu kutangamana,
Muda najipatilia, pasipo na kugombana,
Upeo nimefikia, masharti kushikana,
Najihisi ni mwepesi, mfanowe mbayuwayu,

Wepesi ni mbayuwayu, hali naipendelea,
Kanenepa k**a mbuyu, wenzako kushangilia,
Kanirushia vibuyu, ukawa kiruka njia,
Niache sina nafasi, sitamani kwenda nawe,

Sitaki niende nawe, na wala hatufaani,
Utakacho na upewe, wenzangu mjitwikeni,
Wa msaada usiwe, upweke niachieni,
K**a huko ndo’ kupenda, nitazoea ukiwa,

Kwa kheri ya kuonana, na wala tusijuane,
Iwapo tumetoshana, mitaani tupatane,
Ulimwengu u mpana, jaribu mfukuzane,
Nafasi nyuma hapana, iwapo ni ya mwingine.

22/10/2013

Kwa wale waliochoshwa na maswala ya mapenzi, lenu li jikoni, subira huvuta heri.

19/08/2013

LEO NAASI POMBE_21 JULAI 2013.
Ni mengi nimeshaona, leo hii kuamua, pombe siitaki tena, wenzangu nisikizeni,
Wazazi wameshanena, mvinyo kuondokea, leo hii ninakana, nawasihi nipateni,
Vigumu haya kuona, jaribu kufikiria, hu’tojua hata kona, kuanguka matopeni,
K**a tawi kwenye shina, hutoweza achilia, mengi kwangu kuyabana, kupotezea mapeni,

Nilianza kwa kuonja, ndo’ shida kujitakia, nisiweze kufahamu, ni shimo kujichimbia,
Kapatana na wanjanja, sungura hato’fikia, onja upate utamu, ushauri kuufwata,
Pole pole k**a panja, upeo nikafikia, moja mbili kila zamu, chupa kuzifungulia,
Wala Dada sio wanja, urembo kujipakia, punde kapata wazimu, chakari kupindukia,

Baadaye ‘kawa sugu, wenzangu kuwazomea, njia zote kuzijua, sikutaka la mwadhini,
Nikazidi kuwa pwagu, kipitacho kumezea, gizani hata kwa jua, ‘kuhepa’ msikitini,
Chakula kikawa njugu, pombe kuteremushia, haya yote sikujua, kulala miferejini,
Kupitia kwenye gugu, soni nimeshajitia, lilobaki nilojua, ni ulevi vijijini,

Sikufika maskani, nifikapo ni bahati, kurauka ni dosari, Afisini kuchelewa,
Maruwe ruwe kichwani, kuchanika langu shati, kusiwe lolote shwari, umeachwa kwa ukiwa,
Siendi tena pombeni, nishasema hunipati, mvinyo basi kwaheri, kulewa sio kipawa,
Nipitapo mitaani, langu jina mada nyeti, wala kusiwe na siri, yaso kweli kunenewa,

‘batili hisia zako, na chafu ikawa safi, wabaya huwa warembo, kila bovu huwa zuri,
Wangu atakuwa wako, utadhani huyu hafi, utasifu liso pambo, hutaki hata habari,
,sitambue ulioko, ovyo kuzabwa makofi, sababu ikiwa tembo, maisha kuyajasiri,
Nimeonya tena siko, nimekiri kwake wifi, mfano bora wa tambo, kaka hima jinawiri,

Kahofu uhai wangu, kupokonywa kila mara, nikaporwa yangu mali, kukawa sintofahamu,
Naondoka kwenye wingu, uwamuzi wa imara, nikamusihi jalali, mola bora nirehemu,
Kwako ninatoa fungu, ninatoa na kafara, niepushe hii hali, amani kwangu idumu,
Kaka njoo wanguwangu, tuepuke ufukara, karibuni tujadili, tuepukeni hukumu.

20/07/2013

KIPENZI CLARE

Kwako mimi nimedata, kupinga hatutoweza,
Nashukuru kukupata, kila mara kukuwaza,
Kukupenda sitosita, sitokoma kueleza
Kipenzi changu Clare, wewe ni wangu mchumba,

Wewe ni wangu mchumba, kwingineko sitoenda,
Waambao washaamba, k**a shida tutashinda,
Iwe rege hata rhumba, hapo kwako nitarinda,
Kipenzi changu Clare, penzi langu shaliiba,

Penzi langu shaliiba, mwenzi wako simuwazi,
Sio mama wala baba, watopinga letu penzi,
Kwa kweli penzi mahaba, basi letu tulienzi,
Kipenzi changu Clare, usije niacha mimi,

Usije niacha mimi, dosari kwa maulana,
Mombasa hata miami, ulimwengu kila kona,
Utunzi wangu msomi, naamini twatoshana,
Kipenzi changu Clare, usinidhuru mtima,

Usinidhuru mtima, kunipokeza kiwewe,
Nilikupenda mapema, ujuavyo hata wewe,
Ndio maana nasema, sifazo basi upewe,
Kipenzi changu Clare, wanichanganya kipusa

Wanichanganya mrembo, macho unavyorembua
Malaika una chombo, kifuacho cha sumbua,
Mbeleni una mtambo, busulo lanizingua,
Kipenzi changu Clare, fanya hima nionjeshe,

Fanya hima nionjeshe, kalamu naiondoa,
Wazimu unishikishe, kwangu mimi huna doa,
Joto lako unipashe, uwoga wako ondoa,
Kipenzi changu Clare, tamati nimefikia

14/07/2013

OMBI HUJIBIWA-13/12/2010
Kwa kweli uchanga raha, ukubwa naona ta’bu,
Kilemba namvulia, alonena hayo babu,
Zama zile tulijazwa, maono ja vitabu,
Letu swali lilobaki, tajibiwa langu ombi,

Nawasihi mfahamu, hatuoni jibu waja,
Maulana mkarimu,huzidisha ulotaja,
Tafsirini wenzangu, shukrani ni ya haja,
Letu swali lilobaki, tajibiwa langu ombi,

Ukweli leo shapata, zingatia langu guni,
Mahitaji kishapata, hayaishi duniani,
Mkwasi naye hutaka, chake kapu si pomoni,
Letu swali lilobaki, tajibiwa langu ombi,

Adinasi hujaliwa, ila tu kwacho kiasi,
Lolote lakubaliwa, dhamini ya almasi,
Wakati huu elewa, omba chako kwayo kiasi,
Letu swali lilobaki tajibiwa langu ombi,

Lako tajibiwa ombi, Mola si athumani,
Tusije fuata wimbi, shaurilo fuateni,
Amka sipige kambi, ulikotoka kunani,
Letu swali lilobaki, tajibiwa langu ombi,

Omba kisha nyenyekea, tizamia utokako,
Daraja basi huvukwa, pindi ulifikiapo,
‘vumilivu bivu hula, ombea kiwango chako,
Letu swali lilobaki, tajibiwa langu ombi,

La ziada hamnalo, tamati nishafikia,
Shukrani tuwe nayo, pupa usishikilia,
Shauri tushike hilo, Mola tatuzidishia
Leo hii natuombe, kesho sema shukrani.

13/07/2013

DADA MPENDWA-DISEMBA 2011
Jameni nielezeje, lo! Siamini Challote,
Kwanini umetoka nje, simanzi ‘metanda kote,
Ningependa nami nije, dadangu tuwe sote,
Mapema dada mapema, tulitaka kuwa nawe,

Tulitaka kuwa nawe, kilio hiki cha wengi,
Dunia hamna shangwe, mateso mithili shungi,
Kifo aina ya jiwe, hakiongwi kwa shilingi,
Mapema dada mapema, yalobaki ni majonzi,

Yalobaki ni majonzi, ardhi yatumaliza,
Si mamangu si shanganzi, haya kweli yashangaza,
Mauti yana chokozi, yamehapa kuchokoza,
Mapema dada mapema, machozi yabubujika,

Machozi yabubujika, nikumbukapo wachanga,
Uyatima hujatoka, unakata ja upanga,
Hi’ sasa twaongezeka, utadhani ni mchanga,
Mapema dada mapema, ulikuwa wa muhimu,
Ulikuwa wa muhimu, mfano bora wa mama,
Mawazo yako timamu, sifa zako zinavuma,
Pendo lako kweli tamu, sas lote limehama,
Mapema dada mapema, laiti tungelijua,

Laiti tungelijua, uhai sio bidhaa,
Kuondelewa ukiwa, sharti tungenunua,
K**a pesa tungepewa, mama Beti ashalia,
Mapema dada mapema, pigo kubwa kwake Baba,

Pigo kubwa kwake baba, alikuombea bora,
Kweli alitoa toba, mjini na hata bara,
’ngetia zote mkoba, uhai ngekuwa kura,
Mapema dada mapema, kwetu ni sintofahamu,

Sintofahamu ‘tujia, Dada Dory akasema,
Shikuku kashindwa lia, amebaki ni kuhema,
Robai kashikilia, dunia kweli si pema,
Mapema dada mapema, asemaje sasa Gabu,

Gabu atasema nini, muulizeni Angela,
Amepoteza mwendani, pendo lake ashalila,
Ndugu tushikilieni, shauri lake Wanjala,
Mapema dada mapema, kutuachia Mercy,

Mercy pamoja Sheila, usisahau Sharoni,
Mpwa chatumbo kula, baraka ni yetu Dani,
Sote tushukuru mola, Brayo Vale na Vivian,
Mapema dada mapema, salimu ndugu Joshua,

Iwapo ni matibabu, kifo hakina adabu,
Mapeni kuyaharibu, Baba ajua sababu,
Matabibu walitibu, tuombeni na kwa babu,
Mapema dada mapema, Mungu nawe tuzawabu,

Mwachieni Maulana, Mwenyezi mwenye uweza,
Ushikwapo shik**ana, basi na haya sikiza,
Tumrudie Rabuka, anaweza kututuza,
Tushikeni lake jina, Yeye ni wetu Rabana.

13/07/2013

KATIBA KENYA-JULAI-AGOSTI 2010
Nchi yetu Kenya huru, istahili pongezi,
Historia tukizuru, sifa kwa wasimamizi,
Basi haya tukiguru, katiba kita mizizi,
Katiba yetu wakenya, sio mja binafsi,

Hisibati ni miongo, takribani minne,
Mbeberu mtu mwongo, nipe nafasi ninene,
Mwafrika siwe chongo, fungua jicho uone
Katiba yetu wakenya, sio mja binafsi,

Mwamba ngo’ huvuta kwao, wakale walishanena,
Sheria watunga wao, kidete haya nakana,
Kura tupige Ndio, rukaruka ng’o hamna,
Katiba yetu wakenya, sio mja binafsi,

Heshima kwa viongozi, kitu bure cha hiari,
Kibaki, Raila wazazi, ongoza vema safari,
Kipindicho kwenu wazi, pamoja hebu fikiri,
Katiba yetu wakenya, sio mja binafsi,

Kabila na chuki kando, haki ndio mwendo bora,
Wajir au Kajiado, ’kenya acha kutupora,
Bonde la ufa langu do! Nani kakupa hadhira,
Katiba yetu wakenya, sio mja binafsi,

Hamna zu lisilo doa, sha semwa natuafiki,
Tujenge demokrasia, waziwazi kuwe haki,
Chanda chema pete vikwa, puuza ovyo rafiki
Katiba yetu wakenya, sio mja binafsi.

Address

2757
Kitale
30200

Telephone

+254729623757

Website

Alerts

Be the first to know and let us send you an email when TUNGO ZA Binmasika posts news and promotions. Your email address will not be used for any other purpose, and you can unsubscribe at any time.

Share

Category