16/03/2026
🌿Kupitia Mkutano wa Business of Conservation conference Bcc 2026 iliyofanyika Nairobi Kenya , Mafunzo muhimu kutoka kwa Mtendaji Mkuu wa Jumuiya ya Randilen WMA ni;
Jumuiya ya Hifadhi ya Wanyamapori Randilen (Randilen Wildlife Management Area) imekuwa mfano mzuri wa uhifadhi unaoongozwa na jamii.
Kupitia mpango wa nyanda za malisho (grass banks), takribani 95% ya wafugaji kutoka vijiji wanachama wananufaika kwa kupata maeneo ya malisho. Aidha, mapato yatokanayo na utalii yanaelekezwa katika maendeleo ya vijiji na shughuli za uhifadhi wa eneo, jambo linaloonyesha jinsi uhifadhi unavyoweza kuleta manufaa ya moja kwa moja kwa jamii.
Randilen pia imechangia kuimarisha usalama wa ardhi kwa kusaidia kurejesha ardhi iliyokuwa imechukuliwa na watu binafsi na kuirudisha kwa manufaa ya jamii nzima, pamoja na kusaidia kutatua migogoro ya ardhi na Hifadhi ya Taifa ya Tarangire ambapo takribani ekari 11,160 zilirejeshwa baada mipaka kubainishwa.
Vilevile, juhudi za kupunguza migogoro kati ya binadamu na wanyamapori zimeimarishwa kupitia hatua mbalimbali za kukabiliana na tembo wanaoharibu mazao ya wakulima.
Kwa upande wa maendeleo ya jamii, fursa za ajira na kujiajiri zimeongezeka kupitia miradi k**a Kituo cha Utamaduni cha Wanawake cha Enaboishu.
Wakati huo huo, kikao kilisisitiza umuhimu wa utawala bora kwa kuimarisha mifumo ya usimamizi katika maeneo ya ulinzi wa maliasili, utalii na mapato, usimamizi shirikishi wa malisho, pamoja na kuboresha mawasiliano kati ya uongozi, watendaji na jamii kwa ujumla
Kwa ujumla, ujumbe mkubwa uliotolewa ni kwamba uhifadhi unaoongozwa na jamii unaweza kufanikiwa pale ambapo jamii zinamiliki kikamilifu maliasili zao za asili, zinazisimamia kwa uwajibikaji, na kunufaika moja kwa moja na matunda ya uhifadhi huo.