28/08/2026
WATUMISHI WASISITIZWA UMUHIMU WA KUZINGATIA MIONGOZO YA IPC
Watumishi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa, Bukoba, wameendelea kusisitizwa umuhimu wa kuzingatia miongozo ya Kinga na Udhibiti wa Maambukizi (IPC) katika utoaji wa huduma za afya ili kuhakikisha usalama wa wagonjwa pamoja na watumishi.
Rai hiyo imetolewa na Dkt. Chrisogone German Kutoka Wizara ya Afya wakati akiwasilisha taarifa kwa watumishi wa hospitali hiyo baada ya kukamilika kwa zoezi la ufuatiliaji IPC lililosimamiwa na Timu ya kutoka Wizara ya Afya kwa kushirikiana shirika la CIHEB Tanzania kupitia Mradi wa Usalama wa Afya Duniani.
Akizungumza wakati wa zoezi hilo, amesisitiza watumishi kuzingatia matumizi sahihi ya vifaa kinga binafsi (PPE) wakati wa kutekeleza majukumu yao, akieleza kuwa matumizi hayo ni muhimu katika kujikinga dhidi ya maambukizi na kulinda usalama wa wagonjwa wanaopatiwa huduma.
Aidha, ameishukuru Timu ya Uboreshaji Ubora (QI) ya Hospitali ya Rufaa ya Mkoa, Bukoba, kwa kuendelea kusimamia kwa karibu shughuli za kila siku za hospitali na kuhakikisha utoaji wa huduma unazingatia miongozo na viwango vinavyotakiwa.
Ameitaka Timu hiyo kuendelea kusimamia utekelezaji wa miongozo ya IPC katika maeneo yote ya hospitali na kuhakikisha watumishi wanaendelea kuzingatia taratibu hizo ili huduma za afya ziendelee kutolewa kwa usalama na ubora zaidi.
Kwa upande wake, Afisa Tawala na Rasilimali Watu wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa, Bukoba, Simon Njeya, akitoa neno kwa niaba ya Mganga Mfawidhi, ameishukuru Timu ya IPC kutoka Wizara ya Afya kwa kuendelea kutembelea hospitali hiyo na kutoa ushauri wa kitaalamu unaolenga kuboresha utoaji wa huduma.
Njeya ameahidi kuwa uongozi wa hospitali utafanyia kazi ushauri na maeneo yote yaliyoainishwa kuwa yanahitaji maboresho, huku akisisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya watumishi na timu mbalimbali katika kuhakikisha miongozo ya IPC inatekelezwa ipasavyo.
Zoezi hilo limekuwa sehemu ya juhudi za kuimarisha Kinga na Udhibiti wa Maambukizi .