27/06/2026
Bodi ya Wakurugenzi ya Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Bukoba (BUWASA), ikiongozwa na Mwenyekiti wa Bodi, Bw. Samora Lyakurwa imefanya kikao chake cha mwisho cha kipindi cha uongozi wake kilichofanyika kwenye ukumbi wa mikutano BUWASA.
Kikao hiki kililenga kupitia utekelezaji wa mipango, maendeleo ya miradi pamoja na utendaji wa Mamlaka katika kuhakikisha huduma za majisafi na usafi wa mazingira zinaendelea kuboreshwa kwa wananchi.
Katika kikao hicho, wajumbe walipitia taarifa mbalimbali za utekelezaji wa miradi ya maendeleo, wakajadiliana kuhusu mafanikio yaliyopatikana, changamoto zilizojitokeza pamoja na mikakati ya kuendeleza maboresho katika utoaji wa huduma. Bodi ilieleza kuridhishwa na hatua zilizofikiwa katika utekelezaji wa miradi na kusisitiza umuhimu wa kuendelea kusimamia miradi hiyo kwa ufanisi, uwazi na kuzingatia thamani ya fedha.
Akihitimisha kikao hicho, Mwenyekiti wa Bodi, Bw. Lyakurwa aliwashukuru na kuwapongeza wajumbe wote wa Bodi kwa ushirikiano, kujituma na mchango wao mkubwa katika kusimamia maendeleo ya BUWASA katika kipindi chote walichohudumu.
Aidha, aliipongeza Menejimenti na watumishi wa BUWASA kwa ushirikiano waliouonesha katika kutekeleza maamuzi ya Bodi na kuhimiza kuendelea kufanya kazi kwa weledi, ubunifu na uwajibikaji ili kuhakikisha wananchi wanaendelea kupata huduma bora, salama na endelevu za majisafi na usafi wa mazingira.
"BUWASA itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali katika kusimamia utekelezaji wa miradi ya maendeleo na kuimarisha utoaji wa huduma bora, ikiwa ni sehemu ya dhamira yake ya kuboresha ustawi wa wananchi na kuchochea maendeleo" aliongeza Bw Lyakurwa.
Bodi ya Wakurugenzi BUWASA inatarajiwa kumaliza muda wake tarehe 30,June 2026 baada ya kutumikia Bodi hii kwa muda wa miaka mitatu.
IMETOLEWA NA KITENGO CHA MAWASILIANO NA UHUSIANO BUWASA
26/06/2026