03/08/2026
MAKAMU WA RAIS APONGEZA MAONESHO YA NANE NANE 2026
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi, ametembelea Maonesho ya Kitaifa na Kimataifa ya Nane Nane tarehe3 Agosti 2026 na kupongeza kazi nzuri za waoneshaji za teknolojia mbalimbali zinazoakisi kwa vitendo kaulimbiu yake katika safari ya utekelezaji wa DIRA 2050.
Maonesho ya Nanenane 2026 yanafanyika katika Viwanja vya Dkt. John Samuel Malecela, jijini Dodoma chini ya kaulimbiu "Tambua Soko; Ongeza Tija Kutekeleza DIRA 2050".
Mheshimiwa Makamu wa Rais ametembelea na kupokea maelekezo kutoka kwa wataalamu kuhusu shughuli mbalimbali za uzalishaji na ubunifu wa sekta ya kilimo, mifugo na uvuvi pamoja na mikakati inayotekelezwa katika kufikia malengo ya DIRA 2050.
Katika ziara hiyo, Mheshimiwa Makamu wa Rais ametembelea banda la mdhamini mkuu wa maonesho hayo, Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB), pamoja na mabanda mbalimbali ya maonesho yaliyohusisha vipando vya zao la ulezi kutoka Halmashauri ya Mpwapwa, mbegu bora za mifugo ya mbuzi, kondoo na ng'ombe, vifaranga vya samaki, pamoja na shamba darasa la mbegu za malisho ya mifugo.
Aidha, ametembelea eneo la maadhimisho ya miaka 10 ya Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Tanzania (TARI), pamoja na kushiriki shughuli za Siku ya Ushirika, ambazo zimekuwa sehemu ya matukio muhimu yanayoambatana na Maonesho ya Nane Nane mwaka huu.
Ziara hiyo imehudhuriwa na viongozi mbalimbali wa Serikali, akiwemo Waziri wa Kilimo, Mhe. Daniel Chongolo (Mb); Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mhe. Rosemary Senyamule; Mkuu wa Mkoa wa Singida, Mhe. Halima Dendego; Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Ng'wasi Damas Kamani; Mkurugenzi Mkuu wa TARI, Dkt. Thomas Bwana; Mrajisi wa Vyama vya Ushirika na Mtendaji Mkuu wa Tume ya Maendeleo ya Ushirika Tanzania (TCDC), Dkt. Benson Ndiege, pamoja na wadau mbalimbali muhimu katika mnyororo wa thamani wa Sekta za Kilimo, mifugo na uvuvi.
Wizara Ya Manugu kilimo