13/07/2026
Wananchi wa maeneo ya vijijini wameeleza namna maboresho ya huduma za mawasiliano yalivyosaidia kurahisisha maisha yao, hususan katika kupata huduma za afya na kuwasiliana na ndugu pamoja na jamaa zao.
Mmoja wa wananchi hao, Lucy Kusimula, mkazi wa Kijiji cha Ikowa wilayani Chamwino mkoani Dodoma, amesema hapo awali walikabiliwa na changamoto kubwa za mawasiliano, hali iliyowalazimu kutegemea simu za majirani walipokuwa wakikumbwa na dharura.
Amesema wanawake wajawazito walilazimika kutembea umbali mrefu kufuata huduma za afya, lakini kwa sasa upatikanaji wa huduma za mawasiliano umewezesha mawasiliano ya haraka na kurahisisha hata kupokea fedha kutoka kwa ndugu wakati wa mahitaji ya dharura.
Kwa upande wake, Rose Charles ameishukuru Serikali pamoja na Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF) kwa kuendelea kusogeza huduma za mawasiliano karibu na wananchi kupitia ujenzi wa minara ya mawasiliano.
Amesema hatua hiyo imeimarisha upatikanaji wa huduma muhimu, ikiwemo kuwasiliana na vituo vya afya na kuitisha huduma za dharura kwa akina mama wajawazito, jambo ambalo limeongeza usalama na ustawi wa jamii.
Reposted from TBC DIGITAL