13/08/2026
TANZANIA MWENYEJI WA MKUTANO WA 10 WA WATAALAM WA MIFUGO BARANI AFRIKA 2029
Tanzania imechaguliwa kuwa mwenyeji wa Mkutano wa 10 wa Wataalam wa Mifugo Barani Afrika (10th All Africa Conference on Animal Agriculture – AACAA), unaotarajiwa kufanyika mwaka 2029 nchini Tanzania.
Uamuzi huo umefikiwa tarehe 12 Agosti 2026 na wanachama wa Jumuiya ya Wataalam wa Mifugo Barani Afrika (All Africa Society of Animal Production – AASAP) wanaoshiriki Mkutano Mkuu wa Tisa wa Jumuiya hiyo unaofanyika mjini Abuja, Nigeria, kuanzia tarehe 9 hadi 13 Agosti 2026.
Wanachama wa AASAP wamekubaliana kuichagua Tanzania kuwa mwenyeji wa mkutano huo baada ya kuvutiwa na juhudi na maendeleo yanayofanywa nchini katika kuendeleza Sekta ya Mifugo, pamoja na fursa zilizopo katika maeneo ya utafiti, teknolojia na ubunifu wa mifumo ya uzalishaji wa mifugo.
Kabla ya uamuzi huo, Dkt. Titus Eliamoni Lyatuu, ambaye ni mjumbe wa Kamati Kuu ya Chama cha Wataalam wa Mifugo Tanzania (TSAP) na mwakilishi wa Tanzania katika mkutano huo, aliwasilisha utayari wa Tanzania katika kuandaa na kuendesha mkutano huo mkubwa wa kimataifa. Dkt. Lyatuu alieleza kuwa Tanzania ina fursa mbalimbali za tafiti na maendeleo katika Sekta ya Mifugo ambazo zinaweza kuwa sehemu muhimu ya mijadala ya wataalam kutoka mataifa mbalimbali ya Afrika.
Aidha, Dkt. Lyatuu alieleza vivutio na fursa mbalimbali zinazopatikana nchini Tanzania, ikiwemo mashamba na mifumo mbalimbali ya ufugaji, vivutio vya utalii, utamaduni wa Watanzania, amani na usalama, pamoja na mazingira mazuri ya uongozi na usimamizi wa Sekta ya Mifugo kupitia Wizara ya Mifugo na Uvuvi.
Uchaguzi wa Tanzania kuwa mwenyeji wa mkutano huo unatarajiwa kutoa fursa kwa wataalam, watafiti, taasisi za elimu na utafiti, wafugaji, sekta binafsi na wadau mbalimbali wa Sekta ya Mifugo kutoka Afrika na nje ya Afrika kukutana, kubadilishana uzoefu, kujadili matokeo ya tafiti na kuweka mikakati ya kuendeleza Sekta ya Mifugo barani Afrika.
Katika maandalizi kuelekea mkutano huo, TSAP imejiandaa kushirikisha wadau mbalimbali wa Sekta ya Mifugo na Uvuvi, pamoja na taasisi nyingine zinazohusiana na maendeleo ya sekta hiyo, ili kushirikiana katika maandalizi na kuhakikisha mkuta