05/03/2026
KAYA 2,114 ZENYE UHITAJI MAALUMU HALMASHAURI YA MJI KASULU KUNUFAIKA NA MPANGO WA BIMA YA AFYA KWA WOTE
Mkuu wa Wilaya ya Kasulu Kanali Isaac Mwakisu amezindua zoezi la uandikishaji na ugawaji wa Bima ya Afya kwa wananchi wa Halmashauri ya Mji Kasulu wanaotoka katika familia zenye uhitaji maalumu huku akiwataka wataalam kuhakikisha wanawafikia wanufaika wote waliokusudiwa.
Amesema hayo wakati wa uzinduzi huo katika Ofisi ya Serikali ya Mtaa wa Nyalumanga na kubainisha kuwa Serikali chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imegharamia bima hizo kwa wananchi wasiokuwa na uwezo ili kuwawezesha kupata huduma za matibabu kwa urahisi na kuondoa vikwazo vya upatikanaji wa huduma za afya.
" Awamu hii ni kwa wale watu ambao hawana uwezo wa kugharamia upatikanaji wa Bima , sasa Mhe. Rais amegharamia gharama zote na tunagawa bima za afya lengo kubwa ni kuwezesha wananchi kufikia huduma za matibabu na kuondoa vikwazo vyote na kuleta usawa kwa wananchi kuanzia ngazi ya chini hadi kitaifa "
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Mbelwa Abdallah Chidebwe amebainisha kuwa ahadi ya Chama ni kuhakikisha kila mwananchi anapata Bima ya Afya.
Aidha, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji Kasulu Ayubu Ngalaba Kilugu amewatoa hofu wananchi ambao bado hawajapata Bima na kuwataka kuwa na subira kwa kuwa zoezi hilo bado linaendelea.
"Swala la afya ndugu zangu ni swala nyeti sana watu wengi wanapoteza maisha kwa sababu ya kukosa gharama za matibabu kwa hiyo hiki kitu anachokifanya Mhe. Rais ni kitu kizuri sana kwa hiyo wanakigondo tunamshukuru sana na Kwa wale ambao hamjapata huduma kwa leo bado zoezi hili ni endelevu msife moyo "
Katika hatua nyingine, Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Kasulu Nurfis Azizi amesema amethibitisha kuwa vifaa vya BVR vilivyopo vinafanya kazi vizuri na vinasaidia kurahisisha usajili wa wanufaika.
Meneja wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya, Gwamaka Mwakyoma, ameahidi kusimamia utekelezaji wa Bima kwa weledi na uadilifu, kuhakikisha wananchi wanahudumiwa ipasavyo.
Baadhi ya wanufaika wanamshukuru Rais Dkt. Samia kwa kuwawezesha kupata Bima za Afya ambazo zinaenda kurahisisha upatikanaji wa huduma bora za afya kwa urahisi.
Awamu ya kwanza ya zoezi hilo limejumuisha jumla ya kaya 2114 Halmashauri ya Mji Kasulu ambapo watu 9360 wenye uhitaji maalumu watanufaika.