26/08/2026
MBINGA DC YAWAKUMBUSHA WADAU WA NYAMA KUSHIRIKIANA NA WATAALAMU KUIMARISHA USALAMA WA BIDHAA.
Mkuu wa Divisheni ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi, Mhandisi Evance Haule, amewataka wadau wa sekta ya nyama wakiwemo wachinjaji, wamiliki wa mabucha, na wauza nyama kudumisha ushirikiano wa karibu na wataalamu wa mifugo ili kuimarisha ubora na usalama wa bidhaa hiyo kwa jamii.
Wito huo umetolewa wakati wa kikao kazi leo tarehe 26 Agosti, 2026 kilichowakutanisha wadau hao katika ukumbi wa Halmashauri kwa lengo la kujadili masuala mbalimbali ya usimamizi, uendeshaji, na uzingatiaji wa sheria katika mnyororo wa thamani wa nyama.
Mhandisi Haule amewataka wadau hao kuzingatia kuuza nyama ambayo imepimwa na kukaguliwa na mtaalamu wa mifugo aliyethibitishwa. Hatua ambayo ni muhimu ili kuhakikisha nyama inayomfikia mlaji inafaa kwa matumizi ya binadamu.
Aidha, wadau wamekumbushwa kuongeza umakini katika usafi wa maeneo ya kuchinjia, vyombo vya usafirishaji, na mabucha ili kuepusha hatari ya milipuko ya magonjwa.
Mhandisi Haule alisisitiza wadau wote kuhakikisha wana vibali vyote vinavyotakiwa kwa mujibu wa sheria pamoja na kulipa ushuru wa Halmashauri kwa wakati ili kuchangia maendeleo katika jamii.
Aidha, Afisa Mifugo, ndugu Haruna Masige alieleza kuwa ni muhimu wadau hao kuwa na viongozi ambao watakuwa na jukumu la kuimarisha umoja miongoni mwao pamoja na kuhusika katika kutatua changamoto qanazokabiliana nazo kwa kushirikiana na viongozi wa Halmashauri.
Wadau waliteua wajumbe kadhaa na kupiga kura ambapo ndugu Hance Patrick Turuka kutoka Amani Makoro alichaguliwa kuwa Mwenyekiti, ndugu Zandati John Mdegela kutoka Mapera kuwa Mwenyekiti Msaidizi, ndugu Patrick. kutoka Mkumbi Katibu, ndugu Baltazary B Nchimbi wa Ukata Katibu Msaidizi na Baraka Mbena wa Kigonsera kuwa Mtunza Hazina.