22/08/2026
Halmashauri Serengeti yaendesha zoezi la chanjo ya Kichaa cha Mbwa
Ofisi ya Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Serengeti kupitia Idara ya Kilimo na Mifugo kwa kushirikiana na wadau wa Rabies Free Tanzania imeendesha zoezi la utoaji wa chanjo kwa Mbwa na Paka katika eneo la Serengeti Mjini ikiwa ni hatua ya kuzuia na kudhibiti ugonjwa hatari wa kichaa cha mbwa.
Akizungumza wakati wa zoezi hilo lililofanyika Agosti 22, 2026, Afisa Mifugo wa Halmashauri Bw. Mesiaki Lukumay amesema Halmashauri inalenga kuchanja jumla ya mbwa na paka 45,460 katika Kata zote 30 za Wilaya ya Serengeti. Amesisitiza kuwa chanjo hiyo si tiba kwa mnyama ambaye tayari ameambukizwa kichaa cha Mbwa bali ni kinga dhidi ya ugonjwa huo.
Amesema zoezi hilo ni endelevu kutokana na upatikanaji wa chanjo kupitia Halmashauri pamoja na wadau hatua inayolenga kuhakikisha ugonjwa wa kichaa cha mbwa unatokomezwa katika Wilaya ya Serengeti.
Kwa upande wake Meneja Msaidizi wa Programu ya Rabies Free Tanzania Bw. Machunde Bigambo, amesema hadi sasa jumla ya Mbwa na Paka 11,200 wamechanjwa katika Kata 18, huku akieleza kuwa chanjo hiyo inalenga kuzuia ugonjwa huo kuenea kwa wanyama na hatimaye kuwaambukiza binadamu.
Bw. Machunde amesisitiza kuwa kichaa cha mbwa ni ugonjwa hatari ambao unapotokea huwa hauna tiba. Hivyo amewataka wananchi kuhakikisha Mbwa na Paka wao wanapatiwa chanjo kwa wakati ili kujikinga na ugonjwa huo.
Aidha amewashukuru wananchi kwa kujitokeza kwa wingi kuwaleta Mbwa na Paka wao kwa ajili ya chanjo, pamoja na kuishukuru Halmashauri ya Wilaya ya Serengeti kwa ushirikiano mkubwa katika kufanikisha zoezi hilo.