06/05/2026
Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa Serikali za Mitaa na Idara Maalum za SMZ Mhe. Idrissa Kitwana Mustafa amesema Serikali kupitia Mradi wa BigZ inaendelea kutekeleza ujenzi wa vituo vya kukusanyia taka ngazi ya jamii (Primary Collection Points) kwa lengo la kuimarisha usafi wa mazingira na afya ya jamii katika maeneo ya Mijini na Vijijini.
Ameyasema hayo katika ukumbi wa Baraza la wawakilishi wakati akijibu swali la Muakilishi wa Jimbo la Magomeni Mhe. Mahfoudh Abdalla Mohammed kuhusu mpango wa Serikali wa kujenga madampo (waste collection) katika maeneo yanayotekelezwa mradi wa mitaro ya maji machafu.
Mhe. Kitwana amesema jumla ya vituo vitatu (3) vya kukusanyia taka vitajengwa katika maeneo yanayotekelezwa ujenzi wa mitaro ya maji ya mvua, ikiwemo Shehia ya Meya (Magae), Nyerere (Mtumwajeni) na Sogea Jitini, ambapo mkandarasi M/s Faster Construction Group of Company tayari ameshayakagua na kukabidhiwa maeneo hayo.
Amesema Hatua hii ni sehemu ya mkakati maalum wa kuboresha mfumo wa usimamizi wa taka ngumu, kupunguza uchafuzi wa mazingira na kuongeza ufanisi katika ukusanyaji, usafirishaji na uhifadhi wa taka katika Miji
📆 06 Mei, 2026
📍 Baraza la Wawakilishi, Zanzibar.