31/05/2026
WAZIRI MAKONDA: TANAPA IMEFUNGUA FURSA ZA KIUCHUMI NA UWEKEZAJI KUPITIA UTALII WA MICHEZO NCHINI
Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) kupitia utalii wa michezo unaohusisha riadha, magari, baiskeli na pikipiki imeendelea kufungua fursa za kiuchumi kwa wadau wa utalii, uhifadhi na uwekezaji huku ikitoa nafasi ya kutangaza bidhaa, huduma na vivutio vya utalii vya Tanzania.
Akizindua mbio za Cape to Cairo Arusha International Marathon Mei 31, 2026 jijini Arusha, Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Paul Makonda, alisema utalii wa michezo umeendelea kuitangaza Tanzania kitaifa na kimataifa na unatarajiwa kuongeza idadi ya watalii wanaotembelea nchi.
Mbio hizo ziliwakutanisha washiriki kutoka China, Korea, Kenya, Uganda, Rwanda, Burundi, Uingereza na Tanzania, ambapo baadhi walitembelea Hifadhi ya Taifa Arusha huku wengine wakiahidi kurejea tena kwa ajili ya kutalii.
āNimeona kazi nzuri inayofanywa na TANAPA katika kutangaza vivutio vya utalii. Hifadhi ya Taifa Arusha ni miongoni mwa maeneo yenye vivutio vya kipekee. Wananchi na wadau watumie fursa hizi kujitangaza na kukuza uchumi wao,ā alisema Makonda.
Aliongeza kuwa mwezi Julai kutafanyika Arusha Tourism Marathon, ambapo washiriki watapata fursa ya kukimbia ndani ya Hifadhi ya Taifa Arusha.
Mkuu wa Hifadhi ya Taifa Arusha, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Uhifadhi Witness Shoo, alisema utalii wa michezo umechangia kuongezeka kwa wageni na kufungua fursa zaidi za biashara na uwekezaji.
Kufikia Mei 31, 2026, Hifadhi ya Taifa Arusha imeshiriki kuratibu matukio makubwa ya kimichezo yakiwemo Cape to Cairo Arusha International Marathon, Arusha Tourism Marathon na Subaru Festival.