31/05/2026
GPSA YAFANYA USAFI WA MAZINGIRA YA OFISI KUELEKEA SIKU YA MAZINGIRA DUNIANI 2026
Kuelekea maadhimisho ya siku ya mazingira duniani kwa mwaka 2026, viongozi na watumishi wa Wakala wa Huduma ya Ununuzi Serikalini (GPSA) washiriki usafi wa mazingira kuzunguka Ofisi na vituo vyake siku ya Jumamosi tarehe 30/05/2026.
CPA Juliana Mero (Mkuu wa Kitengo cha Ukaguzi wa Ndani-GPSA) akizungumza kwa niaba ya Afisa Mtendaji Mkuu Prof. Geraldine Arbogast Rasheli kuwa Wakala unatambua umuhimu wa mazingira safi katika kujenga afya bora, kuongeza tija kazini na maendeleo endelevu, ambapo zoezi hili limefanyika katika mikoa yote Tanzania Bara.
CPA Juliana Mero ameongeza, " Kwa GPSA, maadhimisho ya siku ya mazingira duniani si tu fursa ya kukumbusha umuhimu wa kuhifadhi mazingira, bali pia mwito wa kuchukua hatua za vitendo zinazochangia kujenga mazingira safi, salama na endelevu kwa kizazi cha sasa na kijacho".
GPSA inajivunia mchango wake kiujumla katika utunzaji wa mazingira kupitia mfumo wa kidijitali wa utoaji wa huduma zake wa GIMIS ambapo umepelekea kupunguza matumizi makubwa ya karatasi katika Ununuzi wa Umma pamoja na Ununuzi wa bidhaa zisizochafua mazingira ili kuhakikisha fedha za umma zinachangia uchumi wa kijani (Green economy).
Aidha, Wakala unahamasisha matumizi ya nishati safi ya gesi asilia iliyoshindiliwa (CNG-V) na umeme (EV) kwenye magari ya Serikali kwa ujenzi wa vituo vyake katika Mpango Mkakati wake 2026/27-2030/31).
Siku ya kilele ya maadhimisho ya Mazingira Duniani (World Environment Day) ni Juni 5, 2026, ambapo kauli mbiu ya mwaka huu 2026 ni "Dira 2050: Tuwajibike Kukijanisha Tanzania".