30/05/2026
PUGU KAZIMZUMBWI: HAZINA YA UTALII INAYOHIFADHI HISTORIA NA BIOANUAI
Wahifadhi wa Sao Hill wavutiwa na mafanikio ya utalii ikolojia, watakiwa kuhamasisha kura za Tuzo za Kimataifa za Utalii
Na Mwandishi Wetu, Pwani
Hifadhi ya Msitu wa Asili ya Pugu Kazimzumbwi mkoani Pwani imeendelea kujidhihirisha kuwa moja ya hazina kubwa za utalii wa ikolojia nchini baada ya kuvutia wahifadhi kutoka Shamba la Miti Sao Hill waliotembelea eneo hilo kujifunza mbinu za uhifadhi, usimamizi wa bioanuai na maendeleo ya utalii endelevu.
Ziara hiyo imekuja wakati Tanzania ikiendelea kuimarisha juhudi za kuhifadhi rasilimali za misitu na kuendeleza utalii wa asili k**a sehemu ya kuongeza mchango wa sekta hiyo katika uchumi wa taifa, huku Pugu Kazimzumbwi ikitajwa kuwa miongoni mwa maeneo yanayoongoza kwa kuhifadhi urithi wa kihistoria na mazingira ya kipekee karibu na Jiji la Dar es Salaam.
Wakati wa ziara hiyo leo, wahifadhi hao walitembelea vivutio mbalimbali vinavyopatikana ndani ya hifadhi hiyo ikiwemo misitu ya asili yenye bioanuai adimu, njia za utalii wa kutembea msituni, maeneo ya kihistoria pamoja na vivutio vya kiikolojia vinavyovutia watalii wa ndani na nje ya nchi.
Maofisa wa hifadhi hiyo waliwaeleza wageni hao kuhusu hatua zinazochukuliwa kulinda mazingira, kudhibiti shughuli zinazohatarisha misitu na kuendeleza utalii wa ikolojia unaochochea maendeleo ya jamii na kuongeza mapato ya taifa bila kuathiri mfumo wa ikolojia.
Akizungumza baada ya kutembelea vivutio hivyo, Kiongozi wa Msafara huo, CO I Donald Makupa, alisema uzoefu walioupata katika Hifadhi ya Msitu wa Asili ya Pugu Kazimzumbwi utakuwa chachu ya kuboresha mikakati ya uhifadhi katika maeneo wanayoyasimamia.
“Tumeshuhudia namna ambavyo uhifadhi wa misitu unaweza kwenda sambamba na maendeleo ya utalii. Maarifa haya yatatusaidia kuimarisha usimamizi wa rasilimali za misitu na kuongeza thamani ya maeneo yetu ya uhifadhi,” alisema Makupa.
Aliongeza kuwa ushirikiano na kubadilishana uzoefu kati ya taasisi na maeneo mbalimbali ya uhifadhi ni nyenzo muhimu katika kuhakikisha sekta ya misitu na utalii inaendelea kukua kwa manufaa ya taifa.