07/08/2026
MoEST WATATHMINI MAENDELEO YA UTEKELEZAJI WA MRADI WA HEET, OUT
Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia (MoEST) na Chuo Kikuu Huria cha Tanzania (OUT) wamefanya kikao kazi cha kutathmini maendeleo ya utekelezaji wa Mradi wa Elimu ya Juu kwa Mageuzi ya Kiuchumi (HEET) unaotekelezwa na OUT, huku kwa pamoja wakisisitiza usimamizi madhubuti na kasi katika kukamilisha shughuli za mradi kwa viwango vinavyotarajiwa.
Kikao hicho kilichofanyika Agosti 3, 2026, makao makuu ya OUT, Kinondoni jijini Dar es Salaam, kiliongozwa na Mratibu wa Kitaifa wa Mradi wa HEET, Dkt. Kennedy Hosea na kuhudhuriwa na Naibu Makamu mkuu wa chuo anayesimamia Taaluma, Utafiti na Huduma za Kitaalam na Mratibu wa Mradi wa HEET kwa upande wa OUT, Prof. Saganga Kapaya, aidha kulihudhuriwa pia na wajumbe mbalimbali kutoka Wizara ya Elimu Sayansi na Teknologia na wajumbe wa Chuo Kikuu Huria cha Tanzania.
Akizungumza katika kikao hicho, Dkt. Hosea alisisitiza umuhimu wa usimamizi wa karibu, uwajibikaji na ushirikiano kati ya Wizara na taasisi zinazotekeleza mradi huo ili kuhakikisha malengo yake yanafikiwa.
“Mradi wa HEET ni uwekezaji muhimu katika kuimarisha ubora na ushindani wa elimu ya juu nchini. Ni wajibu wetu kuhakikisha kuwa kila shughuli inayotekelezwa chini ya mradi inaleta matokeo yanayokusudiwa kwa kuzingatia muda, ubora na matumizi sahihi ya rasilimali,” alisema Dkt. Hosea.
Kwa upande wake, Mratibu wa Mradi wa HEET kwa OUT, Prof. Saganga Kapaya, alisema kuwa Chuo Kikuu Huria cha Tanzania kitaendelea kuhakikisha utekelezaji wa shughuli za mradi zinafanyika kwa ufanisi ili kuchangia katika kuboresha mazingira ya ufundishaji, ujifunzaji na utafiti pia kuimarisha utoaji wa elimu yenye ubora kwa kuzingatia mahitaji ya sasa ya kitaifa na kimataifa
Mradi wa HEET ni mpango wa Serikali unaolenga kuimarisha sekta ya elimu ya juu nchini kupitia uwekezaji katika miundombinu, teknolojia, utafiti, ubunifu na uendelezaji wa rasilimali watu, kwa lengo la kuchochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii.