17/04/2026
Mhe. Wanu Azindua Kampeni ya ‘Kiduchu’ kuhamasisha Urejeshaji Kidogo Kidogo
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Mhe. Wanu Hafidh Ameir, amezindua rasmi kampeni ya “Kiduchu” na kusisitiza umuhimu wa urejeshaji wa mikopo ya elimu ya juu unaozingatia uwezo wa kila mnufaika hususan katika sekta isiyo rasmi ili kuhakikisha uendelevu wa mfuko kwa manufaa ya vizazi vijavyo. Uzinduzi huo umefanyika leo, (Aprili 17, 2026), katika ofisi za Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB), Kanda ya Mashariki, jijini Dar es Salaam.
Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Mhe. Wanu amesema kuwa katika kipindi cha miaka mitano (kuanzia 2021/2022 hadi 2025/2026), Serikali imefanikiwa kutoa TZS 3.6 trilioni kwa wanafunzi wa vyuo ngazi ya elimu ya kati na ya juu, hatua iliyowezesha vijana wengi kupata elimu bila vikwazo vya kifedha.
Kwa upande wa makusanyo, amebainisha kuwa HESLB imeendelea kuimarisha ukusanyaji wa mikopo kupitia juhudi mbalimbali za uhamasishaji, hatua inayolenga kuhakikisha kuwepo kwa mfuko endelevu wa kugharimia elimu ya kati na ya juu nchini.
Mhe. Naibu Waziri ameeleza kuwa bado kuna changamoto ya baadhi ya wanufaika, hususan wenye kipato cha chini, ambao hawajaanza au wamesitisha urejeshaji wa mikopo kutokana na hali zao za kiuchumi.
Kutokana na hali hiyo, Mhe. Wanu amezindua rasmi kampeni ya “Kiduchu” yenye kaulimbiu “Fresh, Tunasonga!”, inayolenga kuwahamasisha wanufaika kuanza kurejesha mikopo yao kwa kiasi kidogo walichonacho, kwa kuanzia TZS 5,000. Kampeni ya “Kiduchu”, imelenga kuwafikia wanufaika 135,186 wanaodaiwa jumla ya TZS 920 bilioni.
Akimkaribisha mgeni rasmi, Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa HESLB, Prof. Hamisi Dihenga, amesema kampeni hiyo inaakisi kaulimbiu ya “Kazi na Utu” kwa kuzingatia hali halisi ya kipato cha wanufaika.
Naye Mkurugenzi Mtendaji wa HESLB, Dkt. Bill Kiwia, alieleza kuwa madeni yaliyoiva yanafikia TZS 2.78 trilioni kutoka kwa wanufaika 539,103, ambapo hadi sasa TZS 1.84 trilioni zimekusanywa kutoka kwa wanufaika 403,917 waliokwisha. Hata hivyo, bado kuna wanufaika 135,186 ambao hawajafikiwa wanaodaiwa TZS 920 bilioni.