30/08/2026
MTUTURA: SERIKALI ISITISHE VIBALI VYA BANDARI KAVU
Waziri Kivuli wa Ujenzi, Uchukuzi na Miundombinu wa ACT Wazalendo, Mtutura Abdallah Mtutura, ameitaka Serikali kusitisha mara moja utoaji wa vibali vipya vya Bandari Kavu (ICDs) jijini Dar es Salaam, huku bandari kavu zilizopo zipatiwe muda wa miezi sita kusitisha huduma zinazofanyika katikati ya jiji, pembezoni mwa barabara na maeneo yanayosababisha usumbufu kwa wananchi.
Akizungumza leo tarehe 30 Agosti 2026 na waandishi wa habari katika Makao Makuu ya Chama cha ACT Wazalendo, Mtutura amesema ongezeko la Bandari Kavu katika maeneo ya makazi na pembezoni mwa barabara limekuwa likisababisha madhila kwa wananchi, ikiwemo msongamano wa magari, uharibifu wa miundombinu na changamoto za usalama, huku likidhoofisha uchumi wa Dar es Salaam.
Mtutura amesema Bandari Kavu (ICDs) zimekuwa na uhusiano na wafadhili wa CCM pamoja na baadhi ya vigogo wa Serikali, akidai kuwa mfumo huo umetengeneza mwanya wa watu wenye maslahi binafsi kuunganisha biashara za bandari na kampuni zao za usafirishaji wa mizigo kwa lengo la kujipatia faida.
“Bandari kavu (ICDs) zina mizizi ya wafadhili wa CCM na vigogo wa Serikali ambao wametengeneza mwanya wa Bandari na makampuni yao ya usafirishaji wa mizigo ili kujipatia faida huku wakiacha madhila makubwa kwa wananchi na kudhoofisha uchumi wa Dar es Salaam,” amesema Mtutura.
Mtutura ameitaka Serikali kuchukua hatua za haraka kwa kusitisha utoaji wa vibali vipya vya Bandari Kavu, kufanya mapitio ya maeneo yote yenye ICDs na kuwapa waliopo muda wa miezi sita kuondoa shughuli hizo katika maeneo ya katikati ya jiji, pembezoni mwa barabara na maeneo yasiyokidhi vigezo vya mipango miji.