06/06/2026
CAG Akagua Ujenzi wa Jengo la Ofisi ya Taifa ya Ukaguzi Mwanza
Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Charles E. Kichere, amekagua maendeleo ya ujenzi wa Jengo la Ofisi ya Taifa ya Ukaguzi (NAOT) Mkoa wa Mwanza katika eneo la Mkolani. Katika ziara hiyo iliyofanyika tarehe 5 Juni 2026, CAG amepokea taarifa ya maendeleo ya mradi huo unaotekelezwa na Kampuni ya "MASASI Construction Company Limited" chini ya Mshauri Mwelekezi Kampuni ya BICO ya Chuo Kikuu Dar es Salaam.
Akizungumza mara baada ya kukagua, CAG ameeleza kuridhishwa na maendeleo ya mradi huo ambao umefikia asilimia 70 ya utekelezaji na kuwapongeza wasimamizi na wataalam wote kwa usimamizi uliowezesha kazi kuendelea kwa mpango uliopo.
Mradi huo unahusisha ujenzi wa jengo la kisasa la Ofisi lenye ghorofa mbili pamoja na miundombinu muhimu ikiwemo ukumbi wa mikutano, maktaba, kantini, maegesho ya magari na mifumo ya huduma za maji.
Ujenzi wa jengo la NAOT Mwanza unatarajiwa kuboresha mazingira ya kazi, kuongeza ufanisi wa Ukaguzi na kuboresha huduma kwa Wadau wa NAOT Mkoa wa Mwanza.