31/05/2026
UZALISHAJI WA VIUATILIFU NCHINI KUONGEZA NGUVU, VITA DHIDI YA MALARIA - DKT. SEIF
Na: OWM – TAMISEMI.
Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM- TAMISEMI) anayeshughulikia Afya, Dkt. Jafar Seif amesema hatua ya kampuni ya Tanzania Biotech Products Limited (TBPL) kuwekeza nguvu kwenye uzalishaji mkubwa wa mbolea hai, na viuadudu itakuwa na mchango mkubwa katika kupunguza maradhi ya malaria nchini.
Dkt. Seif ameyasema hayo Mei 30, 2026 Kibaha mkoani Pwani, wakati akizungumza katika hafla ya utiaji saini wa hati ya mauziano ya mbolea kati ya Shirika la Maendeleo la Taifa (NDC) na Tanzania Fertilizer Company (TFC), pamoja na hati za ushirikiano kati ya TBPL, Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Tanzania (TARI), Mamlaka ya Udhibiti wa Mbolea Tanzania (TFRA) na Wakala wa Afya ya Mimea na Viuatilifu Tanzania (TPHPA).
Amesema hatua hiyo inaendana na vipaumbele vya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, vya kulinda afya ya jamii na kuongeza thamani ya bidhaa za kilimo, akisisitiza kuwa viuatilifu hivyo vitasaidia kuimarisha mapambano dhidi ya ugonjwa wa malaria nchini.
Kwa upande wake Waziri wa Viwanda na Biashara Mhe. Judith Kapinga amesema hatua hiyo itasaidia kuongeza thamani ya rasilimali za ndani, kupunguza utegemezi wa bidhaa kutoka nje ya nchi na kuchochea ukuaji wa uchumi wa taifa.
Aidha, amezitaka halmashauri ambazo bado hazijachukua viuatilifu katika awamu ya tatu kufanya hivyo kwa wakati ili kuwezesha kuanza kwa ugawaji wa viuatilifu katika awamu ya nne, ambapo mpaka kufikia Mei 29, 2026 zaidi ya halmashauri 70 zilikuwa bado hazijachukua vifurushi vya viudadudu vilivyotengwa kwa ajili ya maeneo yao.
Kiwanda hicho kina uwezo wa kuzalisha lita milioni sita za viuatilifu vya kibaolojia kwa mwaka huku kikiwa na masoko ya ndani na nje ya nchi.