30/05/2026
..
Serikali imeingiza barabara ya Kampala University–Magole–Rada yenye kilomita 6.35 pamoja na barabara ya Njia Nne–Buyuni–Tuliani katika mpango wa DMDP II ambapo zinatarajiwa kujengwa kwa kiwango cha lami kwa awamu ili kuboresha huduma za usafiri kwa wananchi wa Jimbo la Kivule.
Hayo yamebainishwa na Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu , Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM-TAMISEMI) Dkt. Festo Dugange kwa Niaba ya Waziri wa Nchi, OWM-TAMISEMI, alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Kivule, Mhe. Douglas Didas Massaburi, Mei 29, 2026, Bungeni jijini Dodoma, aliyetaka kufahamu ni lini Serikali itakamilisha ujenzi wa Madaraja na Barabara ya Kitunda - Nyangasa - Kibeberu hadi Magole kwa kiwango cha lami.
Dkt. Dugange amesema Serikali tayari imeanza taratibu za manunuzi kwa ajili ya utekelezaji wa miradi hiyo huku ikiendelea kufanya matengenezo ya maeneo korofi ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora ya usafiri hasa kipindi cha mvua.
“Kwa hiyo nimthibitishie Mheshimiwa Mbunge na wananchi wa Jimbo la Kivule kwamba Serikali iko kazini na itahakikisha barabara hizi zinajengwa na zinapitika vizuri kwa manufaa ya wananchi,” amesema Dkt. Dugange.
Aidha, amesema Serikali imeendelea kutenga bajeti kuhakikisha barabara za Kitunda, Nyangasa, Kibeberu hadi Magohe zinapitika muda wote, huku ikijikita zaidi katika ujenzi wa barabara ya Kitunda–Mwangati kwa Mpalange ambapo kiasi cha shilingi milioni 950 kimetengwa kwa mwaka wa fedha 2026/2027.