13/05/2026
TANZANIA KUWA MWENYEJI WA MKUTANO WA KIMATAIFA WA WABUNGE WANAWAKE WA UKANDA WA MAZIWA MAKUU
Na Saidi Saidi, WMJJWM – Dodoma
Tanzania inatarajiwa kuwa mwenyeji wa Mkutano wa Kimataifa wa Wabunge Wanawake wa Ukanda wa Maziwa Makuu (ICGLR) unaotarajiwa kufanyika jijini Dar es Salaam kuanzia Novemba 2 hadi 5, 2026.
Hayo yamebainishwa na Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Dkt. Dorothy Gwajima, Mei 13, 2026 jijini Dodoma wakati wa kikao chake na ujumbe wa Jukwaa la Wabunge la Mkutano wa Kimataifa wa Ukanda wa Maziwa Makuu (ICGLR), ukiongozwa na Rais wake Mheshimiwa Sergio Vaz Mbunge wa bunge la Angola , ambapo Waziri Dkt. Gwajima amesema Tanzania imejipanga kikamilifu kuratibu mkutano huo muhimu unaolenga kuimarisha ushiriki wa wanawake katika uongozi, amani na maendeleo endelevu ndani ya ukanda huo.
Aidha, amesema mkutano huo utatoa jukwaa kwa wabunge wanawake kujadili namna ya kuimarisha mchango wa wanawake katika ujenzi wa amani, kuzuia migogoro, kuimarisha utawala bora pamoja na kushiriki katika maamuzi ya kisiasa na kijamii ndani ya Ukanda wa Maziwa Makuu.
Dkt. Gwajima amesisitiza kuwa kuwawezesha wanawake katika nafasi za uongozi ni hatua muhimu katika kufanikisha maendeleo jumuishi na kudumisha amani ya kudumu katika ukanda huo. Pia amesema uenyeji wa mkutano huo unaendana na dhamira ya Tanzania ya kuendeleza ajenda ya Wanawake, Amani na Usalama, hususan baada ya uzinduzi wa Mpango wa Taifa wa Wanawake, Amani na Usalama uliofanyika Agosti 19, 2025.
Kwa upande wake, Rais wa Jukwaa la Wabunge la Mkutano wa Kimataifa wa Ukanda wa Maziwa Makuu (ICGLR) Mhe. Sergio Vaz ameipongeza Tanzania kwa utayari wake wa kuwa mwenyeji wa mkutano huo, akieleza kuwa ushirikiano kati ya Tanzania na ICGLR utaendelea kuimarisha mshik**ano, mazungumzo na maendeleo katika Ukanda wa Maziwa Makuu.
MWISHO