02/06/2026
TIRA YAPANGA KUTOA ELIMU YA BIMA KWA WATU MILIONI 27 MWAKA 2026/27
Waziri wa Fedha Mhe. Balozi Khamis M***a Omar amebainisha hilo leo Juni 2, 2026 wakati wa Uwasilishaji wa Mapitio ya Utekelezaji wa Mpango na Bajeti wa Mwaka wa Fedha 2025/2026 na Mapendekezo ya Mpango wa Bajeti ya Wizara ya Fedha kwa mwaka 2026/2027 bungeni jijini Dodoma ambapo Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania (TIRA) imepanga kuimarisha zaidi usimamizi na maendeleo ya sekta ya bima nchini katika mwaka wa fedha 2026/27 kupitia utekelezaji wa mikakati mbalimbali ikiwemo usajili wa watoa huduma za bima 2,536 na utoaji wa elimu ya bima kwa wananchi milioni 27 kupitia majukwaa mbalimbali ya mawasiliano na programu za uhamasishaji zitakazotekelezwa nchini kote.
Aidha Waziri ameeleza TIRA imepanga kuendelea kuboresha Mfumo Jumuishi wa Udhibiti wa Bima (Insurance Regulatory Integrated System - IRIS) kwa kuongeza teknolojia ya uchambuzi wa takwimu (Predictive Analytics) ili kuongeza ufanisi katika usimamizi wa sekta na kuimarisha usalama wa mifumo ya TEHAMA na hivyo kuongeza huduma bora kwa wananchi.
Katika kuimarisha utekelezaji wa sheria na kanuni za bima imeelezwa TIRA imejipangia kufanya ukaguzi wa uzingatiaji wa sheria kwa wasajiliwa wa bima 618 nchini, hatua inayolenga kuhakikisha utoaji wa huduma za bima unazingatia viwango na matakwa ya kisheria.
Vilevile, TIRA itafanya tafiti mbili kuhusu mwenendo wa soko la bima nchini ili kupata taarifa muhimu zitakazosaidia katika maboresho ya sera, kanuni na mikakati ya kukuza sekta ya bima. Utekelezaji wa mipango hiyo unatarajiwa kuongeza uwazi, kuimarisha usimamizi wa sekta ya bima na kuchochea ukuaji wa matumizi ya huduma za bima kwa wananchi na wadau mbalimbali nchini
Kamishna wa Bima Dkt. Baghayo A. Saqware na Naibu Kamishna Bi. Khadija I. Said pia wamehudhuria uwasilishwaji huo.