17/08/2026
Katibu wa NEC Uchumi na Fedha Akutana na Uongozi wa TISEZA Ofisi Ndogo za CCM, Lumumba, Dar es Salaam, 17 Agosti 2026.
Katibu wa NEC, Uchumi na Fedha wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Ndugu Jamal Kassim Ali, amekutana na kufanya mazungumzo na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Uwekezaji na Maeneo Maalum ya Uchumi ya Tanzania (TISEZA) Ndugu Gilead John Teri kuhusu fursa za kimkakati za uwekezaji na namna ya kuimarisha mchango wa sekta binafsi katika uchumi wa Taifa.
Mazungumzo hayo yalijikita katika maeneo yenye uwezo mkubwa wa kuchochea ukuaji wa uchumi na kuongeza mapato, hususani uchukuzi na usafirishaji, madini, ardhi na majengo (real estate), pamoja na uwekezaji katika maeneo yenye fursa za kiuchumi.
Aidha, pande hizo zilijadili namna Chama kinavyoweza kuendelea kuendana na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 na kutekeleza kwa ufanisi vipaumbele vilivyoainishwa katika Ilani ya Uchaguzi ya CCM 2025β2030, hususan katika kukuza uwekezaji, uzalishaji, ajira na mapato, kuelekea kufikia malengo makubwa ya uchumi yaliyowekwa na Taifa.
Ndugu Jamal alisisitiza umuhimu wa Chama kuwa na mtazamo wa muda mrefu katika kutambua na kutumia fursa za uwekezaji, huku akisisitiza kuwa ushirikiano na taasisi za Serikali, wawekezaji na sekta binafsi ni muhimu katika kubadili fursa zilizopo kuwa shughuli halisi za kiuchumi zenye tija.
Mazungumzo hayo ni sehemu ya juhudi za Chama Cha Mapinduzi za kujenga ushirikiano na wadau wa uchumi na uwekezaji, kwa lengo la kuongeza ufanisi, mapato na mchango wa rasilimali za Chama katika maendeleo ya Taifa.