09/05/2026
SERIKALI KUMALIZA KERO YA MAJI KIBAIGWA - KONGWA
Serikali imewahakikishia wakazi wa Kata ya Kibaigwa, Wilayani Kongwa, kumalizika kwa changamoto ya upatikanaji wa majisafi, kufuatia mkakati wa Serikali ya Awamu ya Sita wa kununua mitambo ya kisasa ya kuchimbia visima kwa kila mkoa nchini.
Kauli hiyo imetolewa na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba (Mb), wakati akizungumza na Wananchi katika mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye stendi ya mabasi Kibaigwa, Wilaya ya Kongwa Mei 08, 2026.
Akifafanua jitihada za Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika sekta ya maji, Dkt. Nchemba alibainisha kuwa hatua ya awali ya upatikanaji wa mitambo imekamilika, na sasa Serikali inaelekeza nguvu kwenye utekelezaji wa miradi mikubwa.
"Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ameshakamilisha ununuzi wa mitambo ya kuchimbia visima kwa kila mkoa. Hatua inayofuata sasa ni kutenga Bajeti mahususi ya kununua vifaa na kuanza kutekeleza miradi mikubwa ya maji itakayomaliza kero hii kwa wananchi wa Kibaigwa na maeneo ya jirani," alisema Dkt. Nchemba.
Katika ziara hiyo, Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Dodoma (DUWASA), Mhandisi Aron Joseph, ameshiriki kikamilifu kuhakikisha maelekezo ya Serikali yanatekelezwa kwa manufaa ya Wananchi wa Kibaigwa.
Waziri Mkuu yupo katika ziara ya kikazi ya siku mbili katika Wilaya za Kongwa (Kibaigwa) na Mpwapwa. Lengo kuu la ziara hiyo ni kukagua miradi ya maendeleo, kusikiliza na kutatua kero mbalimbali zinazowakabili wananchi.