06/04/2019
CHAMA CHA MAPINDUZI (CCM) CHATOA MAELEKEZO MAZITO KATIKA MKUTANO WA KUMI WA WADAU WA KAHAWA TANZANIA.
Leo tarehe 5 Aprili, 2019 Jijini Dodoma, Dk. Bashiru Ally, Katibu Mkuu wa CCM ametoa maelekezo kwa niaba ya Chama Cha Mapinduzi katika Mkutano wa kumi wa wadau wa kahawa Tanzania kukomesha udalali na unyonyaji kwa wakulima wa zao la kahawa.
Mkutano huo umehudhuriwa na Manaibu Waziri wawili wa kilimo Ndg. Omari Mgumba (Mgeni rasmi) na Innocent Bashungwa, Wakuu wa mikoa inayolima kahawa, Wakuu wa wilaya, Wenyeviti wa halmshauri, Bodi ya kahawa, wakulima wadogo na wakubwa na wafanyabiashara wa kahawa.
Dk. Bashiru Ally akitoa salam na msimamo wa CCM katika mkutano huo ameeleza namna ambavyo Chama kimejipanga katika Ilani yake ya uchaguzi ya mwaka 2015 - 2020 ya kuboresha na kukata mirija ya unyonyaji kwa wakulima wa mazao yote ya kimkakati ikiwemo kahawa.
"Vita ya uchumi inajumuisha sekta ya madini, kilimo, mifugo na uvuvi, hivyo ninyi wadau wa kilimo ni askari katika vita hii kali, na asijitokeze mtu awe wa ndani ya Chama, Serikali au taasisi binafsi kutaka kutukwamisha, uongozi huu wa awamu ya tano chini ya Ndg. John Joseph Pombe Magufuli hautomuacha, atashughulikiwa yeye kabla hajatusaliti". Amesisitiza Dk. Bashiru
Ndg Bashiru ameeleza, CCM haikuomba ridhaa kwa wananchi kutetea makuadi, madalali na wapiga dili kwa wakulima wetu, na hii ni ajenda ya kudumu katika vikao vya Kamati Kuu ya CCM.
"Kamwe tusifanye kazi ya usaliti katika kikao hiki cha kumi, mtoe mapendekezo ya kuwavusha wakulima, sio kuwadidimiza." Katibu Mkuu amesisitiza
Kufafanua msimamo wa CCM katika mazao ya kimkakati ikiwemo kahawa, Dk. Bashiru ameeleza kuwa, ili wakulima kupitia vyama vya ushirika wawe salama katika bei ya kahawa, bodi ya kahawa itoe leseni za soko la moja kwa moja (Direct export) tofauti na hali ilivyo sasa ambapo bodi imekuwa ni kikwazo kikubwa kwa wakulima kutokana na viongozi wa bodi kuwa na mgongano wa maslahi, hivyo kuchelewesha utaoji wa leseni kwenye vyama vya ushirika.
"Bodi ya kahawa, hamuwezi kuwa bodi halali k**a waajiri wenu (wakulima) hawana imani nanyie, bodi ya kahawa mmekuwa ni kichaka cha udalali". Dk. Bashiru amesisitiza
Wakati huo huo Katibu Mkuu ameshauri kuwepo kwa vikao viwili, kwanza cha kujadili namna ya kumsaidia mkulima katika uzalishalishaji na pembejeo na kikao cha pili kiwe cha kujadili namna ya kumsaidia mkulima katika masoko na mikopo, ili kuongeza tija ya kilimo kwa wakulima wetu.
Huu ni muendelezo wa CCM kuisimamia serikali katika sekta zote zinazohudumia wananchi, na kuhakikisha wananchi wanalipwa kulingana na thamani ya jasho lao k**a ilivyoahidiwa katika ilani ya uchaguzi ya mwaka 2015-2020.