14/06/2026
KATIBU WA NEC AKAGUA MIRADI YA MAENDELEO, ASIKILIZA CHANGAMOTO ZA WANANCHI LINDI
Katibu wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa, Idara ya Mambo ya Siasa na Uhusiano wa Kimataifa, Ndugu Rabia Abdalla Hamid, ameanza ziara yake mkoani Lindi kwa kusikiliza maoni na changamoto za wananchi pamoja na kukagua utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo inayotekelezwa katika Manispaa ya Lindi.
Akizungumza katika kikao cha pamoja kilichofanyika katika Ukumbi wa Dockyard Hall, Leo tarehe 14 June 2026, Ndugu Rabia amesema ziara hiyo inalenga kuimarisha ushirikiano kati ya viongozi na wananchi kwa kusikiliza changamoto zinazowakabili na kutafuta njia za kuzitatua ili kuboresha ustawi wa jamii.
Amesema hatua hiyo ni utekelezaji wa maono ya Mwenyekiti wa CCM na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ya kuhakikisha wananchi wanapata nafasi ya kusikilizwa na kushirikishwa katika mchakato wa maendeleo.
Sambamba na hilo, ametembelea na kukagua miradi mbalimbali ya maendeleo, ambapo amepata fursa ya kujionea hatua zilizofikiwa katika utekelezaji wake na mchango wake katika kuinua hali ya maisha ya wananchi wa Lindi.
Aidha, amempongeza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Lindi Ndg. Juma Mnwele kwa ufafanuzi na majibu ya kina aliyoyatoa kuhusu hoja na changamoto zilizowasilishwa na wananchi, jambo lililosaidia kuongeza uelewa na kuimarisha imani ya wananchi kwa viongozi wao.