05/08/2026
WAZIRI AWESO AWATAKA WATENDAJI MBULU KUFANYA KAZI KWA BIDII NA UWAZI
Na Magreth Mbawala,Mbulu DC
Waziri wa Maji, Mhe. Jumaa Aweso, ambaye pia ni Mlezi wa Mkoa wa Manyara, amewataka watendaji wote wa Serikali kufanya kazi kwa bidii na uwazi ili kuendelea kuimarisha imani ya wananchi kwa Serikali yao.
Wito huo ameutoa leo, Agosti 5, 2026, wakati alipofanya ziara ya kikazi katika Halmashauri ya Wilaya ya Mbulu na kukutana na watendaji wa Serikali.
Akizungumza katika ziara hiyo, Mhe. Aweso alisisitiza kuwa kila mtendaji anapaswa kutekeleza majukumu yake kwa bidii katika eneo lake ili kuendelea kutoa huduma bora na kuleta maendeleo kwa wananchi.
“Haipendezi changamoto zilizo ndani ya uwezo wenu kuja kutatuliwa na viongozi au Waziri kutoka Dodoma,” alisema Mhe. Aweso.
Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Mbulu, Mhe. Michael Semindu, alimpongeza Mhe. Aweso kwa kuwa kiongozi msikivu na mchapakazi na kufanya vizuri kwenye Wizara ya Maji.
“Wilaya ya Mbulu maji yanatoka, na katika maeneo mengi huduma ya maji imefika. Hata Mbulu Vijijini wananchi wanapata maji kwa kutumia kadi za malipo ya kabla,” alisema Mhe. Semindu.
Naye Mbunge wa Mbulu Vijijini, Mhe. Dkt. Emanuel Nuwas, alimshukuru Mhe. Aweso kwa kutembelea jimbo lake na kumuomba amfikishie salamu Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kuendelea kutoa fedha nyingi kwa ajili ya miradi ya maendeleo katika Mbulu Vijijini.
Akihitimisha hotuba yake, Mhe. Aweso alimpongeza Mkuu wa Wilaya pamoja na viongozi wengine kwa ushirikiano mkubwa uliopo wilayani hapa.
Manyara Rs
Wizara ya Maji/Ministry of Water - Tanzania
Michael Semindu
Abubakar Kuuli