24/06/2026
Wizara ya Afya kupitia Kitengo cha Dharura na Maafa kwa kushirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI na CIHEB Tanzania kupitia Mradi wa Usalama wa Afya Duniani pamoja na wadau wa sekta ya afya, inaendelea kuimarisha huduma za dharura, ajali na uangalizi wa wagonjwa mahututi nchini kupitia usimamizi shirikishi na mafunzo kwa vitendo ya utayari dhidi ya ugonjwa wa Ebola yanayotolewa sehemu ya kazi kwa watumishi wa afya wanaohudumu katika Idara za Dharura (EMD) na Wagonjwa Mahututi (ICU).
Jitihada hizo zinalenga kuongeza uwezo wa kitaalamu kwa watoa huduma za afya ili kuboresha utayari, ufanisi na ubora wa huduma zinazotolewa wakati wa matukio ya dharura za afya, ikiwemo utambuzi wa mapema, kinga dhidi ya maambukizi, utoaji wa huduma salama pamoja na hatua za awali za kukabiliana na wagonjwa wanaohisiwa kuwa na Ebola.
Aidha, zoezi hilo ni mwendelezo wa mpango wa kitaifa unaolenga kuendelea kujenga uwezo wa watumishi wa afya nchini kupitia mafunzo ya vitendo na usimamizi wa karibu unaowezesha matumizi sahihi ya miongozo na taratibu za huduma za dharura.
Mafunzo haya yamefanyika katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Katavi ambapo watumishi wa afya wanaendelea kujengewa uwezo kupitia mafunzo yanayolenga kuimarisha utayari dhidi ya Ebola, matumizi sahihi ya vifaa vya kujikinga pamoja na utoaji wa huduma kwa kuzingatia usalama wa mtoa huduma na mgonjwa.
Sambamba na hilo, mafunzo hayo yanaendelea kuwawezesha watumishi wa afya kuimarisha ujuzi wa kitaaluma, kubadilishana uzoefu na kuongeza uwezo wa vituo vya kutolea huduma kukabiliana na changamoto mbalimbali za afya ya umma na dharura zinazoweza kujitokeza nchini.