Regional Commissioner's Office-Mara

Regional Commissioner's Office-Mara Contact information, map and directions, contact form, opening hours, services, ratings, photos, videos and announcements from Regional Commissioner's Office-Mara, Government Organization, Musoma.

Ukurasa huu wa Facebook ya Mkoa wa Mara ni maalumu katika kuweka matukio mbalimbali yanayofanyika katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mara katika kutekeleza majukumu yake.

SERIKALI IMETOA KIPAUMBELE KWA MIRADI YA KIMKAKATI YA UCHUKUZI MARA Mkuu wa Mkoa wa Mara Mhe. Kanali Evans Alfred Mtambi...
12/06/2026

SERIKALI IMETOA KIPAUMBELE KWA MIRADI YA KIMKAKATI YA UCHUKUZI MARA
Mkuu wa Mkoa wa Mara Mhe. Kanali Evans Alfred Mtambi leo tarehe 12 Juni, 2026 ameshiriki uzinduzi wa majaribio ya kutua na kuruka kwa ndege katika Uwanja wa Ndege Musoma na kumuomba Waziri wa Uchukuzi Mhe. Profesa Makame Mbarawa kuanza utekelezaji wa miradi ya kimkakati ya uchukuzi ya Mkoa wa Mara.
Akizungumza katika hafla hiyo, Mhe. Mtambi ameitaja miradi hiyo kuwa ni pamoja na mradi wa ujenzi wa reli kwa kiwango cha SGR kutoka Tanga hadi Musoma, mradi wa ukarabati na upanuzi wa Bandari ya Musoma na Ujenzi wa Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Serengeti.
“Kasi hii ya ukamilishaji wa Uwanja wa Ndege Musoma ninaomba ije pia katika miradi hii ya kimkakati ambayo ni muhimu sana kwa uchumi wa wananchi wa Mkoa wa Mara na Tanzania kwa ujumla” amesema Mhe. Mtambi.
Mhe. Mtambi amesema miradi hiyo muhimu katika kukuza uchumi wa wananchi wa Mkoa wa Mara na mikoa ya Kanda ya Ziwa kwa ujumla kwani itafungua fursa nyingi za kiuchumi nchini Tanzania na nchi jirani zinazopakana na Tanzania.
Kanali mtambi ametumia fursa hiyo kuwataka wananchi wa Mkoa wa Mara na watanzania kwa ujumla kuchangamkia fursa za kuanza kwa safari za ndege za abiria katika uwanja wa Ndege Musoma kuwekeza katika fursa mbalimbali za kiuchumi zilizopo katika Mkoa wa Mara.
Akizungumza katika hafla hiyo, Waziri wa Uchukuzi Prof. Makame Mbarawa akitoa ufafanuzi kuhusiana na utekelezaji wa miradi hiyo ya sekta ya uchukuzi amesema Serikali inaifanyia kazi miradi hiyo muhimu ili ianze kutekelezwa.
“Hii miradi Serikali bado inaifanyia kazi ili ianze kutekelezwa mapema iwezekanavyo” amesema Mhe. Mbarawa na kuongeza kuwa miradi hiyo itapewa kipaumbele kwa kuwa ni sehemu muhimu ya utekelezaji wa Dira ya Maendeleo ya Taifa ya Mwaka 2050.
Kwa upande wake, Mbunge wa Musoma Mhe. Mgore Miraji ameishukuru Serikali kwa kukamilisha ujenzi wa Uwanja wa Ndege Musoma na kuiomba Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA) kukamilisha kwa haraka ujenzi wa jengo la abiria katika Uwanja wa Ndege Musoma.
Mhe. Miraji ameiomba Wizara ya Uchukuzi kuanza ukarabati na upanuzi wa Bandari ya Musoma na ujenzi wa mradi wa reli ya SGR kutokea Tanga hadi Musoma ili kuweza kuchechemua fursa mbalimbali za kiuchumi katika Jimbo la Musoma.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge (Miundombinu) Mhe. Moshi Suleiman Kakoso (Mb.) ameipongeza Serikali kwa kukamilisha ujenzi wa uwanja huo na kuwataka wafanyabiashara na wawekezaji wakubwa kutoka Mkoa wa Mara kuwekeza katika Mkoa wa Mara.
“Mimi ninafahamu wafanyabiashara wakubwa ambao ni wazaliwa na wenyeji wa Mkoa wa Mara waliowekeza katika mikoa mbalimbali lakini hawana uwekezaji wowote katika Mkoa huu” amesema Mhe. Kakoso.
Mhe. Kakoso amelitaka Shirika la Ndege Tanzania (ATCL) kutangaza mapema kuhusu kuanza kwa safari za ndege zitakazotua katika Uwanja wa Ndege Musoma ili waweze kupata abiria na mizigo ya kutosha safari zitakapoanza.
Hafla ya uzinduzi wa majaribio ya kutua na kuruka kwa ndege Uwanja wa Ndege Musoma imefanyika katika uwanja huo na kuhudhuriwa na Kamati ya Usalama ya Mkoa, Wakuu wa Wilaya za Mkoa wa Mara, viongozi na watendaji wa Taasisi za Umma, wabunge wa Mkoa wa Mara, viongozi wa CCM Mkoa wa Mara, viongozi wa dini na wananchi.

NDEGE ZA ABIRIA KUANZA KUTUA MUSOMA JULAI, 2026 Waziri wa Uchukuzi Mheshimiwa Profesa Makame Mbarawa leo tarehe 12 Juni,...
12/06/2026

NDEGE ZA ABIRIA KUANZA KUTUA MUSOMA JULAI, 2026
Waziri wa Uchukuzi Mheshimiwa Profesa Makame Mbarawa leo tarehe 12 Juni, 2026 amezindua majaribio ya kuruka na kutua ndege katika Uwanja wa Ndege Musoma na kuahidi kuwa ndege za abiria kuanza kufanya kutua katika uwanja huo mwezi Julai, 2026.
Akizungumza katika hafla, Mhe. Mbarawa ambaye alikuwa mgeni rasmi ameliagiza Shirika la Ndege Tanzania (ATCL) kuharakisha utaratibu wa kuupanga Uwanja wa Ndege Musoma katika ratiba za ndege za abiria ili wananchi wa Mkoa wa Mara waweze kuanza kutumia usafiri huo.
“Ninaiagiza ATCL kuhakikisha kuwa inauingiza Uwanja wa Ndege Musoma katika ratiba za ndege haraka iwezekanavyo ili huduma za usafiri ziweze kuanza kutolewa kwa wananchi” amesema Mhe. Mbarawa.
Mhe. Mbarawa amesema majaribio ya utayari katika viwanja vya ndege vya Musoma na Shinyanga yanaashiria kukamilika kwa sehemu muhimu za miradi ya ukarabati na upanuzi wa viwanja hivyo na kuwa tayari kuanza kutoa huduma kwa wananchi.
Mhe. Mbarawa amezielekeza taasisi zinazohusika na mradi wa ukarabati na upanuzi wa Uwanja wa Ndege Musoma ambazo ni Wakala wa BArabara (TANROADS) na Mamlaka ya Uwanja wa Ndege (TAA) na wakandarasi kukamilisha sehemu iliyobakia katika mradi huo kwa mujibu wa mkataba wa utekelezaji wa mradi huo.
Akizungumza katika hafla hiyo, Mkuu wa Mkoa wa Mara Mhe. Kanali Evans Alfred Mtambi amesema kuzinduliwa kwa majaribio ya kuruka na kutua ndege katika Uwanja wa Ndege Musoma ni maendeleo makubwa yaliyofanywa na Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.
“Mara ya mwisho ndege kubwa kutua katika uwanja huu ilikuwa ni Machi, 2018 ambapo ndege ya Precision Air yenye uwezo wa kubeba abiria 45 ilifanya safari yake ya mwisho katika uwanja huu” amesema Mhe. Mtambi.
Mhe. Mtambi amewataka wananchi wa Mkoa wa Mara kuchangamkia fursa za kuanza kutumika kwa uwanja huo kuanzisha na kukuza shughuli zao ili kuimarisha uchumi wao kwa kuwa watakuwa na uwezo wa kusafiri na kusafirisha mizigo yao kwenda maeneo mbalimbali hapa nchini.
Kanali Mtambi amesema kwa sasa wananchi na wafanyabiashara wanauwezo wa kusafiri kwa muda mfupi kufika maeneo mbalimbali jambo ambalo amesema likitumika vizuri linaweza kuchechemua fursa nyingi za kiuchumi.
“Awali, muda mwingi ulikuwa unatumika katika usafiri lakini sasa ndani ya muda mfupi unakuwa umekamilisha safari au kusafirisha mzigo” amesema Mhe. Mtambi na kuongeza kuwa ni matumaini yake kuwa wananchi wa Mkoa wa Mara wataitumia vizuri fursa hiyo.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA) Abdul Mambokaleo amesema kuwa mradi wa ukarabati na upanuzi wa uwanja huo ulianza kutekelezwa mwaka 2021 kwa gharama ya shilingi bilioni 35.
Ndugu Mambokaleo amesema mradi huo pamoja na mambo mengine umeboresha njia ya kuruka ndege kutoka mita 1600 za changarawe yenye uwezo wa ndege za abiria 45 zilizokuwepo hadi mita 1750 za lami zenye uwezo wa kuwezesha ndege za abiria 80 kutua na kuruka katika uwanja huo.
Ndugu Mambokaleo ameahidi kuwa TAA baada ya kulipa fidia kwa wanachi itaanza kujenga kwa kasi jengo la abiria katika uwanja huo na kukamilisha majengo mengine ya kutolea huduma yanayoendelea kukamilishwa katika mradi huo wakati huduma nyingine zinaendelea kutolewa katika uwanja huo.
Hafla ya uzinduzi wa majaribio ya kutua na kuruka kwa ndege Uwanja wa Ndege Musoma imefanyika katika uwanja huo na kuhudhuriwa na Kamati ya Usalama ya Mkoa, Wakuu wa Wilaya za Mkoa wa Mara, viongozi na watendaji wa Taasisi za Umma, wabunge wa Mkoa wa Mara, viongozi wa CCM Mkoa wa Mara, viongozi wa dini na wananchi.

MTAMBI AKEMEA MAZOEA KATIKA MAANDALIZI YA MBIO ZA MWENGE MARA Mkuu wa Mkoa wa Mara Mhe. Kanali Evans Alfred Mtambi leo t...
30/04/2026

MTAMBI AKEMEA MAZOEA KATIKA MAANDALIZI YA MBIO ZA MWENGE MARA
Mkuu wa Mkoa wa Mara Mhe. Kanali Evans Alfred Mtambi leo tarehe 30 Aprili, 2026 ameongoza kikao cha pili cha Kamati ya Maandalizi ya Mbio za Mwenge wa Uhuru kwa Mkoa wa Mara na kutaka uwajibikaji wa watendaji na viongozi katika katika maandalizi ya Mbio za Mwenge wa Uhuru kwa mwaka 2026.
Akizungumza katika kikao hicho Mhe. Mtambi amewataka viongozi na watendaji kupunguza kufanya kazi kwa mazoea na kufanya maandalizi ya Mbio za Mwenge wa Uhuru kwa mwaka 2026 kulingana na vigezo, maelekezo na miongozo mahususi ya Mbio za Mwenge wa Uhuru kwa mwaka husika.
“Msiyachukulie maandalizi ya Mbio za Mwenge wa Uhuru kwa mazoea, kila mwaka kuna maelekezo na miongozo mipya inayotolewa, tunahitaji umakini na utulivu katika kuichambua na kuitekeleza miongozo husika ili tuweze kufanya vizuri zaidi kuliko mwaka uliopita” amesema Mhe. Mtambi.
Mhe. Mtambi amezitaka Halmashauri kuhakikisha zinatekeleza kwa ufanisi vigezo, miongozo na maelekezo yote ya Mbio za Mwenge wa Uhuru kwa mwaka 2026 ikiwa ni pamoja na kuhakikisha miradi yote itakayopitiwa na Mwenge wa Uhuru ina hati miliki, nyaraka za utekelezaji wa mradi hiyo zipo na kusimamia usajili wa vikundi vya vijana katika Mfumo wa Manunuzi Serikalini (NEST).
Kanali Mtambi amezitaka Halmashauri kuanzisha mashindano mbalimbali ya wanafunzi na washindi wapewe zawadi na Kiongozi wa Mbio za Mwenge ili kuongeza hamasa na ushiriki wa wananchi katika Mbio za Mwenge wa Uhuru mwaka 2026 na ameipongeza Halmashauri wa Mji wa Bunda ambayo mwaka 2025 ilitekeleza kikamilifu agizo hilo.
Mhe. Mtambi amezitaka Wakala wa Barabara za Mijini na Vijijini (TARURA), Wakala wa Maji Vijijini (RUWASA) na Mamlaka za Maji katika Mkoa wa Mara kuhakikisha zinaandaa miradi ya barabara na maji inayokidhi vigezo vya Mbio za Mwenge wa Uhuru kwa kila Halmashauri ili Halmashauri ziweze kutimiza vigezo vinavyohitajika katika Mbio za Mwenge wa Uhuru.
Mhe. Mtambi amewataka wakuu wa Taasisi ambao kwa mujibu wa mwongozo Mbio za Mwenge wa Uhuru kwa mwaka 2026 ni wajumbe wa Kamati ya Mwenge ya Mkoa, walioalikwa kushiriki kikao hicho wakatuma wawakilishi bila taarifa kuwasilisha maelezo ya sababu za kutokushiriki katika kikao hicho kwa Katibu Tawala Mkoa tarehe 04 Mei, 2026.
Mkuu wa Mkoa amewataka washiriki kuhakikisha maandalizi ya Mbio za Mwenye wa Uhuru yanaenda sambamba na maandalizi ya maadhimisho ya sherehe za wakulima (NANENANE) ambayo yanatarajiwa kufanyika wakati huo huo ambapo Mkoa utakuwa katika Mbio za Mwenge wa Uhuru.
Kwa upande wake, Mratibu wa Mwenge wa Uhuru Mkoa wa Mara Ndugu Fidel Baragaye amesema kwa mwaka 2026 Mwenge wa Uhuru utapokelewa katika Mkoa wa Mara tarehe 01 Agosti, 2026 kutoka Mkoa wa Simuyu na utakimbizwa katika Halmashauri tisa na baadaye kukabidhiwa Mkoa wa Mwanza tarehe 10 Agosti, 2026.
Ndugu Baragaye amesema kwa mwaka 2026, mwongozo wa Mbio za Mwenge wa Uhuru umebadilisha vigezo, wajumbe wa k**ati za Mwenge wa Uhuru za Mkoa na Wilaya ili kuongeza hamasa na kuhakikisha wananchi wengi zaidi wanashiriki katika Mbio za Mwenge wa Uhuru.
Katika kikao hicho pia Ndugu Baragaye amewasilisha vigezo, mwongozo, mpango wa Mkoa wa maandalizi na ratiba za Mbio za Mwenge wa Uhuru kwa mwaka 2026 katika Mkoa wa Mara na kuwataka washiriki wa kikao hicho kuusoma na kuutekeleza mwongozo wa Mbio za Mwenge wa Uhuru kikamilifu.
Ndugu Baragaye amesema ujumbe mkuu wa Mbio za Mwenge wa Uhuru kwa mwaka 2026 ni Amani, Umoja na Mshik**ani wa Kitaifa ukiongozwa na kauli mbiu inayosema “Tanzania ni Yetu Sote, Tushik**ane kwa Pamoja kuleta Maendeleo”.
Katika kikao hicho, Mkuu wa Mkoa wa Mara amegawa nakala za vitabu vya miaka sitini ya Mbio za Mwenge wa Uhuru na mwongozo wa Mbio za Mwenge wa Uhuru kwa mwaka 2026 kwa Wakuu wa Wilaya na Wakurugenzi wa Halmashauri za Mkoa wa Mara kwa ajili ya rejea katika maandalizi ya mbio za Mwenge wa Uhuru katika maeneo yao .
Kikao hicho kimehudhuliwa na wajumbe wa Kamati ya Mwenge wa Mkoa ambayo inawahusisha Wajumbe wa Kamati ya Usalama ya Mkoa, Menejimenti ya Sekretarieti ya Mkoa, Wakuu wa Taasisi za Umma na Fedha na waalikwa wa kikao hicho walikuwa Wakuu wa Wilaya, Wakurugenzi wa Halmashauri na Waratibu wa Mbio za Mwenge kwa ngazi za Halmashauri.

MARA YAONGOZA KITAIFA KATIKA UANDIKISHAJI WANAFUNZI WA AWALI Mkoa wa Mara umeongoza kitaifa katika uandikishaji wawanafu...
06/03/2026

MARA YAONGOZA KITAIFA KATIKA UANDIKISHAJI WANAFUNZI WA AWALI
Mkoa wa Mara umeongoza kitaifa katika uandikishaji wawanafunzi darasa la awali maoteo yalikuwa kuandikisha wanafunzi 84,634; jumla ya wanafunzi walioandikishwa ni 89,160 sawa na asilimia 105.35. hadi tarehe 28 Februari, 2026
Akizungumza katika kikao cha tathmini ya masuala ya afya, Mkuu wa Mkoa wa Mara Mhe. Kanali Evans Alfred Mtambi amewapongeza viongozi na wasimamizi wa sekta ya Elimu kwa jitihada kubwa zilizofanyika katika suala la uandikishaji wa wanafunzi.
Mhe. Mtambi amesema katika uandikishaji wa wanafunzi kuanza shule inaonyesha Mkoa wa Mara umejitahidi kuongeza uandikshaji wa wanafunzi kwa madarasa ya awali na darasa la kwanza na kuwataka wasimamizi kuongeza mkazo katika uandikishaji wa kidato cha kwanza.
Akizungumza katika kikao cha tathmini ya lishe, Mhe. Mtambi amewataka Wakuu wa Wilaya na viongozi wa Halmashauri zote kusimamia kikamilifu suala la utoaji wa chakula shuleni na kuhakikisha kuwa wanafunzi wote wanapata angalau mlo mmoja wawapo shuleni.
Aidha, Mhe. Mtambi amewataka viongozi kufuatilia masuala ya utoro wa wanafunzi na hususan wanafunzi wa shule za Sekondari ambao wengi wao hawahudhurii masomo k**a inavyotakiwa kutokana na sababu mbalimbali.
Taarifa ya tathmini ya utekelezaji wa shughuli za elimu katika kipindi cha Julai, 2025 hadi Machi, 2026 iliyotolewa na Katibu Tawala Msaidizi Sehemu ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Dkt. Elpidius Kaganda imesema kuwa katika uandikishaji wa wanafunzi wa shule za awali, wavulana ni 45,590 na wasichana ni 43,570.
Taarifa ya hiyo inaonyesha kuwa Darasa la Kwanza ni watoto 82,698 ambao ni sawa na asilimia 98.51 kati ya maoteo ya kuandkisha watoto 83,945 waliopangwa kuandikishwa darasa la kwanza.
Dkt. Baganda amesema kuwa jumla ya Wanakisomo wa elimu ya Watu Wazima nje ya mfumo rasmi (Memkwa) 568 ambapo wavulana wameandikishwa 297 na wasichana 271 hadi tarehe 28 Februari, 2026.
Aidha, Kidato cha kwanza jumla ya wanafunzi 35,193 wameripoti na kuanza masomo katika shule za Sekondari za Serikali kati ya wanafunzi 41,396 waliochaguliwa kujiunga na shule hizo sawa na asilimia 85.02 ya watoto wote waliochaguliwa.
Uandikishaji wa wanafunzi wa madarasa ya awali, darasa la kwanza na kidato cha kwanza hapa nchini unaendelea hadi tarehe 31 Machi, 2026.
Kikao hicho kimehudhuriwa na Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa wa Mara Ndugu Dominicus Lusasi, Menejimenti ya Mkoa wa Mara, Wakuu wa Wilaya, Makatibu Tawala wa Wilaya, Wakurugenzi na wataalamu wa Halmashauri.

MTAMBI ATAKA MAANDALIZI YA MBIO ZA MWENGE WA UHURU Mkuu wa Mkoa wa Mara Mhe. Kanali Evans Alfred Mtambi leo tarehe 06 Ma...
06/03/2026

MTAMBI ATAKA MAANDALIZI YA MBIO ZA MWENGE WA UHURU
Mkuu wa Mkoa wa Mara Mhe. Kanali Evans Alfred Mtambi leo tarehe 06 Machi, 2026 ameongoza kikao cha kufanya tathmini ya mbio za Mwenge wa Uhuru kwa mwaka 2025 na kupokea taarifa za ratiba ya mbio hizo kwa mwaka 2026 na kuzitaka Wilaya na Halmashauri kuanza maandalizi ya mbio za Mwenge wa Uhuru.
Akizungumza katika kikao hicho, Mhe. Mtambi amesema maandalizi yakifanyika mapema yatausaidia Mkoa kukagua na kujiridhisha kuhusiana na miradi ya iliyochaguliwa kwa ajili ya mbio za mwenge mwaka 2026.
“Ninataka maandalizi yaanze mapema ili kusiwe na kukimbizana siku zikikaribia, uchaguzi wa miradi ufanyike kwa makani kwa kuzingatia miongozo ya Mbio za Mwenge wa Uhuru” amesema mhe. Mtambi
Awali, akitoa taarifa katika kikao hicho Mratibu wa Mbio za Mwenge Mkoa wa Mara Ndugu Fidel Baragaye amesema matokeo yam bio za Mwenge wa Uhuru mwaka 2025 Mkoa wa Mara ulipata alama 56 ma kushika nafasi ya saba kitaifa kati ya mikoa 31 ya Tanzania iliyoshiriki kwenye mbio hizo.
Bwana Balagaye amezitaja Halmashauri zilizofanya vizuri kuwa ni Halmashauri ya Wilaya ya Serengeti iliyopata alama 68.2, Manispaa ya Musoma alama 67 na Halmashauri ya Mji wa Bunda alama 63.8 na Halmashauri ya Mji wa Tarime imeshika nafasi ya mwisho baada ya kupata alama 58.
Bwana Balagaye ameyataka mafanikio yaliyopatikana kuwa ni pamoja na miradi yote 68 iliyotembelewa na kukaguliwa kupitishwa, wananchi kujitokeza kwa wingi kuulaki Mwenge wa Uhuru katika maeneo yote uliyopita, amani kutawala katika maeneo Mwenge wa Uhuru ulipita na ushirikiano mzuri baina ya wadau, viongozi na wananchi.
Ndugu Balagaye amesema kwa mwaka 2026 Mwenge wa Uhuru utapokelewa katika Mkoa wa Mara tarehe 01 Agosti, 2026 kutoka Mkoa wa Simiyu, utakimbizwa Mkoa wa Mara na kukabidhiwa Mkoa wa Mwanza tarehe 10 Agosti, 2026 ukiwa na kauli mbinu “Tanzania ni Yetu Sote, Tushik**ane kwa Pamoja Kuleta Maendeleo”.
Mapendekezo ya ratiba yanaonyesha kuwa Halmashauri ya Mji wa Bunda itapokea tarehe 01 Agosti, 2026; Halmashauri ya Wilaya ya Bunda tarehe 02 Agosti, 2026, Halmashauri ya Wilaya ya Serengeti tarehe 03 Agosti, 2026, Halmashauri ya Wilaya ya Tarime tarehe 04 Agosti, 2026 na Halmashauri ya Mji wa Tarime tarehe 05 Agosti, 2026.
Mbio za Mwenge wa Uhuru kwa mwaka 2026 zitazinduliwa rasmi katika Mkoa wa Kaskazini Pemba tarehe 02 Aprili, 2026 na kilele cha Mbio za Mwenge wa Uhuru na Kumbukumbu ya Baba wa Taifa na wiki ya vijana kitaifa zitafanyika katika Mkoa wa Rukwa tarehe 14 Oktoba, 2026.
Katika kikao hicho, Halmashauri ya Mji wa Tarime ambayo ilikuwa yam mwisho kimkoa imekabidhiwa kinyago wakati Halmashauri ya Wilaya ya Serengeti iliyoongoza katika mbio hizo kimkoa imekabidhiwa cheti cha pongezi.
Kikao hicho kimehudhuriwa na Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa wa Mara Ndugu Dominicus Lusasi, Menejimenti ya Mkoa wa Mara, Wakuu wa Wilaya, Makatibu Tawala wa Wilaya, Wakurugenzi na wataalamu wa Halmashauri.

MATUMIZI YA FEDHA ZA LISHE YAFIKIA ASILIMIA 94.67 MARA Mkuu wa Mkoa wa Mara Mhe. Kanali Evans Alfred Mtambi leo tarehe 0...
06/03/2026

MATUMIZI YA FEDHA ZA LISHE YAFIKIA ASILIMIA 94.67 MARA
Mkuu wa Mkoa wa Mara Mhe. Kanali Evans Alfred Mtambi leo tarehe 06 Machi, 2026 na kuzipongeza Halmashauri kwa kutoa kipaumbele kwenye utekelezaji wa afua za lishe na kuweza kutumia asilimia 94.67 ya bajeti ya Julai- Disemba kwa mwaka wa fedha 2025/2026.
Akizungumza katika ufunguzi wa kikao hicho, Mhe. Mtambi amesema hayo ni mafanikio makubwa kwa kuwa Mkoa wa Mara ulipoanza kutekeleza mkataba wa lishe mwaka 2017/2018 matumizi ya fedha kwa afua za lishe yalikuwa ni asilimia 18 tu ya fedha zote zilizokuwa zimetengwa.
“Kwa sasa Mkoa wetu umeweka kipaumbele kikubwa sana katika kikubwa katika utekelezaji wa afua za lishe kwa kweli ninawapongeza sana viongozi na watendaji wa Mamlaka za Mitaa” amesema Mhe. Mtambi.
Kanali Mtambi pia amezielekeza Halmashauri kuhakikisha kuwa utengaji wa fedha za lishe katika bajeti ya mwaka wa fedha 2026/2027 kuzingatia changamoto za lishe zilizopo kwenye halmashauri zao.
Mheshimiwa Mtambi amezitaka Halmashauri kukamilisha matumizi ya fedha za lishe kwa wakati na kuacha kubadilisha matumizi ya fedha hizo kwa ajili ya kufanyia shughuli nyingine na kuzingatia utoaji wa chakula kwa wanafunzi shuleni.
Amezitaka Halmashauri kufanya tathmini ya hali ya lishe kwa watoto chini ya miaka mitano, usimamizi na utekelezaji kwa ufasaha wa siku ya afya na lishe ya Kijiji/Mtaa na utengaji bajeti ya wahudumu wa afya ngazi ya jamii walau wawili kwa kila mtaa/ kijiji kwa Halmashauri zote.
Aidha, Kanali Mtambi amezitaka Halmashauri kukaa vikao vya tathmini ya lishe kwa wakati mara tu robo mwaka husika inapoishia.
Mhe. Mtambi amewataka wananchi wa Mkoa wa Mara kuchukua tahadhari kutokana na tahadhari za uwepo wa mvua nyingi katika msimu wa masika kwa muda wa kuanzia mwezi Machi hadi Mei, 2026.
Mhe. Mtambi amewataka wananchi kukabiliana na magonjwaya mlipuko na hususan kipindupindu, homa za matumbo wakati huu wa mvua nyingi na kuwataka wananchi kuzingatia kanuni za afya ili kuepukana na magonjwa yanayotokana na uchafu.
Kanali Mtambi amewataka viongozi kusimamia usafi wa mazingira wakati wote na kuwaelimisha wananchi kuacha kutupa takataka hovyo katika maeneo yao na kuwataka madereva kuchukua tahadhari wakati wa mvua wakiwa wanaendesha vyombo vya moto ili kunusuru maisha ya wananchi.
Awali akitoa taarifa kuhusu masuala ya lishe, Afisa Lishe wa Mkoa wa Mara Ndugu Benson Sanga amezishauri Halmashauri kuendelea kutenga fedha kutoka katika vyanzo vya uhakika kwa ajili ya utekelezaji wa afua za lishe.
Ndugu Sanga amesema, wataalamu wa afya wanapendekeza kuwepo kwa ratiba ya vikao vya masuala ya lishe kwa Halmashauri zote za Mkoa wa Mara na kuwepo kwa mizani ya kupima afya katika vijiji na mitaa.
Aidha, amewaomba Wakuu wa Wilaya na Wakurugenzi wa Halmashauri kushiriki vikao vya masuala ya lishe ili kutoa maamuzi yanayotakiwa katika vikao hiyo baada ya taarifa kuonyesha kuwa vikao vingi vya masuala ya lishe kuongozwa na makaimu katika ngazi za Halmashauri na Wilaya.
Kikao hicho kimepokea pia taarifa za utoaji wa chanjo, tahadhari ya mwelekeo wa mvua za msimu wa masika kuanzia Machi hadi Mei, 2026 na hatua zinazotakiwa kuchukuliwa kudhibiti madhara ya mvua hizo kwa wananchi na miundombinu ya Mkoa wa Mara.
Kikao hicho kimehudhuriwa na Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa wa Mara Ndugu Dominicus Lusasi, Menejimenti ya Mkoa wa Mara, Wakuu wa Wilaya, Makatibu Tawala wa Wilaya, Wakurugenzi na wataalamu wa Halmashauri.

RC MTAMBI AMPOKEA MKURUGENZI MKUU WA TAKUKURU Mkuu wa Mkoa wa Mara Mhe. Kanali Evans Alfred Mtambi leo tarehe 06 Machi, ...
06/03/2026

RC MTAMBI AMPOKEA MKURUGENZI MKUU WA TAKUKURU
Mkuu wa Mkoa wa Mara Mhe. Kanali Evans Alfred Mtambi leo tarehe 06 Machi, 2026 amempokea na kuzungumza na Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Ndugu Crispin Chalamila aliyepo katika Mkoa wa Mara kuendelea na majukumu yake ya kikazi.
Akizungumza wakati wa mapokezi hayo, Mhe. Mtambi amemkaribisha Ndugu Chalamila na kumpa taarifa ya Mkoa wa Mara na kumhakikishia kuwa hali ya ulinzi na usalama wa Mkoa wa Mara ipo salama na wananchi wanaendelea kutekeleza majukumu yao ya kila siku.
Mhe. Mtambi ametumia muda huo kuishukuru na kuipongeza TAKUKURU Mkoa wa Mara kwa ushirikiano wanaoutoa katika kudhibiti matumizi mabaya ya fedha za umma katika miradi mbalimbali ya Serikali katika Mkoa wa Mara.
“Kulikuwa na changamoto makusanyo katika vivuko vinavyosimamiwa na TEMESA (Wakala wa Ufundi na Umeme) baada ya TAKUKURU kuingia na kulifanyia kazi sasa hivi mapato yamepanda na vivuko vinaendelea vizuri” amesema Mhe. Mtambi.
Mhe. Mtambi amesema TAKUKURU Mkoa wa Mara imeisaidia Serikali kwa kutoa elimu kwa wananchi, watendaji na viongozi kuhusu rushwa na madhara yake na kudhibiti vitendo vya rushwa na hususan katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo.
Kwa upande wake, Ndugu Chalamila amesema kwa sasa TAKUKURU imejikita zaidi katika kuzuia rushwa kwa kutoa elimu kwa umma, ukaguzi wa mifumo na ufuatiliaji wa miradi ya maendeleo inayotekelezwa na Serikali.
Ndugu Chalamila amemshukuru Mkuu wa Mkoa kwa mapokezi mazuri aliyoyapata kuanzia tarehe 04 Machi, 2025 alipoanza ziara katika Mkoa wa Mara ambapo alikuwa katika Wilaya ya Bunda kwa ajili ya kuzindua ofisi ya TAKUKURU Wilaya ya Bunda na kuzungumza na watumishi.
Ndugu Chalamila amesema leo anategemea kukabidhi mashine za watoto waliozaliwa kabla ya muda kwa Hospitali ya Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere na kuzungumza na watumishi wa TAKUKURU.
Akizungumzia msaada huo, Ndugu Chalamila amesema msaada huo ni sehemu ya kurudisha kwenye jamii na umetolewa baada ya utafiti wao kubaini hospitali hazina hiyo mashine na unatolewa katika Hospitali za Rufaa za Mikoa na Mara ni Mkoa wa 15 kupokea mashine hizo.
Mapokezi hayo yamehudhuriwa pia na Katibu Tawala wa Mkoa wa Mara Ndugu Gerald Musabila Kusaya, Maafisa kutoka TAKUKURU makao makuu na Sekretraieti ya Mkoa wa Mara.

RC MTAMBI AWEKA JIWE LA MSINGI KITUO CHA AFYA KATARYO Mkuu wa Mkoa wa Mara Mhe. Kanali Evans Alfred Mtambi leo tarehe 04...
06/03/2026

RC MTAMBI AWEKA JIWE LA MSINGI KITUO CHA AFYA KATARYO
Mkuu wa Mkoa wa Mara Mhe. Kanali Evans Alfred Mtambi leo tarehe 04 Machi, 2026 amefanya ziara Halmashauri ya Wilaya ya Musoma na kuweka jiwe la msingi katika mradi wa ujenzi wa Kituo cha Afya Ketaryo katika kata ya Tegeruka, Halmashauri ya Wilaya ya Musoma.
Akizungumza katika hafla hiyo, Mhe. Mtambi ameipongeza Halmashauri ya Wilaya ya Musoma kwa utekelezaji mzuri wa miradi ya maendeleo na kutoa mfano kuwa fedha za mradi huo zilitolewa katika Halmashauri nyingi za Mkoa wa Mara lakini Halmashauri ya Wilaya ya Musoma jengo lipo hatua nzuri.
“Mradi huu umetekelezwa vizuri na nimeridhishwa na ubora wa mradi huu k**a ilivyo katika miradi mingi ya Halmashauri ya Wilaya ya Musoma” amesema Mhe. Mtambi na kuongeza kuwa Halmashauri nyingine zilizopewa mradi k**a huo bado ujenzi upo katika hatua za msingi.
Mhe. Mtambi amewataka watumishi watakaopangiwa katika Kituo hicho kufanyakazi na kutoa huduma bora kwa kuzingatia weledi wa kitaaluma kwa wananchi wa Kata ya Tegeruka na maeneo jirani.
Mhe. Mtambi amewataka wananchi kuyatunza majengo ya Kituo hicho na kuwapongeza kwa kuchangia shilingi milioni 15 katika ujenzi wa kituo hicho huku mwekezaji wa eneo hilo akijenga nyumba moja ya mtumishi katika kituo hicho.
Mhe. Mtambi amewataka wananchi kuishi na watumishi wanaofanyakazi katika maeneo yao vizuri ili waweze kutoa huduma bora zenye manufaa kwao na hususan walimu ambao wanafundisha katika maeneo hayo.
Akizungumza na wananchi wa Kata ya Tegeruka Mhe. Mtambi ameitaka Kamati ya Usalama ya Wilaya ya Musoma kurudi katika eneo hilo ili kuchunguza masuala ya usalama yaliyolalamikiwa na wananchi na hususan wizi wa mifugo na mali za wananchi.
Awali, akitoa taarifa ya ujenzi wa mradi huyo, Mganga Mkuu wa Halmashauri ya Wilaya ya Musoma Dkt. Joseph Fwoma amesema ujenzi wa kituo hicho umeanza katika mwaka wa fedha 2025/2026 kwa gharama ya shilingi milioni 250.
Dkt. Fwoma amesema lengo la mradi huo ni kusogeza huduma kwa wananchi wa Kata ya Tegeruka yenye wananchi 13,229 ambao hapo awali kabla ya kujengwa kwa mradi huo walikuwa wanapata huduma mbali na eneo hilo.
Akiwa katika eneo hilo, Mhe. Mtambi alizungumza na kusikiliza kero za wananchi wa Kata ya Tegeruka.
Ziara hiyo ilihudhuriwa pia na Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya CCM Musoma Vijijini, Mkuu wa Wilaya ya Musoma, Kamati ya Usalama ya Wilaya, Kamati ya usimamizi ya Afya Mkoa wa Mara, Mwenyekiti wa Halmashauri Mkurugenzi wa Halmashauri na maafisa wa Halmashauri ya Wilaya ya Musoma.

Wananchi wote wa Mkoa wa Mara mnakaribishwa kushiriki maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani tarehe 08 Machi, 2026
06/03/2026

Wananchi wote wa Mkoa wa Mara mnakaribishwa kushiriki maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani tarehe 08 Machi, 2026

RC AZITAKA HALMASHAURI KUJIPANGA KUPOKEA WANAFUNZI KIDATO CHA KWANZA 2028Mkuu wa Mkoa wa Mara Mhe. Kanali Evans Alfred M...
03/03/2026

RC AZITAKA HALMASHAURI KUJIPANGA KUPOKEA WANAFUNZI KIDATO CHA KWANZA 2028
Mkuu wa Mkoa wa Mara Mhe. Kanali Evans Alfred Mtambi amezitaka Halmashauri za Mkoa wa Mara kujiandaa kupokea wanafunzi wa kidato cha kwanza mwaka 2028 kufuatia kuanza kwa utekelezaji wa Sera mpya ya Elimu itakayolazimu wanafunzi wa darasa la sita na darasa la saba kujiunga na kidato cha kwanza kwa pamoja.
Akizungumza katika kikao hicho, Mhe. Mtambi amezitaka Halmashauri kuweka kipaumbele katika kuwapokea wanafunzi hao kuanzia bajeti ya mapato ya ndani ya mwaka wa fedha 2026/2027 inayoendelea kuandaliwa wakati huu kwa ajili ya kuboresha miundombinu ya elimu itakayotumika kupokea wanafunzi.
“Wanafunzi wa Kidato cha Kwanza watakaopokelewa mwaka 2028 watakuwa ni zaidi ya mara mbili ya wanafunzi wote tuliozoea kuwapokea katika miaka yote, bila kujipanga vizuri Mkoa hautakuwa na miundombinu yakutosha ya kukizi ongezeko hilo” amesema Mhe. Mtambi.
Mhe. Mtambi pia amewataka wajumbe wa kikao hicho kuendelea kutoa elimu na kuwahamasisha wazazi kupeleka watoto wao shule na kuhakikisha wanasoma na kushirikiana na wasimamizi wa elimu wa ngazi mbalimbali kudhibiti utoro wa wanafunzi wa shule za msingi na sekondari ili kuboresha elimu.
Kanali Mtambi amesema Mkoa wa Mara umejipanga kuhakikisha walimu wanafundisha na wanafunzi wanajifunza na kuhakikisha ufaulu wa wanafunzi katika matokeo ya mitihani ya kitaifa yanakuwa vizuri na wastani wa ufaulu wa Mkoa unakuwa mzuri zaidi.
Wakati huo huo, Kamati ya Ushauri ya Mkoa wa Mara imepitisha makadirio ya bajeti ya shilingi 488,996,863,000/= kwa mwaka wa fedha 2026/2027 ambapo kati yake shilingi 18,297,356,000/= kwa ajili ya Sekretarieti ya Mkoa wa Mara wakati shilingi 470,699,507,000/= ni kwa ajili ya Mamlaka za Serikali za Mitaa.
Akizungumza wakati wa kuwasilisha bajeti hiyo, Katibu Tawala Msaidizi Sehemu ya Mipango na Uratibu Ndugu Emmanuel Mazengo vipaumbele vya bajeti kwa mwaka 2026/2027 kwa Sekretarieti ya Mkoa wa Mara kuwa ni usimamizi wa masuala ya ulinzi na usalama; uimarishaji wa utawala bora, uwajibikaji, uwazi, kwa kufanya vika vya kisheria; uratibu wa usimamizi wa utoaji wa huduma za kijamii.
Ndugu Mazengo amesema mambo mengine yaliyopewa kipaumbele ni uratibu wa uwezeshaji wa wananchi kiuchumi; uboreshaji wa mazingira ya kufanyiakazi na makazi ya viongozi Mkoa na Wilaya; uendelezaji wa rasilimaliwatu; na ufuatiliaji na utatuzi wa kero na malalamiko ya wananchi.
Kamati ya ushauri ya Mkoa pia imepokea taarifa ya miradi ya maendeleo itakayotekelezwa katika sekta ya maji na umeme kwa mwaka wa fedha 2026/2027; taarifa ya ukatili wa kijinsia katika Mkoa wa Mara na taarifa ya uhakiki na utoaji wa kadi za Bima ya Afya kwa Wote katika Mkoa wa Mara.
Kikao cha RCC kimehudhuriwa na Katibu Tawala wa Mkoa wa Mara, Wakuu wa Wilaya, Kamati ya Usalama ya Mkoa, Menejimenti ya Sekretarieti ya Mkoa wa Mara, Meya, Wenyeviti na wataalamu wa Halmashauri, viongozi wa dini, viongozi wa vyama vya siasa na wadau wa maendeleo.

Address

Musoma

Alerts

Be the first to know and let us send you an email when Regional Commissioner's Office-Mara posts news and promotions. Your email address will not be used for any other purpose, and you can unsubscribe at any time.

Contact The Organization

Send a message to Regional Commissioner's Office-Mara:

Share