12/06/2026
SERIKALI IMETOA KIPAUMBELE KWA MIRADI YA KIMKAKATI YA UCHUKUZI MARA
Mkuu wa Mkoa wa Mara Mhe. Kanali Evans Alfred Mtambi leo tarehe 12 Juni, 2026 ameshiriki uzinduzi wa majaribio ya kutua na kuruka kwa ndege katika Uwanja wa Ndege Musoma na kumuomba Waziri wa Uchukuzi Mhe. Profesa Makame Mbarawa kuanza utekelezaji wa miradi ya kimkakati ya uchukuzi ya Mkoa wa Mara.
Akizungumza katika hafla hiyo, Mhe. Mtambi ameitaja miradi hiyo kuwa ni pamoja na mradi wa ujenzi wa reli kwa kiwango cha SGR kutoka Tanga hadi Musoma, mradi wa ukarabati na upanuzi wa Bandari ya Musoma na Ujenzi wa Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Serengeti.
“Kasi hii ya ukamilishaji wa Uwanja wa Ndege Musoma ninaomba ije pia katika miradi hii ya kimkakati ambayo ni muhimu sana kwa uchumi wa wananchi wa Mkoa wa Mara na Tanzania kwa ujumla” amesema Mhe. Mtambi.
Mhe. Mtambi amesema miradi hiyo muhimu katika kukuza uchumi wa wananchi wa Mkoa wa Mara na mikoa ya Kanda ya Ziwa kwa ujumla kwani itafungua fursa nyingi za kiuchumi nchini Tanzania na nchi jirani zinazopakana na Tanzania.
Kanali mtambi ametumia fursa hiyo kuwataka wananchi wa Mkoa wa Mara na watanzania kwa ujumla kuchangamkia fursa za kuanza kwa safari za ndege za abiria katika uwanja wa Ndege Musoma kuwekeza katika fursa mbalimbali za kiuchumi zilizopo katika Mkoa wa Mara.
Akizungumza katika hafla hiyo, Waziri wa Uchukuzi Prof. Makame Mbarawa akitoa ufafanuzi kuhusiana na utekelezaji wa miradi hiyo ya sekta ya uchukuzi amesema Serikali inaifanyia kazi miradi hiyo muhimu ili ianze kutekelezwa.
“Hii miradi Serikali bado inaifanyia kazi ili ianze kutekelezwa mapema iwezekanavyo” amesema Mhe. Mbarawa na kuongeza kuwa miradi hiyo itapewa kipaumbele kwa kuwa ni sehemu muhimu ya utekelezaji wa Dira ya Maendeleo ya Taifa ya Mwaka 2050.
Kwa upande wake, Mbunge wa Musoma Mhe. Mgore Miraji ameishukuru Serikali kwa kukamilisha ujenzi wa Uwanja wa Ndege Musoma na kuiomba Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA) kukamilisha kwa haraka ujenzi wa jengo la abiria katika Uwanja wa Ndege Musoma.
Mhe. Miraji ameiomba Wizara ya Uchukuzi kuanza ukarabati na upanuzi wa Bandari ya Musoma na ujenzi wa mradi wa reli ya SGR kutokea Tanga hadi Musoma ili kuweza kuchechemua fursa mbalimbali za kiuchumi katika Jimbo la Musoma.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge (Miundombinu) Mhe. Moshi Suleiman Kakoso (Mb.) ameipongeza Serikali kwa kukamilisha ujenzi wa uwanja huo na kuwataka wafanyabiashara na wawekezaji wakubwa kutoka Mkoa wa Mara kuwekeza katika Mkoa wa Mara.
“Mimi ninafahamu wafanyabiashara wakubwa ambao ni wazaliwa na wenyeji wa Mkoa wa Mara waliowekeza katika mikoa mbalimbali lakini hawana uwekezaji wowote katika Mkoa huu” amesema Mhe. Kakoso.
Mhe. Kakoso amelitaka Shirika la Ndege Tanzania (ATCL) kutangaza mapema kuhusu kuanza kwa safari za ndege zitakazotua katika Uwanja wa Ndege Musoma ili waweze kupata abiria na mizigo ya kutosha safari zitakapoanza.
Hafla ya uzinduzi wa majaribio ya kutua na kuruka kwa ndege Uwanja wa Ndege Musoma imefanyika katika uwanja huo na kuhudhuriwa na Kamati ya Usalama ya Mkoa, Wakuu wa Wilaya za Mkoa wa Mara, viongozi na watendaji wa Taasisi za Umma, wabunge wa Mkoa wa Mara, viongozi wa CCM Mkoa wa Mara, viongozi wa dini na wananchi.