18/05/2026
Katika kuadhimisha Siku ya Ziwa Victoria, Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Mwanza (MWAUWASA) kwa kushirikiana na Bodi ya Maji Bonde la Ziwa Victoria, leo Mei 18, 2026 wameungana na Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Said Mtanda pamoja na viongozi wengine wa serikali akiwemo Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Maji Bi. Rose Ambrose kupanda zaidi ya miti 2,000 katika chanzo cha maji Butimba. Zoezi hili linaongeza idadi ya miti iliyokwisha pandwa kufikia zaidi ya 6,500 katika eneo hilo muhimu.
Akizungumza katika kilele cha maadhimisho hayo, Mkuu wa Mkoa Said Mtanda aliwapongeza wananchi na wadau mbalimbali kwa kujitokeza kwa wingi kushiriki katika juhudi za uhifadhi wa mazingira. Alisema hatua hiyo ni muhimu katika kulinda rasilimali za maji, hususan Ziwa Victoria ambalo lina mchango mkubwa katika maisha ya watu.
Aidha, Mkuu wa Mkoa alieleza kuwa kwa mwaka huu, maadhimisho ya Siku ya Ziwa Victoria yamefanyika kwa mara ya kwanza katika ngazi ya Jumuiya ya Afrika Mashariki, ambapo wakuu wa nchi na mawaziri wa sekta za maji na mazingira walikubaliana kuwa na siku maalum ya kuenzi na kulinda ziwa hilo.
“Ziwa Victoria ni muhimu sana kwa huduma mbalimbali za kijamii na kiuchumi. Maji ni afya, maji ni uchumi na maji ni maendeleo,” alisisitiza Said Mtanda huku akiwataka wananchi kuhakikisha wanatunza miti iliyopandwa ili iweze kudumu na kutoa manufaa yaliyokusudiwa.
Kwa upande wake, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji, Bi. Rose Ambrose, alimshukuru Mkuu wa Mkoa kwa kushiriki kikamilifu katika tukio hilo, na kupongeza juhudi za wadau wote wanaoshiriki katika uhifadhi wa vyanzo vya maji.
Aliongeza kuwa Wizara ya Maji kupitia Bodi ya Maji Bonde la Ziwa Victoria imejiwekea lengo la kupanda miti 10,000 rafiki kwa vyanzo vya maji katika eneo la Butimba, ambapo hadi sasa miti zaidi ya 6,500 tayari imepandwa.
Miti iliyopandwa inalenga kulinda vyanzo vya maji, kuzuia mmomonyoko wa ardhi, kupunguza athari za mabadiliko ya tabianchi na kuboresha mazingira kwa ujumla katika eneo la chanzo cha Butimba.
Maadhimisho hayo yameongozwa na kauli mbiu isemayo: “Maji yetu, mustakabali wetu – tuungane kwa uendelevu wa Bonde la Ziwa Victoria.”