03/06/2026
MANISPAA YA SINGIDA YAPOKEA SH MILIONI 544 KUJENGA SHULE MPYA
Serikali imeendelea kuimarisha sekta ya elimu katika Manispaa ya Singida baada ya kutoa Sh milioni 544 kwa ajili ya ujenzi wa shule mpya ya sekondari katika eneo la Manguanjuki, Kata ya Mandewa.
Fedha hizo zimepokelewa katika kipindi hiki ambacho mwaka wa fedha 2025/26 unakaribia kukamilika, ikiwa ni sehemu ya jitihada za Serikali ya Awamu ya Sita za kuboresha mazingira ya kujifunzia na kuhakikisha wanafunzi wanapata elimu karibu na maeneo wanayoishi bila kulazimika kutembea umbali mrefu.
Akizungumza kuhusu utekelezaji wa miradi ya maendeleo katika Divisheni ya Elimu Sekondari kwa mwaka wa fedha 2025/26, Afisa Elimu Sekondari wa Manispaa ya Singida, Athumani Mnyusi, alisema serikali ilitoa Sh milioni 185 kwa ajili ya kukamilisha miradi mbalimbali ya miundombinu ya elimu.
Alitaja miradi hiyo kuwa ni ukamilishaji wa madarasa mawili katika Shule ya Sekondari Mandewa kwa gharama ya Sh milioni 25, ukamilishaji wa maabara mbili katika Shule ya Sekondari Mughanga kwa Sh milioni 60, maabara mbili katika Shule ya Sekondari Unyianga kwa Sh milioni 60, pamoja na mabweni katika Shule ya Sekondari Mungumaji kwa Sh milioni 40.
Aidha, wadau wa elimu wa CAMFED walitoa Sh milioni 44 zilizotumika kujenga matundu 20 ya vyoo vya wasichana, ambapo matundu 10 yalijengwa katika Shule ya Sekondari Mitunduruni kwa Sh milioni 22 na matundu mengine 10 katika Shule ya Sekondari Senge kwa Sh milioni 22.
Kwa upande mwingine, Serikali Kuu ilitoa Sh milioni 20.4 kwa ajili ya ujenzi wa matundu ya vyoo katika shule za Mtamaa, Mwenge, Uhamaka, Mitunduruni, Maharu na Unyambwa.
Mnyusi aliwataka wazazi na walezi kuendelea kushiriki katika utoaji wa chakula shuleni ili kuwasaidia wanafunzi kusoma katika mazingira bora na kuongeza ufaulu wao wa kitaaluma.
Alisema uwekezaji unaoendelea kufanywa na serikali katika miundombinu ya elimu ni ushahidi wa dhamira yake ya kuhakikisha wanafunzi wanapata elimu bora kupitia mazingira rafiki ya kujifunzia na kufundishia.