04/09/2026
SUMBAWANGA YAJIPANGA KUKABILIANA NA ATHARI ZA MVUA NA EL NIÑO.
Katika kuhakikisha jamii na taasisi mbalimbali zinakuwa tayari kukabiliana na athari zinazoweza kujitokeza kutokana na mvua zinazozidi wastani pamoja na tishio la El Niño, Kamati ya Usimamizi wa Maafa Wilaya ya Sumbawanga imefanya kikao cha kujadili na kuweka mikakati ya maandalizi kabla na wakati wa msimu wa mvua.
Kikao hicho kilichofanyika Septemba 3, 2026, katika Ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Sumbawanga, kimeongozwa na Mkuu wa Wilaya ya Sumbawanga na Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe. Nyakia Ally Chirukile.
Akizungumza katika kikao hicho, Mhe. Chirukile amezitaka mamlaka husika kuchukua hatua za mapema na kuweka mikakati madhubuti ya kukabiliana na hatari zinazoweza kujitokeza, ili kupunguza madhara na maafa yanayoweza kusababishwa na mvua zinazozidi wastani pamoja na El Niño.
Aidha, Mhe. Chirukile amesisitiza umuhimu wa mamlaka husika kuwafikia wafugaji na kutoa elimu kuhusu namna bora ya kudhibiti na kuhifadhi mifugo yao wakati wa maafa, pamoja na kufanya utambuzi na kubaini idadi ya mifugo iliyopo katika vijiji, hatua itakayosaidia kurahisisha uokoaji na utoaji wa msaada endapo maafa yatatokea.
Kwa upande wake, Katibu Tawala wa Wilaya ya Sumbawanga, Bw. Gabriel Masinga, amezitaka mamlaka husika kuendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu namna bora ya kujikinga, kuchukua tahadhari na kuepuka maeneo hatarishi, ili kupunguza madhara yanayoweza kujitokeza wakati wa maafa.
Ameongeza kuwa, maandalizi ya mapema na ushirikiano kati ya Serikali, taasisi mbalimbali na wananchi ni muhimu katika kuhakikisha Wilaya ya Sumbawanga inakuwa tayari kukabiliana na athari za mvua na majanga mengine yanayoweza kujitokeza.