13/08/2026
Wizara ya Uchumi wa Buluu na Uvuvi Zanzibar na Wizara ya Mifugo na Uvuvi ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imefanya Kongamano la Uchumi wa Buluu katika Tamasha la Kizimkazi likiwa na kaulimbiu ya Hifadhi Bahari, Changamkia Fursa za Uchumi wa Buluu lililofanyika katika Hoteli ya Kwanza Kizimkazi.
Kongamano hilo limefunguliwa na Naibu Waziri wa Wizara ya Uchumi wa Buluu na Uvuvi Zanzibar Mheshimiwa Mboja Ramadhan Mshenga ambaye ameelezea umuhimu wa uhifadhi wa bahari, maziwa na mito ili yawe na matumizi endelevu kwa maslahi ya wananchi na taifa kwa ujumla.
Naibu Waziri amesisitiza kuwa kuna fursa nyingi za kiuchumi katika sekta hiyo ya maji ikiwemo kuongeza uwekezaji wa ndani, kikanda na kimataifa, kuzigeuza changamoto kuwa fursa za kiuchumi na kukuza na kuimarisha utamaduni wa Watanzania na kupambana na kupiga vita uvuvi haramu ambao unarudisha nyuma malengo katika sekta hiyo.
Akifunga Kongamano hilo Naibu Waziri wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi ya Serikali ya Jamhuri ya Tanzania Mheshimiwa Ng’wasi Damas Kamani amehimiza ushirikiano wa Taasisi, nchi, kikanda na kimataifa wa uhifadhi na ulinzi wa bahari, kupambana na uvuvi haramu, mabadiliko ya tabianchi na uchafuzi wa mazingira wa taka hasa za plastiki ili kuyafanya maji barani Afrika kuwa salama na yenye tija.
Pamoja na uhifadhi wa bahari aidha amehimiza kutumia teknolojia, kufanya utafiti na ubunifu katika kuongeza mchango wa sekta ya uvuvi kupitia uzalishaji wenye tija, kuongeza thamani na kuimarisha ushindani wa mazao nchini.
Kongamano hilo pia lilijumuisha utiaji Saini wa hati ya makuballiano baina ya Kampuni ya Mwani Zanzibar ZASCO na Mamlaka ya Udhibit wa Mbolea Tanzania TFRA, yakiwa na lengo la kuwezesha uzalishaji na udhibiti wa mbolea ya kimiminika inayotokana na mwani.