04/06/2026
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imewataka wananchi kushiriki kikamilifu katika juhudi za kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi ili kulinda mazingira na kuhakikisha maendeleo endelevu kwa vizazi vya sasa na vijavyo.
Wito huo umetolewa na, KAIMU Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais,Mhe. Hamza Hassan Juma, katika taarifa maalumu ya kuadhimisha Siku ya Mazingira Duniani mwaka 2026 aliyoitoa Ofisini kwake Migombani _ Zanzibar.
Amesema mabadiliko ya tabianchi yameendelea kuathiri Zanzibar kupitia kuongezeka kwa joto, kupungua kwa mvua za msimu, mafuriko na mmomonyoko wa fukwe kutokana na kuongezeka kwa kina cha bahari.
Mhe. Hamza ameeleza kuwa Serikali imeendelea kuchukua hatua mbalimbali za kukabiliana na changamoto hiyo ikiwemo kutekeleza sera, sheria na mikakati ya mazingira, kuimarisha elimu ya mazingira, kujenga uwezo wa jamii na taasisi pamoja na kuendeleza shughuli mbadala za kiuchumi zinazolinda mazingira.
Aidha, amesema Serikali imetenga shilingi bilioni 5 kwa mwaka wa fedha 2026/2027 kwa ajili ya shughuli za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi, ikilinganishwa na shilingi bilioni 4.5 zilizotengwa mwaka 2025/2026.
Amesema maadhimisho ya mwaka huu yanafanyika chini ya kaulimbiu ya Zanzibar isemayo, “Jamii inaanza na wewe; chukua hatua kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi kwa kulinda Zanzibar yetu,” ikiwa ni sehemu ya kuunga mkono kaulimbiu ya kimataifa ya “Climate Action.”
Katika wiki ya maadhimisho, Mhe. Hamza amesema shughuli mbalimbali zimefanyika Unguja na Pemba zikiwemo usafi wa mazingira, upandaji wa miti na mikoko, mafunzo kwa viongozi wa ngazi za jamii pamoja na kampeni za uhamasishaji kupitia vyombo vya habari na mitandao ya kijamii.
Hatahivyo Mhe. Hamza amewataka wananchi kuendelea kuchukua hatua za kuhifadhi mazingira na kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi kwa maslahi ya taifa na vizazi vijavyo.
Kilele cha Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani kwa Zanzibar kinatarajiwa kufanyika Juni 6, 2026 katika eneo la Kiwani, Wilaya ya Mkoani, Mkoa wa Kusini Pemba, ambapo Makamu wa Pili wa Rais, Mheshimiwa Hemed Suleiman Abdulla, anatarajiwa kuwa mgeni rasmi.