31/05/2026
Mkurugenzi Mkuu wa Wizara ya Afya Zanzibar, Dkt. Amour Suleiman Mohamed, amewataka wataalamu waliohitimu mafunzo ya usimamizi wa ubora wa huduma za afya kutumia elimu waliyoipata kuimarisha huduma kwa wananchi na kupunguza malalamiko yanayotolewa katika vituo vya afya.
Dkt. Amour alitoa wito huo kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya Zanzibar wakati wa hafla ya utoaji wa vyeti kwa wahitimu 19 wa mafunzo hayo, iliyofanyika katika ukumbi wa Golden Tulip Zanzibar Airport.
Akizungumza katika hafla hiyo, alisema ubora wa huduma za afya ni jukumu la kila mfanyakazi wa afya, kuanzia mlinzi, wahudumu wa afya hadi viongozi wa hospitali na taasisi mbalimbali za afya.
Alisema wahitimu hao wanapaswa kutumia maarifa na ujuzi walioupata kuwa sehemu ya mabadiliko chanya yatakayosaidia kuimarisha utoaji wa huduma za afya na kuongeza imani ya wananchi kwa taasisi za afya.
Dkt. Amour alisema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar chini ya uongozi wa Dkt. Hussein Ali Mwinyi imeendelea kuipa kipaumbele sekta ya afya kwa kuongeza bajeti, kuimarisha miundombinu ya huduma za afya pamoja na kuboresha mazingira ya kazi kwa wataalamu wa afya ili waweze kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi zaidi.
Kwa upande wake, Meneja wa Mradi kutoka PharmAccess, Dkt. Faiza Abasi, alisema mafunzo hayo yataongeza uwezo wa wataalamu wa afya katika kusimamia ubora wa huduma na kuimarisha ufanisi wa utoaji wa huduma kwa wananchi.
Naye Afisa wa Kitengo cha Ubora katika Wizara ya Afya Zanzibar, Hasfa M. Haji, alisema zaidi ya vituo 300 vya afya tayari vimefanyiwa tathmini ya ubora, huku wahitimu hao wakitarajiwa kuwa sehemu muhimu ya kusimamia viwango vya ubora katika vituo hivyo.
Awali, Mkurugenzi wa Idara ya Uuguzi na Ukunga, Mwanaisha Juma Fakih, alisema kuongezeka kwa wataalamu wa tathmini ya ubora kutasaidia kuimarisha huduma za afya na kupunguza malalamiko ya wananchi kuhusu huduma zinazotolewa katika hospitali na vituo vya afya Zanzibar.
Kwa upande wao, wahitimu wa mafunzo hayo waliahidi kutumia elimu na ujuzi walioupata kuimarisha utoaji wa huduma za afya katika hospitali na vituo vya afya wanavyofanyia kazi na kuishukuru Wizara ya Afya na PharmAccess kwa kuendelea kuwawezesha.