Wizara ya Afya Zanzibar

Wizara ya Afya Zanzibar Ukurasa rasmi wa Wizara ya Afya Zanzibar.
6 Barabara ya Health Office
Mnazi Mmoja S.L.P 236
70467 Mjini Magharibi, Zanzibar. Email: [email protected]

Mkurugenzi Mkuu wa Wizara ya Afya Zanzibar, Dkt. Amour Suleiman Mohamed, amewataka wataalamu waliohitimu mafunzo ya usim...
31/05/2026

Mkurugenzi Mkuu wa Wizara ya Afya Zanzibar, Dkt. Amour Suleiman Mohamed, amewataka wataalamu waliohitimu mafunzo ya usimamizi wa ubora wa huduma za afya kutumia elimu waliyoipata kuimarisha huduma kwa wananchi na kupunguza malalamiko yanayotolewa katika vituo vya afya.

Dkt. Amour alitoa wito huo kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya Zanzibar wakati wa hafla ya utoaji wa vyeti kwa wahitimu 19 wa mafunzo hayo, iliyofanyika katika ukumbi wa Golden Tulip Zanzibar Airport.

Akizungumza katika hafla hiyo, alisema ubora wa huduma za afya ni jukumu la kila mfanyakazi wa afya, kuanzia mlinzi, wahudumu wa afya hadi viongozi wa hospitali na taasisi mbalimbali za afya.

Alisema wahitimu hao wanapaswa kutumia maarifa na ujuzi walioupata kuwa sehemu ya mabadiliko chanya yatakayosaidia kuimarisha utoaji wa huduma za afya na kuongeza imani ya wananchi kwa taasisi za afya.

Dkt. Amour alisema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar chini ya uongozi wa Dkt. Hussein Ali Mwinyi imeendelea kuipa kipaumbele sekta ya afya kwa kuongeza bajeti, kuimarisha miundombinu ya huduma za afya pamoja na kuboresha mazingira ya kazi kwa wataalamu wa afya ili waweze kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi zaidi.

Kwa upande wake, Meneja wa Mradi kutoka PharmAccess, Dkt. Faiza Abasi, alisema mafunzo hayo yataongeza uwezo wa wataalamu wa afya katika kusimamia ubora wa huduma na kuimarisha ufanisi wa utoaji wa huduma kwa wananchi.

Naye Afisa wa Kitengo cha Ubora katika Wizara ya Afya Zanzibar, Hasfa M. Haji, alisema zaidi ya vituo 300 vya afya tayari vimefanyiwa tathmini ya ubora, huku wahitimu hao wakitarajiwa kuwa sehemu muhimu ya kusimamia viwango vya ubora katika vituo hivyo.

Awali, Mkurugenzi wa Idara ya Uuguzi na Ukunga, Mwanaisha Juma Fakih, alisema kuongezeka kwa wataalamu wa tathmini ya ubora kutasaidia kuimarisha huduma za afya na kupunguza malalamiko ya wananchi kuhusu huduma zinazotolewa katika hospitali na vituo vya afya Zanzibar.

Kwa upande wao, wahitimu wa mafunzo hayo waliahidi kutumia elimu na ujuzi walioupata kuimarisha utoaji wa huduma za afya katika hospitali na vituo vya afya wanavyofanyia kazi na kuishukuru Wizara ya Afya na PharmAccess kwa kuendelea kuwawezesha.

Wizara ya Afya Zanzibar imesema inaendelea kuweka tahadhari na kuimarisha ufuatiliaji wa afya katika mipaka, viwanja vya...
28/05/2026

Wizara ya Afya Zanzibar imesema inaendelea kuweka tahadhari na kuimarisha ufuatiliaji wa afya katika mipaka, viwanja vya ndege na bandarini ili kuhakikisha Zanzibar inaendelea kubaki salama dhidi ya ugonjwa wa Ebola unaoendelea kuripotiwa katika baadhi ya nchi za Afrika.

Mkurugenzi wa Kinga na Elimu ya Afya Dk. Slim Salim Slim, alisema hatua hizo zimechukuliwa kufuatia kuongezeka kwa visa vya ugonjwa huo katika nchi jirani ikiwemo Uganda na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC).

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo ya siku tatu kwa waandishi wa habari katika ukumbi wa Skuli ya Tumekuja, Dk. Slim alisema hadi sasa Zanzibar haijaripoti kesi yoyote ya Ebola, lakini Serikali imeendelea kuwa makini ili kuzuia uwezekano wa ugonjwa huo kuingia nchini.

Aidha, alisema Serikali inaendelea kushirikiana na taasisi mbalimbali za afya ikiwemo Afrika CDC pamoja na nchi jirani ili kubadilishana taarifa na kuweka mikakati ya pamoja ya kudhibiti ugonjwa huo.

Dk. Slim alisema Serikali ya Mapinduzi Zanzibar inaendelea kuonesha umuhimu mkubwa wa chanjo kwa kutumia zaidi ya Sh bilioni 1.6 kila mwaka kuhakikisha chanjo muhimu zinapatikana kwa watoto pamoja na wasichana visiwani humo.

Alisema kupitia fedha hizo, watoto wanaendelea kupatiwa chanjo mbalimbali dhidi ya magonjwa hatari huku wasichana wakipata chanjo ya HPV inayosaidia kuwakinga dhidi ya saratani ya mlango wa kizazi.

Aliwahimiza wazazi na walezi kuhakikisha watoto wanapatiwa chanjo zote kwa wakati ili kuwajengea kinga madhubuti dhidi ya magonjwa mbalimbali yanayoweza kuhatarisha maisha yao.

Pia aliwataka wananchi kuendelea kujitokeza kupata chanjo ya Uviko-19 akieleza kuwa chanjo hiyo imechangia kwa kiasi kikubwa kupunguza makali ya ugonjwa huo na kusaidia mwili kuwa na uwezo wa kupambana na virusi vya corona.

Alieleza kuwa Serikali itaendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu umuhimu wa chanjo pamoja na hatua mbalimbali za kujikinga dhidi ya magonjwa ya mlipuko ili kuhakikisha jamii inaendelea kuwa salama na yenye afya njema.

26/05/2026
EID MUBARAQ
26/05/2026

EID MUBARAQ

EID ni Furaha, Eid ni Upendo. Tusherehekee kwa Amani na Upendo huku tukikumbuka kulinda Afya zetu na za Wale wanaotuzung...
26/05/2026

EID ni Furaha, Eid ni Upendo. Tusherehekee kwa Amani na Upendo huku tukikumbuka kulinda Afya zetu na za Wale wanaotuzunguka.

❤️ 🌙🕌♥️

Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya Zanzibar, Dkt Mngereza Mzee Miraji amesema Serikali ya Mapinduzi Zanzibar imejipanga kuima...
22/05/2026

Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya Zanzibar, Dkt Mngereza Mzee Miraji amesema Serikali ya Mapinduzi Zanzibar imejipanga kuimarisha huduma za afya ngazi ya jamii kupitia Wahudumu wa Afya ya Jamii (CHWs), huku akiwataka wahudumu hao kufanya kazi kwa uadilifu, bidii na kujituma kwa ajili ya kuokoa maisha ya wananchi.

Akizungumza katika hafla ya kusaini mikataba na kugawa vifaa kazi kwa wahudumu wa afya waliohitimu mafunzo yao, iliyofanyika SUZA Tunguu, Mkoa wa Kusini Unguja, Dkt Miraji alisema wahudumu hao ni sehemu muhimu katika mapambano dhidi ya changamoto za afya zinazowakabili wananchi, hususan wanawake wajawazito na watoto wachanga.

Alisema Serikali ina matumaini makubwa kuwa kupitia wahudumu hao kutakuwa na maboresho makubwa katika utoaji wa huduma za afya ndani ya jamii pamoja na kuongezeka kwa elimu ya afya kwa wananchi.

Dkt Mngereza alifahamisha kuwa jumla ya wahudumu 753 kutoka shehia mbalimbali za Unguja wamehitimu mafunzo katika awamu ya pili ya programu hiyo, huku wahudumu 1,054 wakipatiwa mafunzo Zanzibar nzima, ambapo 301 wanatoka Pemba.

Alieleza kuwa mbali na huduma za afya ya msingi, wahudumu hao wamejengewa uwezo wa matumizi ya mifumo ya kidigitali ikiwemo mfumo wa “Jamii ni Afya”, mfumo wa kadi za matibabu na mfumo wa ZaneMR, hatua itakayosaidia kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma na ukusanyaji wa taarifa za afya.

Kwa upande wake, Mkuu wa Kitengo cha Uratibu wa Wahudumu wa Afya Ngazi ya Jamii Zanzibar, Halima Ali Khamis alisema wahudumu hao wameandaliwa kuwa daraja muhimu kati ya jamii na sekta ya afya, huku mafunzo yao yakifanyika kwa muda wa miezi sita.

Alisema dhamira ya Serikali ni kuhakikisha kila mwananchi anapata huduma za msingi za afya kwa ukaribu zaidi kupitia wahudumu waliopata mafunzo maalum ya kuwahudumia wananchi katika maeneo yao.

Naye mwakilishi kutoka Shirika la De Tree Hannah Mikidadi kwa niaba ya Willow alisema taasisi hiyo itaendelea kushirikiana na Serikali ya Zanzibar katika kuimarisha huduma za afya ya jamii kupitia matumizi ya teknolojia za kidijitali.

Kwa upande wao, wahitimu wa mafunzo hayo walisema wamepata ujuzi na uwezo mkubwa wa kuwahudumia wananchi kwa weledi na kutumia mifumo ya kidijitali kutoa huduma.

Wizara ya Afya Zanzibar imesema itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali wa afya wakiwemo CIHEB Tanzania na Shirika l...
22/05/2026

Wizara ya Afya Zanzibar imesema itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali wa afya wakiwemo CIHEB Tanzania na Shirika la Afya Duniani katika kuhakikisha huduma za afya zinaendelea kutolewa kwa kuzingatia miongozo ya usalama wa afya iliyopo nchini pamoja na ile ya kimataifa.

Akifunga mafunzo ya kuandaa mwongozo maalumu wa kuzuia na kudhibiti maambukizi kupitia Mradi wa Usalama wa Afya Duniani (IPC), Mkurugenzi wa Kinga na Elimu ya Afya Zanzibar, Dkt. Salim Slim amesema mafunzo hayo yamekuwa na mchango mkubwa katika kuimarisha uwezo wa watendaji wa afya juu ya udhibiti wa maambukizi katika hospitali za Wilaya na Mkoa.

Amesema uwepo wa mwongozo huo ni sehemu ya juhudi za Serikali ya Mapinduzi Zanzibar za kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora, salama na zenye kuzingatia viwango vya afya vilivyowekwa na taifa pamoja na Shirika la Afya Duniani.

Dkt. Slim amesema Serikali kupitia Wizara ya Afya imeendelea kuimarisha mifumo ya kinga dhidi ya magonjwa ya kuambukiza pamoja na kutoa elimu kwa wahudumu wa afya na jamii ili kuhakikisha wananchi wanakuwa salama dhidi ya majanga mbalimbali ya kiafya yanayoweza kujitokeza wakati wowote.

Aidha ameishukuru CIHEB Tanzania kwa ushirikiano wao katika kufanya tathmini kwenye hospitali za Zanzibar pamoja na kuandaa mwongozo huo ambao unatarajiwa kusaidia kubadili baadhi ya tabia za watendaji wa afya hususan katika kuzingatia usafi na kanuni za kujikinga dhidi ya maambukizi.

Kwa upande wake Mwakilishi kutoka n Shirika la Afya ulimwenguni WHO Janeth S. Masuma amezipongeza juhudi za Wizara ya Afya Zanzibar pamoja na wadau wa afya kwa kufanikisha mafunzo hayo, yakielezwa kuwa hatua muhimu katika kuimarisha kinga dhidi ya maambukizi.

Amesema WHO itaendelea kuunga mkono jitihada za Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kupitia Wizara ya Afya kwa kuwajengea uwezo wafanyakazi wa afya, kuimarisha mifumo ya huduma za afya pamoja na kushirikiana na taasisi mbalimbali katika kuhakikisha usalama wa afya kwa wananchi wote.

SERIKALI ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia Wizara ya Afya inaendelea kuimarisha huduma za afya ya mama na mtoto pamoja na...
22/05/2026

SERIKALI ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia Wizara ya Afya inaendelea kuimarisha huduma za afya ya mama na mtoto pamoja na huduma za chanjo katika hospitali na vituo vya afya Unguja na Pemba, hatua ambayo imechangia kupungua kwa vifo vya akina mama na watoto wachanga pamoja na kuongezeka kwa huduma za kinga dhidi ya magonjwa mbalimbali ya watoto.

Hayo yameelezwa na Kaimu Waziri wa Afya Zanzibar Dkt Saada Mkuya Salum katika hotuba ya  bajeti ya Wizara ya Afya kwa mwaka wa fedha 2026/2027, ambapo Serikali imeendelea kuwekeza kwa kiwango kikubwa katika sekta ya afya ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora na salama.

Amefahamisha kuwa kwa mujibu wa taarifa hiyo, jumla ya wajawazito 56,774 walihudhuria kliniki katika vituo vya afya na hospitali mbalimbali Zanzibar kwa kipindi cha Julai 2025 hadi Machi 2026. Aidha, wajawazito 42,697 walijifungua katika hospitali na vituo vya afya chini ya usimamizi wa wataalamu wa afya.

Kati ya wajawazito hao 36,369 walijifungua kwa njia ya kawaida na 6,328 walijifungua kwa njia ya upasuaji huku Wajawazito 1,779 walijifungua nyumbani.

Katika hatua nyingine, Serikali imefanikiwa kupunguza vifo vya akina mama vinavyotokana na uzazi kutoka vifo 145 kwa kila vizazi hai 100,000 mwaka 2023 hadi kufikia vifo 121 mwaka 2025.

Aidha, vifo vya watoto wachanga ndani ya mwezi mmoja baada ya kuzaliwa vimepungua kutoka watoto 13.2 kwa kila vizazi hai 1,000 mwaka 2023 hadi watoto 11 mwaka 2025.

Serikali pia imeendelea kuimarisha mfumo wa rufaa wa “M-Mama” kwa ajili ya wajawazito na watoto wachanga ambapo kina mama 959 pamoja na watoto wachanga 128 walipatiwa huduma za rufaa za dharura kwa kipindi hicho.

Kwa upande wa chanjo, Serikali imeendelea kuhakikisha watoto wanapatiwa chanjo muhimu za kuwakinga dhidi ya magonjwa hatari ambapo watoto 74,416 walipatiwa chanjo ya BCG, watoto 51,253 walipata dozi ya tatu ya chanjo ya Polio (OPV3), watoto 50,993 walipatiwa dozi ya tatu ya chanjo ya PENTA, Watoto 57,298 walipatiwa chanjo ya Surua (MR2).

Aidha, wasichana 17,610 walipatiwa chanjo ya HPV2 ya kukinga saratani ya shingo ya kizazi, ikilinganishwa na wasichana 10,696 waliopatiwa chanjo hiyo mwaka uliopita.

TRAVEL ADVISORY NO.1 📢
21/05/2026

TRAVEL ADVISORY NO.1 📢

Muendelezo wa kikao kazi cha uandaaji wa mwongozo maalumu wa IPC kupitia Mradi wa Usalama wa Afya Duniani umeendelea kwa...
21/05/2026

Muendelezo wa kikao kazi cha uandaaji wa mwongozo maalumu wa IPC kupitia Mradi wa Usalama wa Afya Duniani umeendelea kwa lengo la kuandaa nyenzo itakayosaidia kuboresha utekelezaji wa huduma za afya katika hospitali mbalimbali nchini.

Mwongozo huo unatarajiwa kuwa chachu ya kuongeza uelewa kwa watendaji wa sekta ya afya kuhusu umuhimu wa kuzingatia kanuni na taratibu za kinga na udhibiti wa maambukizi (IPC) wanapotekeleza majukumu yao ya kila siku.

Kupitia mwongozo huo, watendaji wa hospitali watawezeshwa kuhakikisha usalama wao binafsi pamoja na usalama wa wagonjwa wanaowahudumia, jambo litakalosaidia kupunguza maambukizi ya magonjwa ndani ya vituo vya kutolea huduma za afya.

Aidha, hatua hiyo itachangia kuimarisha ubora wa huduma za afya kwa wananchi na kuongeza mazingira salama kwa wagonjwa na wahudumu wa afya hapa nchini

Address

Mnazi Mmoja Zanzibar
Zanzibar City

Opening Hours

Monday 07:30 - 15:30
Tuesday 07:30 - 15:30
Wednesday 07:30 - 15:30
Thursday 07:30 - 15:30
Friday 07:30 - 15:30

Telephone

+255242231614

Alerts

Be the first to know and let us send you an email when Wizara ya Afya Zanzibar posts news and promotions. Your email address will not be used for any other purpose, and you can unsubscribe at any time.

Contact The Organization

Send a message to Wizara ya Afya Zanzibar:

Share