02/06/2026
Katibu Mkuu Wizara ya Utalii na Mambo ya Kale Zanzibar Dkt. Aboud Suleiman Jumbe amefanya Mkutano na Vyombo vya habari kueleza kuhusiana na Tamasha la Muziki la Italia na Zanzibar, linalotarajiwa kufanyika chini ya Ufadhili wa Ubalozi wa Italia hapa Tanzania kwa kushirikiana na Wizara ya Utalii na Mambo ya Kale, Wizara ya Habari, Utamaduni Sanaa na Michezo, na Chuo cha Muziki wa Nchi za Majahazi (Dhow Countries Music Academy).
Ameeleza hayo leo wakati akizungumza na Waandishi wa Habari Ofisini kwake katika Ukumbi wa Wizara iliyopo Kikwajuni - Unguja.
Dkt. Aboud amesema kwamba Ubalozi wa Italia nchini Tanzania, na Wizara ya Utalii na Mambo ya Kale, Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, kwa pamoja Inawakaribisha Wadau wote katika Tamasha Maalum la Muziki Asilia wa Italia litakalofanyika Zanzibar, na kujumuisha Kikundi cha Muziki Asilia cha Italia kiitwacho Officina Zoe, kikundi cha Dhow Countries Music Academy kutoka Zanzibar .
Dkt. Aboud amefafanua kua Tamasha hili litakuwa ni la siku mbili litaanza tarehe 5 Juni 2026 ambapo Wanasanaa watakuwa katika Eneo la Shambaland Park, Pwani Mchangani na Siku ya Pili, tarehe 6 Juni 2026, Saa Kumi na Moja Jioni, ambapo Wasanii hao watakuwa katika Bustani za Forodhani, Mji Mkongwe.
Aidha Dkt . Aboud amefahamisha kuwa Ziara ya kundi hili nchini Tanzania inafanyika katika maadhimisho ya miaka 80 ya Jamhuri ya Italia, ambayo huadhimishwa kila ifikapo tarehe 2 Juni na Mwaka huu inaadhimishwa Miaka 65 ya Uhusiano wa kidiplomasia kati ya Tanzania na Italia.
Sambamba na hayo Dkt. Aboud alipata fursa ya kuwashukuru kwa dhati kabisa Viongozi wa kitaifa, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mheshimiwa Dkt Hussein Ali Mwinyi, kwa kuendelea kuiongoza vyema nchi ya Tanzania --- na hasa katika kuitangaza Zanzibar na Tanzania katika medani za Utalii.