19/08/2026
Katibu Mtendaji wa Tume ya Mipango Zanzibar, Dkt. Josephine Rugate Kimaro, ameongoza kikao kazi kilichowakutanisha viongozi wakuu wa Tume ya Mipango Zanzibar na ujumbe wa kidiplomasia kutoka Uingereza, kwa lengo la kutathmini mafanikio yaliyopatikana katika utekelezaji wa Mpango wa Maendeleo wa Zanzibar Awamu ya Kwanza (ZADEP I) na kuweka misingi ya utekelezaji wa awamu ya pili ya mpango huo, ZADEP II.
Kikao hicho kilichofanyika leo katika Ukumbi wa Wizara ya Fedha na Mipango, kimejadili maeneo mbalimbali ya ushirikiano wa maendeleo kati ya Zanzibar na Uingereza.
Akizungumza katika kikao hicho, Dkt. Kimaro amesema ushirikiano huo umejikita katika sekta mbalimbali, zikiwemo miundombinu, utalii, uimarishaji wa taasisi za Serikali, usalama na utawala bora.
Amesema Uingereza imeendelea kuwa mshirika muhimu katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo Zanzibar, ikiwemo miradi ya ujenzi na uimarishaji wa miundombinu mbalimbali.
Aidha, amesema ushirikiano huo unalenga kuimarisha utoaji wa huduma za kijamii, kuongeza fursa za ajira na kupanua wigo wa shughuli za kiuchumi, hatua ambazo zinatarajiwa kuongeza mapato ya wananchi pamoja na Serikali.
Kwa upande wake, Kamishna wa Idara ya Mipango ya Kitaifa na Maendeleo ya Kisekta kutoka Tume ya Mipango Zanzibar, Mohamed Masoud Salim, amesema barabara zinazojengwa katika maeneo ya Fumba na Kizimkazi ni za kimkakati
Kamishna Salim amefahamisha kuwa Serikali tayari imeweka mikakati thabiti ya kuimarisha ulinzi na usalama, huduma za dharura za afya, pamoja na upanuzi wa miundombinu ya usafiri.
Aidha, amesema mipango hiyo inajumuisha upanuzi wa uwanja wa ndege ili kufikia uwezo wa kuhudumia wageni milioni 1.1, sambamba na kuanzishwa kwa mfumo wa usafiri wa umma unaotumia mabasi ya umeme.
Hatua hizo ni sehemu ya juhudi za Serikali za kuimarisha miundombinu, kukuza shughuli za kiuchumi na kijamii, pamoja na kuweka mazingira wezeshi ya kufikiwa kwa malengo ya maendeleo ya Zanzibar.