04/05/2026
WATENDAJI WA ZIPA WAPATIWA MAFUNZO MAALUM KUHUSU UTAFUTAJI NA USIMAMIZI WA FEDHA ZA MIRADI YA NISHATI
Watendaji wa Mamlaka ya Kukuza Uwekezaji Zanzibar (ZIPA) wamepatiwa mafunzo maalum yenye lengo la kuwajengea uwezo katika kutafuta, kufuatilia na kuandaa miradi ya maendeleo hususani katika sekta ya nishati.
Mafunzo hayo yameandaliwa na ZIPA kwa kushirikiana na Shirika la umoja wa Mataifa (UN) Idara ya Uchumi na Kijamii pamoja na Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Biashara na Maendeleo (UNCTAD).
Akifungua Mafunzo hayo na Katibu Mkuu Wizara ya Kazi na Uwekezaji Nd. Khamis Suleiman Mwalimu kwa niaba ya Waziri wa Kazi na Uwekezaji Mhe. Shariff Ali Shariff amesema, mafunzo hayo yanakuja wakati muafaka ambapo Serikali ipo katika hatua za kuimarisha jitihada za kutafuta rasilimali fedha kwa ajili ya kugharamia miradi ya maendeleo.
Kwa upande wake, Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Dkt. Richard Muyungi, amesema, Serikali ina mkakati madhubuti wa kuhamasisha matumizi ya nishati jadidifu ili kupunguza athari za mabadiliko ya tabianchi na kuchochea maendeleo endelevu.
Amebainisha hali ya uzalishaji wa umeme nchini inaendelea kuimarika, huku akieleza kuwa matumizi ya gesi asilia yanaendelea kuwa sehemu muhimu ya mchanganyiko wa nishati.
Aidha, amewataka washiriki wa mafunzo hayo kutumia fursa hiyo kujifunza kwa kina na kujenga mashirikiano imara yatakayosaidia kuvutia rasilimali fedha na kuendeleza miradi yenye tija kwa Taifa.
Naye Mkurugenzi Mtendaji wa ZIPA, Saleh Saad Mohamed, Ameeleza kuwa, mafunzo hayo yatawasaidia Watendaji wa ZIPA yatawajengea Uwezo watendaji kuwa na uelewa mpana wa vyanzo vya fedha na mbinu za kuandaa miradi itakayovutia wawekezaji na wafadhili.
“Mafunzo haya ni jukwaa muhimu la kujifunza na kubadilishana uzoefu, lakini pia ni hatua ya kuwawezesha watendaji wetu kuwa wabunifu zaidi katika kuibua na kusimamia miradi ya kimkakati,” amesema.
Amebainisha kuwa, katika kipindi cha miaka mitano iliyopita, ZIPA imesajili zaidi ya miradi 630, ambayo utekelezaji wake unategemea kwa kiasi kikubwa upatikanaji wa nishati ya uhakika.
Development