12/08/2026
ZANZIBAR INVESTMENT BANK KUJA NA FURSA MPYA YA MITAJI KWA WAWEKEZAJI ZANZIBAR
Serikali ya Mapinduzi Zanzibar imeendelea kuchukua hatua za kuimarisha mazingira ya uwekezaji kwa kuandaa uanzishwaji wa Benki ya Uwekezaji Zanzibar (ZIB), taasisi inayolenga kuongeza upatikanaji wa mitaji kwa wawekezaji na kuchochea ukuaji wa uchumi wa Zanzibar.
Hayo yameelezwa na Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Kukuza Uwekezaji Zanzibar (ZIPA), Ndg. Saleh Saad Mohamed, wakati akifungua kikao kazi kilichowakutanisha wadau mbalimbali wa uwekezaji, kilichofanyika Maruhubi, Zanzibar.
Mkurugenzi Saleh amesema uanzishwaji wa benki hiyo utasaidia kwa kiasi kikubwa kuimarisha mazingira ya uwekezaji Zanzibar na kuwa kichocheo muhimu cha ukuaji wa uchumi.
“Lengo la benki hii ni kuhakikisha wawekezaji na miradi ya kimkakati wanapata mifumo na vyanzo vya fedha vinavyohitajika ili kukua na kufikia malengo yao,” amesema.
Kwa upande wao, ujumbe kutoka Wizara ya Fedha, pamoja na kampuni inayoshirikiana katika mchakato wa kuanzishwa kwa Benki ya Uwekezaji Zanzibar, umeeleza kuwa benki hiyo inatarajiwa kutoa fursa mbalimbali za ufadhili, ikiwemo ikiwemo ufadhili wa miradi, huduma za benki ya uwekezaji, uwekezaji wa mtaji wa hisa na uhamasishaji wa mitaji, ili kusaidia miradi yenye uwezo mkubwa kufikia hatua ya utekelezaji.
Wamesema sekta zinazoweza kunufaika na huduma hizo ni pamoja na miundombinu, uchumi wa buluu, viwanda, biashara ndogo na za kati (SMEs), utalii, nishati, pamoja na miradi mingine ya kimkakati inayokwenda sambamba na vipaumbele vya Serikali ya Zanzibar.
Aidha, wameeleza kuwa ZIB inatarajiwa kuunganisha na kuwezesha upatikanaji wa mitaji kutoka vyanzo mbalimbali, ikiwemo Serikali, taasisi za maendeleo, sekta binafsi, masoko ya mitaji, pamoja na wawekezaji wa ndani na wa kimataifa.
Hatua hiyo inalenga kuongeza uwezo wa Zanzibar katika kuvutia na kuelekeza mitaji mikubwa kwenye miradi yenye tija, kuchochea uwekezaji katika sekta muhimu za uchumi na hatimaye kuharakisha maendeleo endelevu ya Zanzibar.