10/11/2025
Mwenyekiti wa Taifa wa ACT-Wazalendo na Aliyekuwa Mgombea wa Nafasi ya Urais wa Zanzibar kupitia Chama hicho katika Uchaguzi Mkuu wa hivi karibuni, Mheshimiwa Othman Masoud Othman, leo Jumatatu Novemba 10 2025, amefanya mazungumzo na Viongozi wa Ngazi mbali mbali wa Mkoa wa Kichama wa Chake Chake Kisiwani Pemba, ili kujadili yaliyojiri Nchini, katika Zoezi hilo la Kitaifa.
Kikao hicho ambacho kimewajumuisha Viongozi wa Kamati za Uongozi wa Ngazi za Mkoa, Majimbo, Matawi, pamoja na waliokuwa Mawakala wao, kwa Mkoa huo wa Kichama, kilikuwa na Ajenda ya Kusikiliza Taarifa juu ya Matukio yaliyojitokeza katika Mchakato wote wa Uchaguzi, sambamba kupokea maagizo ya Chama, kimefanyika hapo Ukumbi wa Kwale, Jimbo la Ziwani.
Wakielezea baadhi ya changamoto walizokutana nazo katika Siku ya Uchaguzi ya Tarehe 29 Oktoba (na Tarehe 28 Siku ya Kura ya Mapema) Mawakala, Waangalizi, na
Viongozi wa Chama hicho wamesema, kilichojiri ni wizi, uporaji, uchafuzi na hujuma za wazi wazi, dhidi ya maamuzi, haki, ridhaa na sauti kubwa ya umma, ndani na nje ya masanduku ya kura.
Wakieleza hayo, kwa niaba ya Wahusika wengine na kwa nyakati tofauti, Bw. Khamis Mselem Ali wa Tibirinzi, Bw. Saleh Abdurahman wa Chonga, na Bw. Said Omar wa Ole, wameeleza kuwa watu wengi waliokuja kupiga kura siyo ambao walikuwemo ndani ya Daftari la Kudumu la Wapigakura wa Vituo-husika; bali ni mapandikizi na mamluki kutoka maeneo mengineyo, ambao hawakustahiki.
"Waliopiga-kura walipatiwa rundo la karatasi za kura kuanzia tano, kumi, ishirini, mia na zaidi; na pindipo tukihoji ama kuzuia ubadhirifu na uchafuzi huo, tulitishiwa-uhai wetu kwa mtutu wa bunduki, vipigo, tulikuwa tunatolewa nje ya Vituo kwa nguvu, huku Askari wakiangalia tu bila ya hatua yoyote", amesimulia Bw. Kassim Omar wa Michakaini ambaye alikuwa miongoni mwa Mawakala hao.
"Tulishuhudia wasimamizi wa Uchaguzi katika vituo wakizipiga wao kura na kuzijaza katika masanduku ya kura, lakini kubwa tulinyimwa hata fursa ya kuhesabu kura pamoja na kunyimwa fomu za matokeo na vituo vingi kura hazikuhesabiwa kabisa", amesimulia Bi Asha Mohamed, mkaazi wa Pondeani.
"Tulishuhudia Wasimamizi wa Kura wakitoroka na Fomu za Matokeo, na pia Masanduki ya Kura yakiwa wazi; tulipojaribu kuwafuata, walitutisha kwa bunduki, na wakatuambia ambaye anataka kifo ajaribu kufuatilia", ameeleza Bimkubwa Ali, mkaazi wa Chake Chake Mjini.
Miongoni mwa Mawakala hao, aliyejitambulisha kwa jina la Bakari Juma wa Vitongoji amesema, " tulichoshuhudia Mheshimiwa ni hujuma za kusikitisha kabisa; hawa Vikosi na Bunduki zao walitutisha ili tumuache Msimamizi ajaze Mamia ya Kura katika Sanduku; na hata Mgombea wa Jimbo langu alipokuja na yeye aliambiwa hana haki aondokea, au atakiona cha- moto".
"Tuliyoyashuhudia itafika kesho hatuyamalizi Mheshimiwa, maana ni wizi wa mchana-kweupe haijawahi kutokea; Magari ya Serikali tunayajua, yalikuja yamejaza watu wasiostahiki, walikuwa wakimimina kura watakavyo kuwatilia Wagombea wa CCM, hasa pale baada ya muda wa mwisho wa kupiga kura", ameeleza Bw. Said Rashid, mkaazi wa Ziwani.
Katika salamu na shukran zake mbele ya Viongozi hao, pia akizungumzia changamoto hizo, Mheshimiwa Othman amesema Lengo Kuu la Chama hicho siyo kupigania Nafasi za Kuongoza katika Serikali ya Umoja wa Kitaifa, bali ni kujenga mustakbali mwema wa Nchi, ambao ni wa kudumu, kwaajili ya Vizazi vya sasa na baadae.
Amesema, Mikakati ya Chama hicho na msimamo wa sasa wa Viongozi wake, ikitanguliwa na subra, ni katika njia inayopelekea kuiokoa Nchi ibaki na amani na Utulivu, licha ya dhulma kubwa iliyoshuhudiwa, ili khatimaye kuhakikisha Dhamira hiyo inafikiwa.
Amesema lengo siyo kuongoza Serikali ya Umoja wa Kitaifa, kwa mtindo ule wa 'kufunika kombe', bali ni kutafuta suluhisho la kudumu litakaloinyoonsha Nchi na kuielekeza katika khatma njema, na ikibidi hata kuepukana na Chaguzi zilizojaa vitisho, machafuko, umwagaji wa damu, wizi na hujuma za kila aina.
"Ndugu zangu nataka niwaambie kwamba hiki siyo Chama cha Uchaguzi, wala cha kutafuta nafasi katika Serikali ya Umoja wa Kitaifa, bali Dhamira yetu ni kuendeleza harakati za kupigania kujenga Mustakbali mwema wa Nchi utakaojali maslahi na heshima ya kila mtu, kwaajili ya maisha bora, sasa na hapo baadae", amesema.
Aidha, ameongeza kwa kusema, "Viongozi na Waasisi wa Nchi waliongoza wakaleta Mapinduzi, wakatunga Katiba na Miongozo mbali mbali ili kuleta muafaka, hadi kufikia kuwepo Serikali ya Umoja wa Kitaifa, baada ya kushuhudia na kisha kuchoshwa na mauwaji, mateso na madhila kwa wananchi; na khatimaye wakasema hayo hayana nafasi tena katika kuongoza Nchi ya Watu Wastaarabu, k**a Zanzibar na Tanzania kwa ujumla".
"Sasa iweje leo yatumike Mamilioni ya Fedha za Wananchi kuitisha Uchaguzi uliojaa vituko, hila, hujuma na wizi, almuradi ili mtu fulani awepo madarakani, hata iwapo Umma umemkataa; kwetu sisi hili halikubaliki katu", ameongeza Mheshimiwa Othman.
Akisisitiza Msimamo wake, Viongozi, na Chama chake kwa ujumla, baada ya kile alichotaja kuwa 'uhuni mkubwa wa Uchaguzi', nakwamba hawako-tayari kuingia Serikalini na kuongoza pamoja na Watu waliopora Haki, Demokrasia na Heshima ya Wananchi walio-wengi, Mheshimiwa Othman ameeleza kuwa kilichopita katika Matukio yote hayo ni 'Awamu ya Kwanza', na sasa kilichopo ni kuipigania Haki ya Umma Mkubwa walioshirikiana kumchagua na kumpigia-kura yeye na Wenzake.
"Lengo letu ilikuwa kuwafikia Wazanzibari wote, kuomba tuwe pamoja na tuungane katika kuyafikia Malengo ya Kuinusuru Zanzibar; na haya yote tumefanikiwa kuyafikia; kilichosalia naomba mtuamini ili tukamilishe hatua iliyobaki", ameeleza Mheshimiwa Othman.
Amekiambia Kikao hicho kwamba wao siyo Watu wa vurugu wala wa- purukushani, bali yeye, Wafuasi wa Chama chake, na Wazanzibari waungwana wote ni waumini wa amani na watetezi wa Nchi na Maendeleo endelevu yasiyokuwana vitisho.
Aidha amesema kutokana na Takwimu Sahihi ambazo Chama chake, pamoja na vyanzo vyao mbali mbali vya kuaminika, kabla Matokeo ya Kura hayajapinduliwa, walikwishajizolea Ushindi wa Nafasi ya Urais wa Zanzibar kwa zaidi ya Asilimia 70; na pia Majimbo 32 kwa Viti vya Ubunge na Uwakilishi, Unguja na Pemba.
Amefahamisha kuwa kutokana na uhakika na ushahidi juu ya ushindi huo, Chama chake pia kimechukua HATUA YA KUFUNGUA KESI MAHAKAMANI ili kudai MAJIMBO HAYO ambayo ACT-Wazalendo walishinda.
"Ndiyo maana hata Wazee wetu waliokuwa Watawala na Wakuu wa Nchi hii wameniita wakaniambia "WEWE PAMOJA NA WAFUASI WAKO WOTE HONGERENI SANA! MUAMINI KILICHOIBWA NI 'FURNITURE' TU, BALI NYUMBA IPO SALAMA NA HESHIMA IPO PALE PALE", amebainisha Mheshimiwa Othman.
Ameeleza kuwa yeye na Viongozi wenzake walikuwa-nazo taarifa kamili juu ya maandalizi na mipango ya hujma na machafuko, ikiwemo ya mauaji dhidi ya wananchi wasiokuwa na hatia, bali kwa Qadar Yake Mwenyezi Mungu, Dua nyingi na hekima kubwa, yalipelekea kuinusuru Nchi hii kutokana na majanga hayo.
"Kwahivyo sisi tunachotafuta ni jambo ambalo litakuwa na Maslahi ya Nchi kwa muda mrefu pamoja na Wananchi wake; na wala siyo Maslahi ya wachache, au Maslahi ya ACT- Wazalendo", amesisitiza Mheshimiwa Othman akiwakumbusha Wanachama na Wafuasi wake kwamba hiyo ndiyo imekuwa SILAHA MUHIMU YA USHINDI WAO.
Hivyo pia, katika mnasaba wa msimamo wa Chama hicho baada ya 'hujuma za Uchaguzi', Mheshimiwa Othman amehimiza umoja na mshik**ano, na pia kupokea TAARIFA RASMI KUTOKA KWA VIONGOZI, na wala siyo 'maburungutu' ya upotoshaji yenye dhamira mbaya ya kuwagawa na kuwavunja-moyo.
Kwa upande wake, Makamu Mwenyekiti wa ACT-Wazalendo upande wa Zanzibar, Ndugu Ismail Jussa amesema yaliyotokea na vitisho vinavyoendelea ni kielelezo kwamba Wazanzibari wamemkubali na kumsikiliza Mheshimiwa Othman na Chama chake.
"Kiongozi wetu alitutaka tuungane na tumeungana; ametutaka tudumushe amani na hali inaonekana; Nchi ipo salama, na sasa ametuambia anaendele kupigania haki yetu nasi sote tunasema tuko pamoja naye na tutaipata haki ya nchi yetu Inshaallah", ameeleza Jussa huku akisisitiza kwamba Mheshimiwa Othman ndiye Chaguo na Mkombozi wa Kweli wa Visiwa hivi.
Naye, Naibu Katibu Mkuu wa ACT-Wazalendo Zanzibar, Ndugu Omar Ali Shehe, pamoja na Mwenyekiti wa Mkoa wa Kichama wa Chake Chake, Ndugu Yussuf Salim Khamis, wamesema, Wanachama wa Mkoa huo, na Wazanzibari kwa ujumla, wapo tayari kuungana na Kiongozi wao huyo katika mapambano ya kuitafuta haki yao iliyoporwa.
"Mheshimiwa hili kwetu halijaisha, na tunakuhakikishia hatujachoka na tunaendelea kupambania haki yetu", ameeleza Nd. Omar.
Viongozi mbali mbali wameambatana na Mheshimiwa Othman katika Hafla hiyo, wakiwemo Wenyeviti, Makatibu wa Majimbo na Matawi, wakiongozwa na Mratibu wa Chama hicho Pemba, Ndugu Rashid Ali Abdallah.
Kitengo cha Habari,
Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar
Novemba 10, 2025.