Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais Zanzibar

Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais Zanzibar Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais Zanzibar,

Mwenyekiti wa Taifa wa ACT-Wazalendo,  Mheshimiwa Othman Masoud Othman, leo Jumanne Novemba 18 2025, amefanya Mazungumzo...
18/11/2025

Mwenyekiti wa Taifa wa ACT-Wazalendo, Mheshimiwa Othman Masoud Othman, leo Jumanne Novemba 18 2025, amefanya Mazungumzo na Viongozi wa Ngazi mbali mbali wa Mikoa ya Kichama ya Kaskazini A na B Unguja.

Mazungumzo hayo ambayo ni muendelezo wa Ziara zake Unguja na Pemba, yakilenga katika kuwashukuru Wananchi, kusikiliza Mtiririko wa Matukio ya uporaji wa Mchakato wote wa Uchaguzi Mkuu wa hivi karibuni Nchini, pamoja na kutoa msimamo na muelekeo wa Chama chake, yamefanyika kwa nyakati tofauti katika Ofisi za ACT-Wazalendo, za Shangani Mkokotoni na Kiomba-Mvua Bumbwini.

Akizungumza mbele ya Mamia ya Wanachama, Wapenzi, pamoja na Viongozi hao Mheshimiwa Othman, amesema Chama chake hakioni haja ya madaraka, wakati ambapo Umma na Ulimwengu wote ukishuhudia dhulma, wizi na uporaji wa Uchaguzi, hali ambayo inadhoofisha heshima na murua wa Nchi na Taifa kwa ujumla.

Amesema, haiwezekani katu kwa Viongozi kujiweka madarakani kupitia wizi wa kura, uporaji na udanganyifu dhidi ya maamuzi ya Wananchi walio-wengi, kisha Nchi au Jamii ikayafikia maendeleo ya kweli.

Amefahamisha kuwa kwa upande wake, Chama chake, pamoja na matarajio ya Umma wa Wananchi hapa Visiwani, Uchaguzi wa Oktoba Mwaka huu haukuwa kwaajili ya kushiriki na kutafuta njia ya kuvihusisha Vyama vya Siasa Serikalini, bali Dhamira Kuu ilikuwa ni kuweka Misingi ya kutafuta haki na heshima, kwaajili ya Vizazi vya sasa na baadae.

"Kwa mantiki hiyo ndugu zangu tuelewe; na hapa naomba tufahamu, kwamba safari ya kupigania haki na heshima ya Nchi yetu, sasa ndio inaanza; au sivyo", ameongeza na kuhoji Mheshimiwa Othman.

Ameeleza kwamba, pamoja na hatua ambazo wameanza kuzichukua katika kupigania haki ya Wananchi iliyoporwa katika Uchaguzi huo, Chama chake kimeamua kutumia Njia za Kistaarabu; na ikishindikana watarudi tena kuushauri umma, lipi la kufanya.

"Kwanza tumeamua kutumia mlango wa kisheria wa kufungua Kesi ya kudai haki yetu Mahak**ani", amefahamisha Mheshimiwa Othman, huku akisisitiza ahadi ya kuwashirikisha Wanachama na Wananchi katika hatua zote.

Amebainisha kwamba hatua na harakati hizo zote zinahitaji zaidi subra na mshik**ano wa makundi yote, pamoja na kusikiliza maelekezo ya Viongozi wao.

Aidha amesema kwasasa hawapo katika kujadili juu ya kuingia au kutokuingia katika Serikali ya Umoja wa Kitaifa, kwani Msingi wa yote ni khatma ya Nchi na heshima ya watu wake, pamoja na kurudisha 'ufalme' wa wananchi wenyewe.

Akitoa salamu zake kwa Wanachama, Wapenzi na Wafuasi, Makamu Mwenyekiti wa ACT-Wazalendo Zanzibar, Ndugu Ismail Jussa amesema, "nguvu moja, ahadi ya kweli na mshik**ano wa Wananchi wote wakitaraji Mamlaka ya Nchi, ni mambo yaliyopelekea kuwaduwaza watawala na vyombo vyao, hadi sasa wakiwa wanajiuliza juu ya fedheha na aibu iliyowapata, huku wakiendelea kulaumiana".

Jussa ameeleza hayo akisema, umoja, mshik**ano na kufuata maelekezo ya Viongozi, yamekuwa silaha na siri kubwa ya mafanikio, kuelekea katika ukombozi wa kweli wa Nchi, wanaouhitaji Umma wa Wananchi.

Naye, Naibu Katibu Mkuu wa ACT-Wazalendo Zanzibar, Ndugu Omar Ali Shehe, ameeleza msimamo wa Wananchi kuwa wana Mapenzi, Hamasa na Matumaini makubwa, na kwamba hawawezi kukata tamaa; wataendelea kupambania haki, wao na Viongozi wao wa ACT-Wazalendo, hadi pale haki na heshima ya Nchi ipatikane.

Baadhi ya Waliokuwa Mawakala, pamoja na Viongozi wa Majimbo ya Nungwi, Kijini, Mkwajuni, Tumbatu, Chaani, Bumbwini, Donge na Mahonda wameeleza Hadhara hiyo juu ya changamoto na namna walivyoshuhudia matukio ya uporaji wa kura na kile walichoita 'uchafuzi' wa zoezi hilo kwa ujumla, wakitaja vitisho, vipigo dhidi ya Mawakala wa upinzani, ubabaishashi wa matokeo, sambamba na Maafisa wa Tume ya Uchaguzi kuwa sehemu ya wahujumu ambao kwa kiasi kikubwa wakitokea katika Vikosi vya Serikali; namna walivyokuwa wakiingiza kura za wizi, na kukimbia na Fomu za Matokeo.

Viongozi mbali mbali wameambatana na Mheshimiwa Othman katika Hafla hiyo, wakiwemo Wenyeviti na Makatibu wa Ngazi zote za Uongozi za Mikoa hiyo ya Kichama, wakiongozwa na Katibu wa Habari na Uenezi wa ACT-Wazalendo, Ndugu Salim Bimani.

Kitengo cha Habari,
Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar
Novemba 18, 2025.

Mwenyekiti wa Taifa wa ACT-Wazalendo, Mheshimiwa Alhaj Othman Masoud Othman, leo Jumamosi, Novemba 15 2025, amejumuika n...
15/11/2025

Mwenyekiti wa Taifa wa ACT-Wazalendo, Mheshimiwa Alhaj Othman Masoud Othman, leo Jumamosi, Novemba 15 2025, amejumuika na Viongozi, Waumini wengine wa Kiislamu pamoja na Wananchi, katika Maziko ya Marehemu Sheikh Sherali Champsi, ambaye alikuwa Kiongozi wa Muda Mrefu wa Kamati ya Kitaifa ya 'Miladun-Nabiy', ya hapa Zanzibar.

Aidha, Marehemu Sheikh Sherali aliwahi-kuwa Mmoja wa Alama za Mji Mkongwe na ametumikia Taifa katika Shughuli mbali mbali zikiwemo za Polisi; Jumuiya ya Wafanyabiashara (Chamber of Commerce); na katika Taasisi za Kijamii, mathalan Jumuiya ya Ismailiya Zanzibar.

Sheikh Sherali, ambaye alifariki-dunia jana Novemba 14, amesaliwa hapo Msikiti wa Ijumaa Malindi, Sala ambayo imeongozwa na M***i Mkuu wa Zanzibar, Sheikh Saleh Omar Kaabi, na khatimaye kuzikwa katika Makaburi ya Ismailiya, huko Mwanakwerekwe, Mkoa wa Mjini-Magharibi Unguja.

Innalillahi Waina Ilayhi Raajiun. Mwenyezi Mungu Ailaze Roho ya Marehemu Mahala Pema Peponi. Amiin!

Kitengo cha Habari
Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar
Novemba 15, 2025.

15/11/2025

Wananchi Micheweni Pemba wamuombea Dua Mhe Othman Masoud

Mwenyekiti wa Taifa wa ACT-Wazalendo Mheshimiwa Alhaj Othman Masoud Othman, amewaasa Wananchi wasiwe na huzuni juu ya ya...
14/11/2025

Mwenyekiti wa Taifa wa ACT-Wazalendo Mheshimiwa Alhaj Othman Masoud Othman, amewaasa Wananchi wasiwe na huzuni juu ya yale yaliyotokea hivi karibuni Nchini, na wazingatie Ukubwa wa Rehma za Mwenyezi Mungu, wakiamini kwamba haki haipotei, na dhulma katu haikubaliki.

Alhaj Othman ameyasema hayo leo Novemba 14, 2025, alipojumuika na Waumini wenzake wa Kiislamu pamoja na Wananchi, katika Sala ya Ijumaa, hapo Msikiti wa Chamboni Micheweni, Mkoa wa Kaskazini Pemba.

Amesema, "ni dhahiri baada ya yaliyotokea wapo wengi ambao wamehuzunika na wengine kughadhibika, bali la muhimu zaidi ni kutanguliza subra na shukran kwa imani kwamba Rehma Zake Mwenyezi Mungu ni Kubwa".

Ameeleza kuwa lililoleta huzuni na masikitiko makubwa ni kuona wapo ambao wamepora mamlaka kwa njia za kughushi, hadaa na hila, licha ya kujileta mbele ya jamii wakijivika sura za imani na kujidai kuhimiza amani.

"Kwasababu waliofanya haya tunawajua hatuna- budi kuwafika na kuwaeleza ubaya wa waliyoyatenda, pamoja na kuwakataa kutokana na dhulma hiyo", amesema Mheshimiwa Othman huku akihimiza subra baina ya Wananchi, sambamba na kujenga imani kwa hikma na juhudi ambazo Viongozi wanazitekeleza katika kupambania haki zao.

Aidha ameongeza kwa kusema, "tunachoomba kwenu ni mshik**ano na subra; wakati huu tukiendelea kuitafuta haki yetu kwa njia za amani na utulivu, na Inshaallah itapatikana".

Akitoa Khutba Mbili, Khatib na Imamu wa Sala hiyo, Sheikh Shaame Mbwana Shaame, amekumbusha wajibu wa waumini kutenda wema, ili kuiepusha jamii kutokana na kila aina za uovu, unaoweza kuipoteza heshima, sasa na kwa vizazi vijavyo.

"Rehma ya Mwenyezi Mungu ipo karibu na wale watendao mema, Ndugu zangu pia utu wa mwanadamu ni kutenda wema na kuepuka kila baya; hata iwapo ni yale yanayomgusa mtu, dhidi ya mtu mwengine, katika kujinufaisha na anasa za dunia", amefahamisha Khatib huyo.

Mara baada ya Ibada hiyo Waumini wa Mskiti huo, wakiongozwa na Imamu Sheikh Ali Makame Kombo, walimuombea Dua Maalum Alhaj Othman, wakimuomba Mwenyezi Mungu Amfanyie wepesi, katika majukumu yake.

Viongozi mbali mbali wa Jamii, Dini na Siasa wamejumuika na Mheshimiwa Othman katika Ibada hiyo, wakiongozwa na Mwenyekiti wa Mkoa wa Kichama Micheweni Maalim Rashid Khalid.

Kitengo cha Habari
Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar
Novemba 14, 2025.

Mwenyekiti wa Taifa wa ACT-Wazalendo,  Mheshimiwa Othman Masoud Othman, amesema, licha ya kushuhudiwa hapa Nchini Wizi, ...
12/11/2025

Mwenyekiti wa Taifa wa ACT-Wazalendo, Mheshimiwa Othman Masoud Othman, amesema, licha ya kushuhudiwa hapa Nchini Wizi, Ubadhirifu na Dhulma kubwa ya waziwazi katika Uchaguzi Mkuu wa hivi karibuni, Zanzibar imeweza kuepuka Maafa na Machafuko, kutokana pia na busara za Viongozi Wakuu wa Chama hicho.

Mheshimiwa Othman ameyasema hayo leo Jumatano Novemba 12 2025, alipofanya mazungumzo na Viongozi wa Kamati za Uongozi, Ngazi za Majimbo, Matawi na baadhi ya Mawakala, wa Chama chake, kwa Mkoa wa Kichama wa Wete Pemba.

Akizungumza pia na Mamia ya Wafuasi wake hao, waliojitokeza kumsikiliza hapo Ukumbi wa Istiqama Mjini Wete, Mheshimiwa Othman ambaye alikuwa Mgombea wa Nafasi ya Urais wa Zanzibar kupitia ACT-Wazalendo, katika Uchaguzi Mkuu wa hivi karibuni, ameeleza kwamba Chama hicho kimefanya kila iwezekanavyo kuepusha machafuko na mauaji yasitokee, ili kulinda maslahi ya Taifa zima.

"Alhamdulillahi yote haya tuliyapambania kutokana na busara na uoni wa mbali wa Viongozi wa Chama chetu, tukijua kwamba watawala wanaopapia madaraka wao wanachoamini ni vurugu, ghilba, fujo na wizi, hata iwapo watagharimu damu na maisha ya watu wasiokuwa na hatia", amesema.

Ameongeza kwa kusema, "tuliwambia Inshaallah sisi hatutoingiza watu barabarani, bali Mwenyezi Mungu Mwenyewe Ndiye Ataingia Barabarani; naam! Akaidhihirisha fedheha ya mipango yao madhalimu"..

Ameeleza kuwa yeye na Chama chake wamesikitishwa mno na Machafuko yaliyotokea katika maeneo mbali ya Tanzania Bara, ambayo yalisababisha maafa makubwa ya watu na mali, licha ya kwamba kwa kiasi kikubwa hayo yalipangwa yatokee dhidi ya Wananchi wa hapa Visiwani, Unguja na Pemba.

"Binafsi tuliwafuata Watawala na Viongozi Wakuu wote tukawaambia 'halahala mti na macho... ', hayo mambo yasitokee kwani tulikwishabaini mipango ya kuleta maafa na mauaji kwa makusudi ikiandaliwa", amesema Mheshimiwa Othman akiekeza Hatua ambazo yeye na Viongozi wenzake wa Chama chake walizichukua, ili kuepusha vurugu, kabla na baada ya Uchaguzi Mkuu huo wa Oktoba Mwaka huu.

Amefahamisha kuwa yote hayo ni kutokana na ukweli wa maandalizi yaliyokuwepo, yakiwemo ya Maelfu ya Askari, Vikosi na Majeshi walioletwa Zanzibar, wakiwa na Silaha za Hatari, ili kuwaangamiza Wazanzibari, k**a ambavyo wamekuwa wakitekeleza kila mara.

"Kwa hili Ndugu zangu, hatuna sababu ya kusikitika wala kuhuzunika, kwani mradi wao haukuwa; badala yake pamoja na uhuni, uporaji na dhulma waliyotenda, bado walitamani kuleta maafa: ingawa hatimaye tumevuka salama; hivyo tembeeni kifua-mbele, mkiamini sisi ni washindi", ameeleza.

Aidha ametoa mwelekeo wa Chama chake akisema kuwa 'safari ya mapambano ya kupigania haki ya wananchi iliyoporwa, bado inaendelea'.

Ametaja hatua za sasa kuwa ni pamoja na Kufungua Kesi Mahak**ani ili kudai Ushindi wa Chama hicho, katika Majimbo yote ya Uchaguzi yaliyoporwa.

Akijibu kauli za baadhi ya watu wanaohoji kwanini Wajumbe wa Chama hicho wameingia katika Baraza la Wawakilishi la Zanzibar, na huku kilichotendeka ni dhulma ya waziwazi, na k**a kwamba ni kuhalalisha ubadhirifu huo, au kuukubali uchaguzi uliojaa ghilba na wizi, Mheshimiwa Othman amesema, "ACT-Wazalendo haiwezi kuukubali uhuni uliotendeka, bali vita yoyote inahitaji maarifa na mbinu".

Kuhusu iwapo wataingia katika Kuongoza Serikali ya Umoja wa Kitaifa, Mheshimiwa Othman amesema, "iliyodhulumiwa na iliyosalitiwa ni haki na maamuzi ya Wananchi wote, kwani iliyoporwa ni haki na Sauti yao ya Demokrasia; ingawa si hayo tu bali pia imeibwa heshima ya Nchi nzima".

Amelaumu ile ambayo ameiita tabia mbaya ya kuwahusisha vijana wadogo wasiostahiki katika Wizi wa Kura, kupitia Uchaguzi huo, sambamba na baadhi ya Watu wenye Dhamana za Uongozi Serikalini, wakiwemo Askari, Vikosi vya Ulinzi na Usalama, Mawaziri, Makatibu Wakuu, Wakuu wa Mikoa na Wilaya, ambao pia walishuhudiwa wakipora haki na sauti hiyo kubwa ya Demokrasia, ndani ya Nchi hii.

"Uchaguzi ulivyofanyika ndugu zangu, ni k**a kwamba tulivamiwa na Majizi, Majambazi, Mafiya wa Dawa za Kulevya, kwa namna ambavyo wakipapatika bila aibu wala heshima, wakiiba kura ili kuwaweka baadhi ya Watu wao madarakani".

Amesema la kushangaza ni kuona Wahalifu na Wezi hao, wakiwekewa mazingira kuwa Mawaziri na Viongozi wa Ngazi za Juu Serikalini.

Hivyo, amesema mwelekeo wa sasa ni kuipambania haki ya wananchi iliyoporwa, kwa nguvu zote, ikibidi waliotenda jinai na dhulma yote wawajibishwe; na wala mjadala siyo kuingia au kutoingia Serikalini.

Amewahimiza Wafuasi wake na Wananchi kwa ujumla, waendeleze subra, umoja na mshik**ano; wasichokozeke, wakiamini juu ya nguvu, hikma na juhudi za Viongozi wao katika kupigania haki yao hiyo.

"Hakuna wakati ambao tunahitaji subra, umoja na mshik**ano, huku tukimtegemea Mwenyezi Mungu kwa udhati k**a sasa; na hivyo mtuamini Viongozi wenu, na wala msikubali kuchokozeka kwa hali yoyote; hatutopoa, na wala hatupoi, hadi pale ambapo Haki ya Wananchi iliyoporwa irudishwe; na hatutosimama hadi Safari iishe; hapa imetosha, basi", amefahamisha.

Akitoa shukrani za Chama hicho kwa Wanachama, Wapenzi na Wafuasi, Makamu Mwenyekiti wa ACT-Wazalendo Zanzibar, Ndugu Ismail Jussa, amesema Ushindi ambao Chama chake kiliupata, siyo tu kwamba umesadifu umoja na mshik**ano walioutamani, bali wameuonesha Ulimwengu, mwelekeo wa Njia Mpya ya Ukombozi wa Zanzibar.

Naye, Naibu Katibu Mkuu wa ACT-Wazalendo Zanzibar, Ndugu Omar Ali Shehe, pamoja na Mwenyekiti wa Mkoa wa Kichama wa Wete, Ndugu Juma Khamis Ali, wamebainisha Matumaini ya Wazanzibari wote, kwamba ni kuiona haki ambayo ni dhahiri imepokwa, ikirudi mikononi kwa Umma ambao kwa kiasi kikubwa, walikichagua Chama hicho.

Aidha Viongozi wa majimbo ya Wete, Pandani, Mtambwe, Kojani, na Gando wameeleza changamoto na namna walivyoshuhudia matukio ya uporaji wa kura na 'uchafuzi' wa zoezi hilo la kidemokrasia kwa ujumla, wakitaja vitisho, vipigo dhidi ya Mawakala wa upinzani, sambamba na Maafisa wa Tume ya Uchaguzi, ambao kwa kiasi kikubwa wakiwa ni kutoka Vikosi vya Serikali, jinsi walivyokuwa wakiingiza kura za wizi, na kukimbia na Fomu za Matokeo, na pia Masanduku ya Kura.

Huo ni Muendelezo wa Ziara ya Kikazi Ya kichama ambayo Mheshimiwa Othman amendelea nao Kisiwani Pemba, baada ya Uchaguzi Mkuu uliopingwa na kulaumiwa, kwamba uligubikwa na wizi na uporaji, Ndani na Nje ya Tanzania.

Viongozi mbali mbali wameambatana na Mheshimiwa Othman katika Hafla hiyo, wakiwemo Wenyeviti, Makatibu wa Majimbo na Matawi, wakiongozwa na Mratibu wa Chama hicho Pemba, Ndugu Rashid Ali Abdallah.

Kitengo cha Habari,
Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar
Novemba 12, 2025.

Ahadi ya Mheshimiwa Othman kwa Wananchi wa Pemba.
11/11/2025

Ahadi ya Mheshimiwa Othman kwa Wananchi wa Pemba.

Mwaka wa Kuinusuru Zanzibar

Mwenyekiti wa Taifa wa ACT-Wazalendo, ambaye  alikuwa Mgombea wa Nafasi ya Urais wa Zanzibar kupitia Chama hicho katika ...
11/11/2025

Mwenyekiti wa Taifa wa ACT-Wazalendo, ambaye alikuwa Mgombea wa Nafasi ya Urais wa Zanzibar kupitia Chama hicho katika Uchaguzi Mkuu wa hivi karibuni, Mheshimiwa Othman Masoud Othman, leo Jumanne Novemba 11 2025, amefanya mazungumzo na Viongozi wa Ngazi mbali mbali wa Mkoa wa Kichama wa Micheweni Kisiwani Pemba, ili kujadili Matukio yaliyojiri Nchini, katika Zoezi hilo la Kitaifa.

Kikao hicho ambacho ni muendelezo wa Ziara yake kisiwani Pemba, na kilichowajumuisha Viongozi wa Kamati za Uongozi wa Ngazi za Mkoa, Majimbo, Matawi, pamoja na waliokuwa Mawakala, kwa Mkoa huo wa Kichama, kimefanyika hapo Ukumbi wa Sadam, Jimbo la Micheweni, ambapo pia Kimesikiliza Taarifa za Ushahidi wa baadhi ya Matukio yaliyojitokeza katika Mchakato wote wa Uchaguzi, sambamba na kupokea Maagizo ya Chama.

Katika Kikao hicho, Mheshimiwa Othman ambaye ameambatana na Mke wake, Mama Zainab Kombo Shaib, pamoja na Viongozi Waandamizi wa chama hicho, amepokea Ripoti za kile Wajumbe walichokiita 'Uchafuzi' wa Uchaguzi Mkuu, kwa Majimbo Manne (4) ya Mkoa wa Kichama wa Micheweni.

Kitengo cha Habari,
Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar
Novemba 11, 2025.

Mwenyekiti wa Taifa wa ACT-Wazalendo na Aliyekuwa Mgombea wa Nafasi ya Urais wa Zanzibar kupitia Chama hicho katika Ucha...
10/11/2025

Mwenyekiti wa Taifa wa ACT-Wazalendo na Aliyekuwa Mgombea wa Nafasi ya Urais wa Zanzibar kupitia Chama hicho katika Uchaguzi Mkuu wa hivi karibuni, Mheshimiwa Othman Masoud Othman, leo Jumatatu Novemba 10 2025, amefanya mazungumzo na Viongozi wa Ngazi mbali mbali wa Mkoa wa Kichama wa Chake Chake Kisiwani Pemba, ili kujadili yaliyojiri Nchini, katika Zoezi hilo la Kitaifa.

Kikao hicho ambacho kimewajumuisha Viongozi wa Kamati za Uongozi wa Ngazi za Mkoa, Majimbo, Matawi, pamoja na waliokuwa Mawakala wao, kwa Mkoa huo wa Kichama, kilikuwa na Ajenda ya Kusikiliza Taarifa juu ya Matukio yaliyojitokeza katika Mchakato wote wa Uchaguzi, sambamba kupokea maagizo ya Chama, kimefanyika hapo Ukumbi wa Kwale, Jimbo la Ziwani.

Wakielezea baadhi ya changamoto walizokutana nazo katika Siku ya Uchaguzi ya Tarehe 29 Oktoba (na Tarehe 28 Siku ya Kura ya Mapema) Mawakala, Waangalizi, na
Viongozi wa Chama hicho wamesema, kilichojiri ni wizi, uporaji, uchafuzi na hujuma za wazi wazi, dhidi ya maamuzi, haki, ridhaa na sauti kubwa ya umma, ndani na nje ya masanduku ya kura.

Wakieleza hayo, kwa niaba ya Wahusika wengine na kwa nyakati tofauti, Bw. Khamis Mselem Ali wa Tibirinzi, Bw. Saleh Abdurahman wa Chonga, na Bw. Said Omar wa Ole, wameeleza kuwa watu wengi waliokuja kupiga kura siyo ambao walikuwemo ndani ya Daftari la Kudumu la Wapigakura wa Vituo-husika; bali ni mapandikizi na mamluki kutoka maeneo mengineyo, ambao hawakustahiki.

"Waliopiga-kura walipatiwa rundo la karatasi za kura kuanzia tano, kumi, ishirini, mia na zaidi; na pindipo tukihoji ama kuzuia ubadhirifu na uchafuzi huo, tulitishiwa-uhai wetu kwa mtutu wa bunduki, vipigo, tulikuwa tunatolewa nje ya Vituo kwa nguvu, huku Askari wakiangalia tu bila ya hatua yoyote", amesimulia Bw. Kassim Omar wa Michakaini ambaye alikuwa miongoni mwa Mawakala hao.

"Tulishuhudia wasimamizi wa Uchaguzi katika vituo wakizipiga wao kura na kuzijaza katika masanduku ya kura, lakini kubwa tulinyimwa hata fursa ya kuhesabu kura pamoja na kunyimwa fomu za matokeo na vituo vingi kura hazikuhesabiwa kabisa", amesimulia Bi Asha Mohamed, mkaazi wa Pondeani.

"Tulishuhudia Wasimamizi wa Kura wakitoroka na Fomu za Matokeo, na pia Masanduki ya Kura yakiwa wazi; tulipojaribu kuwafuata, walitutisha kwa bunduki, na wakatuambia ambaye anataka kifo ajaribu kufuatilia", ameeleza Bimkubwa Ali, mkaazi wa Chake Chake Mjini.

Miongoni mwa Mawakala hao, aliyejitambulisha kwa jina la Bakari Juma wa Vitongoji amesema, " tulichoshuhudia Mheshimiwa ni hujuma za kusikitisha kabisa; hawa Vikosi na Bunduki zao walitutisha ili tumuache Msimamizi ajaze Mamia ya Kura katika Sanduku; na hata Mgombea wa Jimbo langu alipokuja na yeye aliambiwa hana haki aondokea, au atakiona cha- moto".

"Tuliyoyashuhudia itafika kesho hatuyamalizi Mheshimiwa, maana ni wizi wa mchana-kweupe haijawahi kutokea; Magari ya Serikali tunayajua, yalikuja yamejaza watu wasiostahiki, walikuwa wakimimina kura watakavyo kuwatilia Wagombea wa CCM, hasa pale baada ya muda wa mwisho wa kupiga kura", ameeleza Bw. Said Rashid, mkaazi wa Ziwani.

Katika salamu na shukran zake mbele ya Viongozi hao, pia akizungumzia changamoto hizo, Mheshimiwa Othman amesema Lengo Kuu la Chama hicho siyo kupigania Nafasi za Kuongoza katika Serikali ya Umoja wa Kitaifa, bali ni kujenga mustakbali mwema wa Nchi, ambao ni wa kudumu, kwaajili ya Vizazi vya sasa na baadae.

Amesema, Mikakati ya Chama hicho na msimamo wa sasa wa Viongozi wake, ikitanguliwa na subra, ni katika njia inayopelekea kuiokoa Nchi ibaki na amani na Utulivu, licha ya dhulma kubwa iliyoshuhudiwa, ili khatimaye kuhakikisha Dhamira hiyo inafikiwa.

Amesema lengo siyo kuongoza Serikali ya Umoja wa Kitaifa, kwa mtindo ule wa 'kufunika kombe', bali ni kutafuta suluhisho la kudumu litakaloinyoonsha Nchi na kuielekeza katika khatma njema, na ikibidi hata kuepukana na Chaguzi zilizojaa vitisho, machafuko, umwagaji wa damu, wizi na hujuma za kila aina.

"Ndugu zangu nataka niwaambie kwamba hiki siyo Chama cha Uchaguzi, wala cha kutafuta nafasi katika Serikali ya Umoja wa Kitaifa, bali Dhamira yetu ni kuendeleza harakati za kupigania kujenga Mustakbali mwema wa Nchi utakaojali maslahi na heshima ya kila mtu, kwaajili ya maisha bora, sasa na hapo baadae", amesema.

Aidha, ameongeza kwa kusema, "Viongozi na Waasisi wa Nchi waliongoza wakaleta Mapinduzi, wakatunga Katiba na Miongozo mbali mbali ili kuleta muafaka, hadi kufikia kuwepo Serikali ya Umoja wa Kitaifa, baada ya kushuhudia na kisha kuchoshwa na mauwaji, mateso na madhila kwa wananchi; na khatimaye wakasema hayo hayana nafasi tena katika kuongoza Nchi ya Watu Wastaarabu, k**a Zanzibar na Tanzania kwa ujumla".

"Sasa iweje leo yatumike Mamilioni ya Fedha za Wananchi kuitisha Uchaguzi uliojaa vituko, hila, hujuma na wizi, almuradi ili mtu fulani awepo madarakani, hata iwapo Umma umemkataa; kwetu sisi hili halikubaliki katu", ameongeza Mheshimiwa Othman.

Akisisitiza Msimamo wake, Viongozi, na Chama chake kwa ujumla, baada ya kile alichotaja kuwa 'uhuni mkubwa wa Uchaguzi', nakwamba hawako-tayari kuingia Serikalini na kuongoza pamoja na Watu waliopora Haki, Demokrasia na Heshima ya Wananchi walio-wengi, Mheshimiwa Othman ameeleza kuwa kilichopita katika Matukio yote hayo ni 'Awamu ya Kwanza', na sasa kilichopo ni kuipigania Haki ya Umma Mkubwa walioshirikiana kumchagua na kumpigia-kura yeye na Wenzake.

"Lengo letu ilikuwa kuwafikia Wazanzibari wote, kuomba tuwe pamoja na tuungane katika kuyafikia Malengo ya Kuinusuru Zanzibar; na haya yote tumefanikiwa kuyafikia; kilichosalia naomba mtuamini ili tukamilishe hatua iliyobaki", ameeleza Mheshimiwa Othman.

Amekiambia Kikao hicho kwamba wao siyo Watu wa vurugu wala wa- purukushani, bali yeye, Wafuasi wa Chama chake, na Wazanzibari waungwana wote ni waumini wa amani na watetezi wa Nchi na Maendeleo endelevu yasiyokuwana vitisho.

Aidha amesema kutokana na Takwimu Sahihi ambazo Chama chake, pamoja na vyanzo vyao mbali mbali vya kuaminika, kabla Matokeo ya Kura hayajapinduliwa, walikwishajizolea Ushindi wa Nafasi ya Urais wa Zanzibar kwa zaidi ya Asilimia 70; na pia Majimbo 32 kwa Viti vya Ubunge na Uwakilishi, Unguja na Pemba.

Amefahamisha kuwa kutokana na uhakika na ushahidi juu ya ushindi huo, Chama chake pia kimechukua HATUA YA KUFUNGUA KESI MAHAKAMANI ili kudai MAJIMBO HAYO ambayo ACT-Wazalendo walishinda.

"Ndiyo maana hata Wazee wetu waliokuwa Watawala na Wakuu wa Nchi hii wameniita wakaniambia "WEWE PAMOJA NA WAFUASI WAKO WOTE HONGERENI SANA! MUAMINI KILICHOIBWA NI 'FURNITURE' TU, BALI NYUMBA IPO SALAMA NA HESHIMA IPO PALE PALE", amebainisha Mheshimiwa Othman.

Ameeleza kuwa yeye na Viongozi wenzake walikuwa-nazo taarifa kamili juu ya maandalizi na mipango ya hujma na machafuko, ikiwemo ya mauaji dhidi ya wananchi wasiokuwa na hatia, bali kwa Qadar Yake Mwenyezi Mungu, Dua nyingi na hekima kubwa, yalipelekea kuinusuru Nchi hii kutokana na majanga hayo.

"Kwahivyo sisi tunachotafuta ni jambo ambalo litakuwa na Maslahi ya Nchi kwa muda mrefu pamoja na Wananchi wake; na wala siyo Maslahi ya wachache, au Maslahi ya ACT- Wazalendo", amesisitiza Mheshimiwa Othman akiwakumbusha Wanachama na Wafuasi wake kwamba hiyo ndiyo imekuwa SILAHA MUHIMU YA USHINDI WAO.

Hivyo pia, katika mnasaba wa msimamo wa Chama hicho baada ya 'hujuma za Uchaguzi', Mheshimiwa Othman amehimiza umoja na mshik**ano, na pia kupokea TAARIFA RASMI KUTOKA KWA VIONGOZI, na wala siyo 'maburungutu' ya upotoshaji yenye dhamira mbaya ya kuwagawa na kuwavunja-moyo.

Kwa upande wake, Makamu Mwenyekiti wa ACT-Wazalendo upande wa Zanzibar, Ndugu Ismail Jussa amesema yaliyotokea na vitisho vinavyoendelea ni kielelezo kwamba Wazanzibari wamemkubali na kumsikiliza Mheshimiwa Othman na Chama chake.

"Kiongozi wetu alitutaka tuungane na tumeungana; ametutaka tudumushe amani na hali inaonekana; Nchi ipo salama, na sasa ametuambia anaendele kupigania haki yetu nasi sote tunasema tuko pamoja naye na tutaipata haki ya nchi yetu Inshaallah", ameeleza Jussa huku akisisitiza kwamba Mheshimiwa Othman ndiye Chaguo na Mkombozi wa Kweli wa Visiwa hivi.

Naye, Naibu Katibu Mkuu wa ACT-Wazalendo Zanzibar, Ndugu Omar Ali Shehe, pamoja na Mwenyekiti wa Mkoa wa Kichama wa Chake Chake, Ndugu Yussuf Salim Khamis, wamesema, Wanachama wa Mkoa huo, na Wazanzibari kwa ujumla, wapo tayari kuungana na Kiongozi wao huyo katika mapambano ya kuitafuta haki yao iliyoporwa.

"Mheshimiwa hili kwetu halijaisha, na tunakuhakikishia hatujachoka na tunaendelea kupambania haki yetu", ameeleza Nd. Omar.

Viongozi mbali mbali wameambatana na Mheshimiwa Othman katika Hafla hiyo, wakiwemo Wenyeviti, Makatibu wa Majimbo na Matawi, wakiongozwa na Mratibu wa Chama hicho Pemba, Ndugu Rashid Ali Abdallah.

Kitengo cha Habari,
Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar
Novemba 10, 2025.

Mwenyekiti wa Taifa wa ACT-Wazalendo Mheshimiwa Alhaj Othman Masoud Othman, amewahimiza Wananchi, na hasa waumini wa din...
07/11/2025

Mwenyekiti wa Taifa wa ACT-Wazalendo Mheshimiwa Alhaj Othman Masoud Othman, amewahimiza Wananchi, na hasa waumini wa dini ya Waislamu kuzingatia Misingi ya Malezi ya Kiimani, katika kulinda amani na ustawi wa Jamii, ili kulinusuru Taifa.

Alhaj Othman ameyasema hayo leo Novemba 07, 2025, alipojumuika na Waumini wenzake wa Kiislamu pamoja na Wananchi, katika Sala ya Ijumaa, hapo Masjid Mwitani, Msikiti uliopo Mtemani Wete, Mkoa wa Kaskazini Pemba.

Mheshimiwa Othman ameiambia Hadhira hiyo kubwa iliyojitokeza hapo, na ambayo imemuomba atoe Salamu zake, hasa baada ya Uchaguzi Mkuu wa hivi karibuni, kwamba kilichotokea ni dhahiri Watu wenyewe Wazanzibari, wakiwemo Vijana wadogo, walitumiwa kuhujumu haki, nje ya Miongozo na Misingi ya Dini ya Kiislamu.

"Mnapokubaliana na mkaweka Miongozo yenu k**a Binaadamu Wastaarabu, hata k**a haipo ndani ya Msahafu, pindipo wakitokea Watu wakaikiuka, hiyo inakuwa ni dhulma, na Mwenyezi Mungu katu Haikubali", amesema Mheshimiwa Othman akieleza yale yaliyotendeka yakiwemo ya kupora Uchaguzi Mkuu wa hivi karibuni Nchini kote.

Amefahamisha kwamba takriban Chaguzi zote zilizotangulia hapo kabla, palishuhudiwa Watu walioongoza hujuma na mauaji, kwa kiasi kikubwa walitokea nje ya Zanzibar, bali uporaji wa mara hii uliwahusisha, wenyewe- kwa-wenyewe kutoka Unguja na Pemba.

"Moja, kubwa ambalo tumelipata mara hii, Mwenyezi Mungu Ametubainishia kuwa hujuma na uovu wameutenda wenyewe Ndugu zetu, Watoto wetu, Kaka zetu, Ami zetu, Shangazi zetu au Dada zetu, kutoka hapa hapa kwetu", amesema.

Amesema, laiti k**a Jamii hii ambayo Viongozi wake kwa asilimia kubwa ni Waislamu, wangelisimamia kwa kufuata Miongozo ya Haki, Imani na Malezi yenye Maadili, ingelikuwa ajabu kuona dhulma na hujuma za kiutawala, wanazokutana-nazo wananchi wasiokuwa na hatia, zikitendeka mfululizo kiasi cha kuushangaza Ulimwengu hata kwa Wasiokuwa-Waislamu.

"Ifike hatua katika Nchi yetu hii, zikifika nyakati za uchaguzi kusiwe na hofu, mashaka, wasiwasi wala taharuki", ameeleza Alhaj Othman akihimiza umuhimu wa amani ya kweli hapa Nchini.

Amebainisha kwamba, tatizo kubwa ni kutofuata Miongozo ya Dini, Imani, Malezi, pamoja na Mafundisho ya Mtume Muhammad (SAW); na badala yake baadhi ya Watawala kuzingatia mno maslahi binafsi ya kidunia, huku akisema kinachoonekana sasa ni "ukimya wa khofu, na siyo amani".

Aidha, Mheshimiwa Alhaj Othman amebainisha kwamba kilichotokea katika Uchaguzi huo, yanapaswa kuleta mazingatio ya kiimani, na wala siyo ya kufumbiwa-macho, kwa kile kinachoonekana ni amani ya woga.

Aidha amefahamisha kwamba, kinachotakiwa ni kutafutwa suluhisho la kudumu ili kuwa na utulivu, haki na amani ya kweli, inayojali malezi na maadili bora, hasa kwa vijana na vizazi vijavyo.

Hivyo, Mheshimiwa Othman ametahadharisha mwenendo huo, ambao amesema unazalisha 'uheshimiwa na waheshimiwa wa kinafiki', huku Wananchi katika nyoyo zao wakiamini kwamba Vyeo hivyo 'ni feki', vimepatikana kwa njia na misingi ya batili, dhulma na haramu.

Pamoja na yote hayo, Mheshimiwa Othman amerudia ahadi yake kwamba, yeye na Viongozi wenzake, ambao Umma Mkubwa wa Wananchi wengi uliwachagua kwa kuwapigia kura nyingi za Ushindi, kupitia Uchaguzi Mkuu wa hivi karibuni, watahakikisha wanapigania na kutetea haki hiyo iliyoporwa, kwa njia zote za hikma, na ili khatimaye kujenga Misingi ya Amani ya Kweli na ya Kudumu, kwa maslahi ya Taifa zima.

Akitoa Khutba Mbili, Khatib na Imamu wa Sala hiyo, Sheikh Ali Abdi Abeid, amesisitiza haja ya Waumini wa Kiislamu kuwa na Subra na kutokukata tamaa, hasa katika mitihani na utafutaji wa haki, kwani kufanya hivyo ni miongoni mwa Madhambi Makubwa, na pia kukengeuka Misingi ya Dini ya Kiislamu.

Khatib huyo amesisitiza akisema, "Qur-an Tukufu imetuhimiza tusikae kimya katika kupinga dhulma; tusichoke katika kutetea haki zetu; tusikate tamaa na Rehma za Allah; wala tusichupe Mipaka Yake tunapopata neema au tunapoamua kulipiza kisasi".

Viongozi mbali mbali wa Jamii, Dini na Siasa wamejumuika na Mheshimiwa Othman katika Ibada hiyo, wakiongozwa na Makamu Mwenyekiti wa ACT- Wazalendo Zanzibar, Ndugu Ismail Jussa; wakiwemo pia Mratib wa Chama hicho Kisiwani Pemba, Ndugu Rashid Ali Abdalla; pamoja na Mwenyekiti wa Mkoa wa Kichama wa Wete, Ndugu Juma Khamis Ali.

Mara baada ya Ibada hiyo Alhaj Othman amewatembelea, kuwajulia-hali na kubadilishana mawazo na Masheikh Mashuhuri wa Mji wa Wete, wakiwemo Sheikh Rashid Hamad Othman wa Utaani; Sharif Ghazal Abdalla wa Selemu; na Dokta Issa Said Mohamed wa Mtemani.

Kitengo cha Habari
Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar
Novemba 07, 2025.

Address

Zanzibar

Website

Alerts

Be the first to know and let us send you an email when Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais Zanzibar posts news and promotions. Your email address will not be used for any other purpose, and you can unsubscribe at any time.

Share