16/08/2026
BPRA Yatoa Elimu ya Usimamizi wa Mirathi kwa Wasiokuwa Waislamu
Ofisi ya Wakala wa Usajili wa Biashara na Mali Pemba (BPRA) imeendelea na ziara za kutoa elimu kwa jamii, ambapo safari hii imetembelea Kanisa la Roman Catholic lililopo Kizimbani, Wete Pemba, kwa lengo la kutoa elimu kuhusu usimamizi wa mirathi kwa wasiokuwa Waislamu pindi mmiliki wa mali anapofariki.
Katika ziara hiyo, Mratibu wa BPRA Pemba, Ndg. Mohammed Ali Maalim, alitoa ufafanuzi kuhusu umuhimu wa kusajili mali na biashara zote zinazomilikiwa, akisisitiza kuwa uwasilishaji wa mirathi ni hatua muhimu katika kulinda haki na umiliki wa mali.
Naye Msaidizi Mrajis Nyaraka BPRA Zanzibar, Ndg. Khamis Haji Bakar, alitoa ufafanuzi kuhusu taratibu zinazofuatwa katika usimamizi wa urithi wa mali kwa wasiokuwa Waislamu. Aidha, aliwataka waumini kufika katika ofisi za BPRA zilizopo Unguja na Pemba ili kuziwasilisha mali zao kwa mujibu wa sheria na taratibu zilizowekwa.
Kwa niaba ya waumini wa Kanisa la Roman Catholic lililopo Wete Pemba, Makamo mwenyekiti wa Parokia kanisa la Roman Catholic Nd. Innocent Selle aliishukuru BPRA kwa kuwafikishia elimu hiyo, akieleza kuwa waumini wengi hawakuwa na uelewa wa kutosha kuhusu taratibu za usimamizi wa mirathi ya mali kwa wasiokuwa Waislamu.
BPRA — Usajili Wetu, Safari ya Mafanikio Yako.